Thursday, April 26, 2012
Mwizi akikurupushwa
WATU ninawausia, hadhari kuichukua,
Mwizi ukinyemelea, ni vyema kujiandaa,
Kwani akishtukia, aweza akakuua,
Mwizi akikurupushwa, huwa mkali kama chui !
Aibapo katulia, mipango kujatimia,
Kuta atazibomoa, na mwanya kujipatia,
Mlango akachagua, wapi pa kuingilia,
Mwizi akikurupushwa, huwa mkali kama chui !
Dirisha hulichagua, ikibidi hivyo kuwa,
Ndani akatumbukia, chake kuichagulia,
Na kisha kuyoyomea, aende kujiuzia,
Mwizi akikurupushwa, huwa mkali kama chui !
Ndani anapoingia, kaziye kujifanyia,
Ukaja kumshtua, uoga utamwigia,
Katika kujiokoa, kama chui atakuwa,
Mwizi akikurupushwa, huwa mkali kama chui !
Aweza kukurukia, kisha akakuparua,
Ukali ukizidia, lazima atakurarua,
Na damu akakutoa, uhai kuutishia,
Mwizi akikurupushwa, huwa mkali kama chui !
Ila ukijiandaa, akashindwa jitetea,
Akasalimu sheria, na mikono kunyanyua,
Pingu ukishamtia, hana la kuambulia,
Mwizi akikurupushwa, huwa mkali kama chui !
Hirizi atabetua, na hata akaing'oa,
Kinga imemkataa, tena haitomfaa,
Mwenye akajijutia, watu wengi kumjua,
Mwizi akikurupushwa, huwa mkali kama chui !
Itamjua dunia, na heshima kupotea,
Ukutani kuishia, mbio alizokimbia,
Na wengine huzimia, au presha kupaa,
Mwizi akikurupushwa, huwa mkali kama chui !
Hii ndiyo Tanzania, wenyewe tunajijua,
Kila mwenye kudhania, huenda akajifaa,
Huja akajaishia, chini kuja kuhcimbiwa,
Mwizi akikurupushwa, huwa mkali kama chui !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment