Saturday, June 12, 2010

Waja kisha huondoka

Si wa kutumainia, Waja kisha huondoka,
Hao ni wapita njia, sio watu wa kukaa,
Wana lao wanajua,lako hawewezi shika,
Waja kisha huondoka, sisi ni wapita njia.


Wanatalii dunia, uwezo wameushika,
Kila wakikuchekea, ni kicheko cha dhihaka,
Hawatakusaidia, hapo ulipo kunyanyuka,
Waja kisha huondoka, sisi ni wapita njia.


Mbwata matako hulia, wakiapta cha kushika,
Sinema kwao dunia, hutazama wakacheka,
Na wao kufurahia, neema walizodaka,
Waja kisha huondoka, sisi ni wapita njia.


Katu hautoingia, katika yao hakika,
Hesabu imetimia, wewe hawajakuweka,
Wewe ni wa kutumiwa, sio wa kutajirika,
Waja kisha huondoka, sisi ni wapita njia.


Hawa ukishawajua, vizuri utajiweka,
Kaa huku watambua, wewe kwao ni wahaka,
Chombo kinachotumiwa, mali zikazalishika,
Waja kisha huondoka, sisi ni wapita njia.


Wafaa hukusifia, na vilivyo kukupika,
Ili uwe manufaa,watakapo wakafika,
Na mengi hukuachia, ili wewe kuridhika,
Waja kisha huondoka, sisi ni wapita njia.


Ila kaa ukitambua, kwa mtu kma kiraka,
Hubanduliwa tambaa, au nguo kuchanika,
Na hivyo ikishakuwa, hutupwa kwenye majaa,
Waja kisha huondoka, sisi ni wapita njia.


Niongoze ya -Jalia, kwa changu nikanyanyuka,
Hapa nilipofikia, naomba zaidi kuvuka,
Inifae hii njia, kizazi changu kushika,
Waja kisha huondoka, sisi ni wapita njia.

No comments: