Ndio wanaochochea, uroho nayo tamaa,
Kama mvuvi kuvua, bila nyavu kutumia,
Na kulima asojua, akavuna na kupaa,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !
Vijana wawahadaa, tena kisaikolojia,
Kamari imeshakua, jina lake inafaa,
Na wakubwa walokuwa, nuksi hawajaijua,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !
Imani zatuvunjia, na vijana kupotea,
Na vichaa walokuwa, kazi wanazikimbia,
Na idadi tunajua, mia haitafikia,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !
Matangazo ni balaa, tivii na redio pia,
Ovyo zinavyotumiwa, ni ila imeingia,
Na kula anayejua, wana atawaambia,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !
Vilio zitatutia, pasiwe pa kukimbilia,
Wanyonge tunanyolewa, kidogo tulichopewa,
Na wkubwa wanajaa, matumbo kuwalegea,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !
Uhuni umeingia, kucheza nazo ruia,
Na rahisi walokuwa, vijana wahusudiwa,
Ujinga waliojaa, ktuokana nayo njaa,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !
Milionea tungekuwa, kama hivyo ingekuwa,
Rahisi kujichumia, pale usipopandia,
Hata mie ningekuwa, iwe ninawaringia,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !
Walakini haijawa, na wala haitakuwa,
Kuchuma ni kuumia, tena sana kukimbia,
Uchumi ni kukataa, mfukoni kuzitoa,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !
Uchumi ni kukataa, mfukoni kuzitoa,
Ila ikiwa yafaa, kwa hivyo kuingizia,
Vinginevyo wafulia, ovyoovyo kutumia,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !
Simu zinatuibia, hili ninawaambia,
Na nyie msiojua, zaidi mtaumia,
Ukiziona kimbia, salama utaijua,
Tungekuwa milionea, watu wote, kama ndivyo !
Thursday, April 26, 2012
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment