Thursday, April 26, 2012

Msiba tulio nao



Tunalia Tanzania, msiba umeingia,
Nchi sasa inaliwa, nzige wameshaingia,
Hakuna kinachobakia, jangwa yote imekua,
Msiba tulio nao, ni msiba wa taifa !

Wenye meno wanajaa, hadi mifupa watwaa,
Kazi ni kujitafunia, na sio kuhudumia,
Huliwa kisicholiwa, haramu hawajaijua,
Msiba tulio nao, ni msiba wa taifa !

Kwa ukubwa kuupewa, leseni wamechukua,
Halali imeshakua, hata wizi kutumia,
Haraka wapigania, kileleni kwenda kaa,
Msiba tulio nao, ni msiba wa taifa !

Ubepari ninalia, nchi umeshaiumbua,
Haya zimetukataa, ni aibu zinajaa,
Kila ukiangalia, nusura sijaijua,
Msiba tulio nao, ni msiba wa taifa !

Vijana waliokuwa, tayari mabilionea,
Njia walizotumia, zote mashaka zajaa,
Na wakubwa wanajua, sijui wamegaiwa?
Msiba tulio nao, ni msiba wa taifa !

Wenzangu Watanzania, ni wote tunaumia,
Daima nanyi nitakua, haki yetu kutetea,
Moto tukiwaashia, kuzimwa haitakuwa,
Msiba tulio nao, ni msiba wa taifa !

Shetani keshawaingia, nchi hawataifaa,
Yao wajitafutia, wao na zao jamaa,
Sasa kilichobakia, ni fatwah kujaitoa,
Msiba tulio nao, ni msiba wa taifa !

Na laana kuwaachia, wao na vizazi vyao pia,
Pasiwe watapotia, mguu salama wakawa,
Na kikubwa kinachokuwa, kidogo kikaishia,
Msiba tulio nao, ni msiba wa taifa !

Uchungu wasiokuwa, uzazi hawajaujua,
Miioyo iliyovia, yabisi imeshajaa,
Hakuna kutumainia, zuri kuja kutokea,
Msiba tulio nao, ni msiba wa taifa !

Yarabi nakulilia, watu wangu wapotea,
Ni usiku umekua, na hawaioni njia,
Tushushie zako taa, nuru kutuangazia,
Msiba tulio nao, ni msiba wa taifa !

Al-jumaa 27-04-2012
Zanzibar. Tanzania.

Heri kuzaliwa ng'ombe Ulaya

Heri kuzaliwa ng'ombe Ulaya,
Kuliko ya mtu kwetu Afrika,
Vijana wetu wananiambia,
Nao ujumbe umekwishafika!

Heri kuzaliwa ng'ombe Ulaya,
Ni nini walichokifikiria;
Hadi kama hayo wametamka ?
Udhia uongozi ulokuwa ?

Heri kuzaliwa ng'ombe Ulaya,
Lazima na mimi kuulizia,
Majibu yangu si ya uhakika,
Ila kuna walakini ninajua !

Heri kuzaliwa ng'ombe Ulaya,
Vipimo vipya ukivitumia,
Kila kitu sasa kinatupwaya,
Bado vya watoto tunavivaa?

Heri kuzaliwa ng'ombe Ulaya,
Na kusoma yawe yaeleweka,
Wengi wetu hatujajitambua,
Uvivu watu umetujaa!

Heri kuzaliwa ng'ombe Ulaya,
Ng'ombe huko anatunzika,
Na virutubisho pia  hupewa,
Kwa ubora nyumba zinajengeka!

Heri kuzaliwa ng'ombe Ulaya,
Hospitalini atibika,
Kwenye gari pekee anakaa,
Wala hakuna kudhulumika!

Heri kuzaliwa ng'ombe Ulaya,
Afrika hayatofanyika,
Umasikini waupalilia,
Hili ndilo bara la wastahika !

Heri kuzaliwa ng'ombe Ulaya,
Hili ndilo bara la wastahika !
Tayari waliokwishakupotea,
Na safari wala haijaanzika!


Milionea tungekuwa

Ndio wanaochochea, uroho nayo tamaa,
Kama mvuvi kuvua, bila nyavu kutumia,
Na kulima asojua, akavuna na kupaa,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !

Vijana wawahadaa, tena kisaikolojia,
Kamari imeshakua, jina lake inafaa,
Na wakubwa walokuwa, nuksi hawajaijua,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !

Imani zatuvunjia, na vijana kupotea,
Na vichaa walokuwa, kazi wanazikimbia,
Na idadi tunajua, mia haitafikia,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !

Matangazo ni balaa, tivii na redio pia,
Ovyo zinavyotumiwa, ni ila imeingia,
Na kula anayejua, wana atawaambia,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !

Vilio zitatutia, pasiwe pa kukimbilia,
Wanyonge tunanyolewa, kidogo tulichopewa,
Na wkubwa wanajaa, matumbo kuwalegea,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !

Uhuni umeingia, kucheza nazo ruia,
Na rahisi walokuwa, vijana wahusudiwa,
Ujinga waliojaa, ktuokana nayo njaa,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !

Milionea tungekuwa, kama hivyo ingekuwa,
Rahisi kujichumia, pale usipopandia,
Hata mie ningekuwa,  iwe ninawaringia,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !

Walakini haijawa, na wala haitakuwa,
Kuchuma ni kuumia, tena sana kukimbia,
Uchumi ni kukataa, mfukoni kuzitoa,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !

Uchumi ni kukataa, mfukoni kuzitoa,
Ila ikiwa yafaa, kwa  hivyo kuingizia,
Vinginevyo wafulia, ovyoovyo kutumia,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !

Simu zinatuibia, hili ninawaambia,
Na nyie msiojua, zaidi mtaumia,
Ukiziona kimbia, salama utaijua,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !

Mwizi akikurupushwa





WATU ninawausia, hadhari kuichukua,
Mwizi ukinyemelea, ni vyema kujiandaa,
Kwani akishtukia, aweza akakuua,
Mwizi akikurupushwa, huwa mkali kama chui !

Aibapo katulia, mipango kujatimia,
Kuta atazibomoa, na mwanya kujipatia,
Mlango akachagua, wapi pa kuingilia,
Mwizi akikurupushwa, huwa mkali kama chui !

Dirisha hulichagua, ikibidi hivyo kuwa,
Ndani akatumbukia, chake kuichagulia,
Na kisha kuyoyomea, aende kujiuzia,
Mwizi akikurupushwa, huwa mkali kama chui !

Ndani anapoingia, kaziye kujifanyia,
Ukaja kumshtua, uoga utamwigia,
Katika kujiokoa, kama chui atakuwa,
Mwizi akikurupushwa, huwa mkali kama chui !

Aweza kukurukia, kisha akakuparua,
Ukali ukizidia, lazima atakurarua,
Na damu akakutoa, uhai kuutishia,
Mwizi akikurupushwa, huwa mkali kama chui !

Ila ukijiandaa, akashindwa jitetea,
Akasalimu sheria, na mikono kunyanyua,
Pingu ukishamtia, hana la kuambulia,
Mwizi akikurupushwa, huwa mkali kama chui !

Hirizi atabetua, na hata akaing'oa,
Kinga imemkataa, tena haitomfaa,
Mwenye akajijutia, watu wengi kumjua,
Mwizi akikurupushwa, huwa mkali kama chui !

Itamjua dunia, na heshima kupotea,
Ukutani kuishia, mbio alizokimbia,
Na wengine huzimia, au presha kupaa,
Mwizi akikurupushwa, huwa mkali kama chui !

Hii ndiyo Tanzania, wenyewe tunajijua,
Kila mwenye kudhania, huenda akajifaa,
Huja akajaishia, chini kuja kuhcimbiwa,
Mwizi akikurupushwa, huwa mkali kama chui !

Siasa si kila kitu



WENGINE wamgechanua, katika teknolojia,
Na sayansi kuikwea,  kileleni kufikia,
Na biashara kupaa, hadi angani kwelea,
Siasa si kila kitu, ila fursa hakuna !

Kama wenu walilia, kura kwenda kugombea,
Wetu bado waotea, mataifa kuingia,
Dunia ikawajua, wala sio Tanzania,
Siasa si kila kitu, ila fursa hakuna !

Mbali wanafikiria, ndio mana wazamia,
Meli wasizozijua, wapi zinaeleka,
Malengo wafukuzia, waachane na udhia,
Siasa si kila kitu, ila fursa hakuna !

Hata soka walilia, majuu kwenda kukaa,
Timu ndogo kuchezea, mbali sana wangekua,
Na mateja na vichaa, hata nao wangepungua,
Siasa si kila kitu, ila fursa hakuna !

Wangali wanatakiwa, matunda kuyatungua,
Rahisi ingelikuwa, saa hizi wangetoa,
Nyumba kujijengea, ambazo tunawatania,
Siasa si kila kitu, ila fursa hakuna !

Sera inazikataa, mwisho zitakubaliwa,
Unafiki ulokuwa, hadithi ikatimia,
Mbichi zile zimekuwa, kumbe huku zatakiwa,
Siasa si kila kitu, ila fursa hakuna !

Namimi nitarudia, hadi watu wakajua,
Ukweli ulokuwa, na wakweli walokuwa,
Na kisha kujipandia, kile kinachotakiwa,
Siasa si kila kitu, ila fursa hakuna !

Kuna kazi kuamua, kidogo kuwagawia,
Na senti ikichangiwa, wakati wa kujitolea,
Vitatengezwa vifaa, na miji ikachanua,
Siasa si kila kitu, ila fursa hakuna !

Akili zinatakiwa, watu wanazifukia,
Barabara zingefaa,mwanzo hadi akheria,
Maji tungelichimbua, kila kona Taznaia,
Siasa si kila kitu, ila fursa hakuna !

Ila tunavyotambua, wengi watajiumbua,
Misaada wangojea, kwenda kujipaulia,
Ujasiriamalia, ndio unakataliwa,
Siasa si kila kitu, ila fursa hakuna !

Tunaweza jifanyia, mengi sana yalokuwa,
Ila hili wahofia, ufakiri utatoa,
Watu wakiendelea, wakubwa watang'olewa,
Siasa si kila kitu, ila fursa hakuna !

Uchumi wanauua, ila yao kutimia,
Kisha wanasingizia, hata vile visokuwa,
Wajinga wakiwajua, ni nini kitatembea?
Siasa si kila kitu, ila fursa hakuna !

Mimi ninayahofia, wala sitaki kisia,
Ingawa ninayajua, na roho inaumia,
Sihiri ninakataa, kwenda kuitazamia,
Siasa si kila kitu, ila fursa hakuna !


Monday, April 2, 2012

Mtaji ni kama mbegu

Ukifa hautokuwa, mtaji inavyokua,
Kitu hakitobakia, kufilisika ni njia,
Na ukishakuishiwa, mengi yatakusumbua,
Mtaji ni kama mbegu, ukiula haukui!

Talanta ukijaliwa, budi kuziangalia,
Tofauti ukajua, na hela iliyokuwa,
Kuguswa kutoridhia, salama mkabakia,
Jina mchoyo ukipewa, kubali na kuridhia,
Mtaji ni kama mbegu, ukiula haukui!

Mtaji mizizi hutoa, ndipo panapoanzia,
Hapo ukishikilia, chini hutotumbukia,
Ila ukja legea, pabaya utaingia,
Mtaji ni kama mbegu, ukiula haukui!

Mtaji wataka kulea, na maji kuumwagia,
Na hesabu kuzijua, unavyotakiwa kukua,
Usije ukapungua, nakisi ukaingia,
Mtaji ni kama mbegu, ukiula haukui!

Mtaji wataka mbolea, na samadi kuitia,
Na udongo kubambua, k isha ukadadavua,
Na dawa kuumwagiwa, wadudu kutokaribia,
Mtaji ni kama mbegu, ukiula haukui!

Kitu ukishagundua, mwenyewe kujifanyia,
Ndugu kutowaachia, na rafiki na jamaa,
Wengi waharibikiwa, watu kutumainia,
Mtaji ni kama mbegu, ukiula haukui!

Mtaji umeumbua, tajiri walodhania,
Wakajikuta nazaa, imekwishawachezea,
Hakuna wa kulmlilia, yazidi sepa dunia,
Mtaji ni kama mbegu, ukiula haukui!

Kila wakifikiria, uzembe wawashtakia,
Laiti wangelijua, mtaji wasingetoa,
Mchomgoma umekua,kushuka ukikataa,
Mtaji ni kama mbegu, ukiula haukui!

Kidogo ukidokoa, huwezi kurudishia,
Huwa kama ni balaa, ukianza nyong'onyea,
Dhiki hukukimbilia, wengine kuwakimbia,
Mtaji ni kama mbegu, ukiula haukui!

Kila muabudu pesa

MWISHO huja kuikosa, kila muabudu pesa,
Kila kitu humsusa, akabaki hana hisa,
Muflisi kutonesa, liporomoke darasa,
Kila muabudu pesa, mwisho huja kuikosa!

Huzitamani anasa, aanze naye kutesa,
Akaziacha fursa, vyenye pato kuvinusa,
Akahama kudodosa, ahamie kutomasa,
Kila muabudu pesa, mwisho huja kuikosa!

Huwa ni kisa na mkasa, tena visivyo msasa,
Abakie kipukusa, ndizi isiyo hasusa,
Mwilini akipapasa, akute hanayo hisa,
Kila muabudu pesa, mwisho huja kuikosa!

Hisia haiwi hisa, wala halipi posa,
Mchumba utamkosa, ambebe bwana Issa,
Na mwishowe ukasusa, ndoa uache kabisa,
Kila muabudu pesa, mwisho huja kuikosa!

Kosa halijawa kosa, hadi kurudia kosa,
Baraka ikikigusa, nusura huwa mkasa,
Ya jana yakawa sasa, mtu uzidi kutesa,
Kila muabudu pesa, mwisho huja kuikosa!

Pamoja kujipapasa, shilingi nimeikosa,
Koti nimeshalinusa, bado siioni pesa,
Na chini nimetikisa, naona yote mkasa,
Kila muabudu pesa, mwisho huja kuikosa!

Watu huja kuwatesa, kila muabudu pesa,
Akakopa na kususa, madeni yakawa h isa,
Na kokote mkunusa, harufu mtaikosa,
Kila muabudu pesa, mwisho huja kuikosa!

Mtaenda kwenye misa, na masjidi kugusa,
Dua mtie vitasa, bado huwa ni makosa,
Nyusi akishapepesa, yote huwa yake hisa,
Kila muabudu pesa, mwisho huja kuikosa!

Ukitaka kumgusa, hupasuka kama kasa,
Akalia na kususa, eti nyie mwamtesa,
Keshalishindwa darasa, kumsomesha si ruksa,
Kila muabudu pesa, mwisho huja kuikosa!

Na pesa itamtosa, milele ikamsusa,
Abaki kula mikasa, na vingine vyenye tasa,
Rehema kutomgusa, h adi tawba kunusa,
Kila muabudu pesa, mwisho huja kuikosa!

Tumezoea majembe

Nawasema kuurumbembe, waliokubuhu vijembe,
Vichwa vyao wasivimbe, kuwasifu nisiambe,
Ninawaona ni ng'ombe, kuchinjwa wao ujumbe,
Tumezoea majembe, havitushindi vijembe!

Niacheni niwachambe, wanaokifu wajumbe,
Hata kitu wasirambe, kwenye hizo zao tembe,
Na popote wasitambe, bado ni wala maembe,
Tumezoea majembe, havitushindi vijembe!

Ajira yao waimbe, ili watu wasigombe,
Hutaka vichwa wavimbe, wavipate na vikombe,
Kwa kuzing'oa pembe, na kumwaga nyingi pombe,
Tumezoea majembe, havitushindi vijembe!

Wanataka uwalambe, na ya kwao uyaimbe,
Kama sivyo wakukumbe, wakuchanje kwa uwembe,
Macho yako wakufumbe, ya ovyo usiwachambe,
Tumezoea majembe, havitushindi vijembe!

Nendeni mkawabambe, huku wamevaa pembe,
Ni majini msiombe, mkutane na wazembe,
Bilauri na vikombe, huvitumia wachambe,
Tumezoea majembe, havitushindi vijembe!

Nalipika langu sembe, na mchuziwe wa shombe,
Vinginevyo usiambe, riziki yangu si chembe,
Pawa tila ni uvimbe, kwanini mguu usivimbe ?
Tumezoea majembe, havitushindi vijembe!

Nanywa hili langgu kombe, majirani msisambe,
Nitazikomesha ngebe, vya kwangu wasiviibe,
Niwafungie mikebe, wasikike wasitambe,
Tumezoea majembe, havitushindi vijembe!

Hatuogopi vijembe, tumezoea majembe,
Vinginevyo msitambe, wimbo wenu tuuimbe,
Na siku ya siku tugombe, mchawi wetu tumzombe,
Tumezoea majembe, havitushindi vijembe!

Kuna harufu ya hongo

HUJIFANYA watawala, wananchi wakazuga,
Wao wakipata kula, makombo watagawa-ga,
Maua katika yala, ni sehemu ya maboga,
Kuna harufu ya hongo, kauli za viongozi!

Ila lazuka suala, lisilotaka uoga,
Kileo pia kimila, udhia tukaubwaga,
Watu wasio fadhila, nao tupate waaga,
Kuna harufu ya hongo, kauli za viongozi!

Wanaotumia hela, haki zetu kuvuruga,
Kukataa yao hila, pembeni tukawaswaga,
Wabakie wenye ala, akili wanaotumia,
Kuna harufu ya hongo, kauli za viongozi!

Zinakwama zetu hali, kwa kuyabeba maboga,
Ni wachache wa fadhili, kwayo wakishakuroga,
Hukufanza ni anzali. wakazidi kujikoga,
Kuna harufu ya hongo, kauli za viongozi!

Ya kwao sio kamili, ndio kisa wanahonga,
Na wengine majahili, hujuma wanazitunga,
Budi mustakabali, hawa tukawavuruga,
Kuna harufu ya hongo, kauli za viongozi!

Ili tupate jamali, wa kale tuwapa bega,
Tuiwashe na kandili, yaliyo bora kuiga,
Tusiwe tena mithili, viumbe wanaofugwa,
Kuna harufu ya hongo, kauli za viongozi!

Hali zetu kubadili, budi tuache kuhongwa,
Tukamhofu Adili, kiboko kutotupiga,
Tukazijenga amali, na wengine kutuiga,
Kuna harufu ya hongo, kauli za viongozi!

Tumuombeni Jalali, mabaya tukayabwaga,
Uondoke mushkeli, neema tupate oga,
Zinawiri zetu hali, utu tupate kujenga,
Kuna harufu ya hongo, kauli za viongozi!

Unavuta blanketi

Kiasi ungelijua, yako ungeliyapima,
Yasipate kupungua, au kuzidi kasima,
Katikati ukatua, ungali bado wahema,
Unavuta blanketi, jua lakuamkua?

Muda unapoachia, yaweza zuka nakama,
Hili ukatangulia, na yale yakasimama,
Subira wasiokuwa, ndipo hapo hulalama,
Unavuta blanketi, jua lakuamkua?

Usingizi kuugua, ukizidi unauma,
Hali ikawa ni mbaya, pasiwe tena uzima,
Na haSa pakuzingatia, palipo na ndarahima,
Unavuta blanketi, jua lakuamkua?

Muda wataka tambua, umuhimu kuupema,
Na kila linalokuwa, nafasi ukaisoma,
Na somo ukalitoa, bila kuvunja kalmima,
Unavuta blanketi, jua lakuamkua?

Na usipojitambua, hili kwako si lazima,
Ila yatakayotokea, ujumbe zitautuma,
Na haki ukaridhia, bila vingine kusema,
Unavuta blanketi, jua lakuamkua?

Huwezi ukaelwa, muda wake mahakama,
Haukufuli rufaa, na masmaha kuchuma,
Hutoka ukaishia, hakuna kurudi nyuma,
Unavuta blanketi, jua lakuamkua?

Muumba wa zetu sanaa, namshukuru Adhama,
Nami nililopangiwa, kwa wakati kutazama,
Chumo nikajichumia, pahala pema kusimama,
Unavuta blanketi, jua lakuamkua?

Unavuta blanketi

Kiasi ungelijua, yako ungeliyapima,
Yasipate kupungua, au kuzidi kasima,
Katikati ukatua, ungali bado wahema,
Unavuta blanketi, jua lakuamkua?

Muda unapoachia, yaweza zuka nakama,
Hili ukatangulia, na yale yakasimama,
Subira wasiokuwa, ndipo hapo hulalama,
Unavuta blanketi, jua lakuamkua?

Usingizi kuugua, ukizidi unauma,
Hali ikawa ni mbaya, pasiwe tena uzima,
Na haSa pakuzingatia, palipo na ndarahima,
Unavuta blanketi, jua lakuamkua?

Muda wataka tambua, umuhimu kuupema,
Na kila linalokuwa, nafasi ukaisoma,
Na somo ukalitoa, bila kuvunja kalmima,
Unavuta blanketi, jua lakuamkua?

Na usipojitambua, hili kwako si lazima,
Ila yatakayotokea, ujumbe zitautuma,
Na haki ukaridhia, bila vingine kusema,
Unavuta blanketi, jua lakuamkua?

Huwezi ukaelwa, muda wake mahakama,
Haukufuli rufaa, na masmaha kuchuma,
Hutoka ukaishia, hakuna kurudi nyuma,
Unavuta blanketi, jua lakuamkua?

Muumba wa zetu sanaa, namshukuru Adhama,
Nami nililopangiwa, kwa wakati kutazama,
Chumo nikajichumia, pahala pema kusimama,
Unavuta blanketi, jua lakuamkua?

Ukililia kiatu

KIATU ukililia, unapaswa kutambua,
Wapo waliozaliwa, miguu hawakupewa,
Hapungukiwi Jalia, ila hilo karidhia,
Ukililia kiatu, mwenzio miguu hana!

Mzazi hupungukiwa, unapaswa kulijua,
Ndiye anayezitoa, pindi anapojaliwa,
Kama asipogaiwa, ni kipi atakigawa?
Ukililia kiatu, mwenzio miguu hana!

Siwezi kujisifia, riziki ninaigawa,
Yapo juu alokuwa, nami ninamgonjea,
Hushukuru nikipewa, na kukosa naridhia,
Ukililia kiatu, mwenzio miguu hana!

Maisha yana hatua, kupata na kupotea,
Kama somo ukijua, sahihi na kukosea,
Na mengine majaliwa, hauwezi kuyajua,
Ukililia kiatu, mwenzio miguu hana!

Yako wewe angalia, na tosheka ukijua,
Wako juu watakuwa, nawe kati kubakia,
Na chini wakafatia, kama wewe wasojaliwa,
Ukililia kiatu, mwenzio miguu hana!

Mwana ninakuusia, jenga kinaya na dunia,
Na hautopungukiwa, utatosheka radhia,
Yao ukaangalia, na yako ukatumia,
Ukililia kiatu, mwenzio miguu hana!

Tosheka nayo dunia, nayo itakuachia,
Nje wanaoangalia, na husuda kuwajaa,
Husumbuka na dunia, kufa bado wana njaa,
Ukililia kiatu, mwenzio miguu hana!

Huwa watu wa kulia, kucheka wakakohoa,
Maji hawawezi tia, kinywani wametulia,
Shinikizo huingia, mapema kuteketea,
Ukililia kiatu, mwenzio miguu hana!

Akili ukijaliwa, wapaswa kuzitumia,
Fakiri ukijijua, juu zitakunyanyua,
Na subira ukilea, inshallah utajaliwa,
Ukililia kiatu, mwenzio miguu hana!

Chemchemi ikikauka

Mnagombea kitu gani, kisima hakina maji,
Nikifanya tathmini, hakuna mnachohitaji,
Na ujio siuoni, ila kuhama kijiji,
Chemchemi bila maji, mnagombea kitu gani ?

Nawaona Kisauni, bado mwatafuta m aji,
Walio kaskazini, sasa wawapeni uji,
Kiu hakiuamini, bado chalilia maji,
Chemchemi bila maji, mnagombea kitu gani ?

Na nyie Mchikichini, yako wapi mahitaji,
Mnauchoma ubani, wageuka kuwa mboji,
Bado yako ughaibuni, kwenu yasita hayaji,
Chemchemi bila maji, mnagombea kitu gani ?

Nimeuliza yamini, kama kuna ufujaji,
Yakawa bila thamani, tokea kwenye thaluji,
Wanasema yumkini, kwa hili si wasomaji,
Chemchemi bila maji, mnagombea kitu gani ?

Chemchemi bila maji, mnagombea kitu gani ?

Nimefika na Uzini, nilipotoka Kimbiji,
Utafiti kubaini, kisa chake ukosaji,
Na majibu si yakini, ila kuna uhitaji,
Chemchemi bila maji, mnagombea kitu gani ?

Nauliza Mkoani, na Chake kwenye mji,
Wao wayaficha ndani, mvua wakitaraji,
Watakuwamo shakani, ikiwa nayo haiji,
Chemchemi bila maji, mnagombea kitu gani ?

Malindi nikasaini, na Lamu nimewahoji,
Nauliza kuna nini, maji yakwama Buruji,
Au wapuuza dini, kakasirika wao Jaji?
Chemchemi bila maji, mnagombea kitu gani ?

Wanateta hadharani, bandari wanaitaraji,
Kama si leo mwakani, na nasara waundaji,
Kisiwa kiko shakani, Maajid kumsujudi,
Chemchemi bila maji, mnagombea kitu gani ?

Neno toka mafichoni

WAJE juu na madege, na helikopta pia,
Wapambe kama nzige, anga na hii dunia,
Naweza nisiwaige, bado nikawanyanyua,
Neno toka mafichoni, linaweza kuwa dawa?

Hakika mfanywa bwege, neno lake akijua,
Yumkini wamroge, ndio chini hutulia,
Ujinga tena afuge, kwake huwa ni nazaa,
Neno toka mafichoni, maskini kaamini?

Keshalikinai bunge, yake haliwezi jua,
Na japo mchafukoge, kuringa yake ridhaa,
Mpeni maji aoge, yake mkayaachia,
Neno toka mafichoni, mayatima waridhia ?

Watu hawajawa ndege,tunduni mkawatia,
Maishani muwafuge, uhuru kutowaachia,
Huja waje walichonge, sawia lililokuwa,
Neno toka mafichoni, wasonacho walijua ?

Haijengwi kwa mizengwe, hii yetu Tanzania,
Haya bure mjivunge, mtakuja sanzuliwa,
Na wenyewe mjiroge, wengine kusingizia,
Neno toka mafichoni, linaweza kuwa dawa?

Demokrasia kikongwe, kila kitu inajua,
Elimu budi mlenge, msojua kurudia,
Burebure msijikoge, kaburi mwajichimbia,
Neno toka mafichoni, maskini kaamini?

Yapo yasiyo matege, twaweza zungumzia,
Na chama chenu mjenge,mambo mkafanikiwa,
Vingenevyo mringe,nasi tutawaangalia,
Neno toka mafichoni, mayatima waridhia ?

Twataka nchi mjenge,ushabiki twakataa,
Wabora wenu muige, uongo kutokuzua,
Nyoyo za watu mkonge, ridhaa mkapatiwa,
Neno toka mafichoni, linaweza kuwa dawa?

Ubabe budi mbwage, au utawaambua,
Watu ovyo msipige, madhambi mkayavaa,
Laana muwe vihongwe, mkaja kuachiwa,
Neno toka mafichoni, maskini kaamini?

Kirini ulegelege, ndani umeingia,
Gamba ili 'litokage', nusunusu kutoachia,
Na mkitaka 'mlindwagwe', wapo wa kushikilia,
Neno toka mafichoni, mayatima waridhia ?

Kengele sasa mpige, upya mpate zaliwa,
Ajizi msikoroge, sumu mkajinywea,
Ukweli msijivunge, vijan wawakataa,
Neno toka mafichoni, wasonacho walijua ?

Kisa wao mwatenge, kuzaa na wa kutozaa,
Mkayaweka magenge, utu kujivurugia,
Kisha wenu muwafuge, wengine kuwaachia,
Neno toka mafichoni, wasonacho walijua ?

Waona kanga na vitenge, mjini mkivigawa,
Vijijini muwakoge, uongo kuwaachia,
Na mbele wasisonge, karne yakaribia,
Neno toka mafichoni, wasonacho walijua ?