Tuesday, September 4, 2012

DHULUMA YA UUAJI



MAMBO yanapoanzia, kila mtu bize huwa,
Hakuna wa kufikiria, na sababu kuijua,
Huhangaika na dunia, hadi yakikuzungua,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Huyo aliyeuawa, si wa kwetu alikuwa,
Msiba tumesikia, wala hatukumjua,
Nani angemlilia, licha ya kumchangia,
Muuaji akianza, hujui anayefata!

Kawaida tulijua, na kukubali kuambiwa,
Nchi inaendelea, na usalama yajaa,
Kikombe kimetulia, kumbe chini chavujia,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Mwingine akafatia, hakutoka wetu mkoa,
Hayo tulipyajua, wala hatukujistua,
Huzuni ikaambaa, nani kumsikitikia?
Muuaji akianza, hujui anayefata!

Machozi yakasinzia, na macho yakalemaa,
Si wa wetu mkoa, nini kujihangaikia,
Kaida tukapanua, kiada lililokuwa,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Juzi aliyeuawa, si wa yetu wilaya,
Mbali sana katokea, kwenye zege na maziwa,
Ikawa kujisemea, bwana katoa, katwaa!
Muuaji akianza, hujui anayefata!

Innali lillahi pia, wa inna illahi pia,
Rajiuni tukatia, imani kuifatia,
Kwani hatukutambua, wala asili kujua,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Kadari tukaamua, mbele ametangulia,
Nyuma tunafuatia, bila ya kuhujumiwa,
Shetani katuhadaa, yote sawa kudhania,
Muuaji akianza, hujui anayefata!

Daktari kaibiwa, kama vile ni bidhaa,
Msituni katupiwa, wakidhani kajifia,
Fisi atamfagia, wasafi wakabakia,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Walimu wanahofia, kitanzi chaning'inia,
Vitisho wavipokea, bila watu kuwajua,
Watumwa au watumiwa, hilo hawajalijua,
Muuaji akianza, hujui anayefata!

Mwislamu kumkwaa, chini kaangukia,
Watu tukaangalia, moyoni twajisemea,
Mkorofi amekua, haki yake kupigania!
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Njiani kumuachia, sisi tukafikiria,
Nguvu ameshaishiwa, kaanguka kwa njaa,
Pale hatukumnyanyua, sembuse kumchangia?
Muuaji akianza, hujui anayefata!

Alipopaangukia, wala hatukuanglaia,
Wenyewe tukaamua, akili hakutumia,
Kawaida tukavaa, desturi kwendelea,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Mwingine akauawa, dini yetu asokuwa,
Sisi tukajikalia, ya kwetu kuangalia,
Kama vile tunajua, sisi hayatatokea,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Mwingine akauawa, kabila letu hakuwa,
Mmakonde kazaliwa, chamaki mchanga kaua,
Mzaramo kamkimbia, kamuacha auawa,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Kisha akafuatia, kibaka tunayemjua,
Siku haikuishia, mwana wetu kazuliwa,
Pale alipofumaniwa, wizi akasingiziwa,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Tairi wakamtia, na moto kumuashia,
Mwana akateketea, huku tunamuangalia,
Mwanamke katujia, si mwizi atulilia,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Sadaka ilishakuwa, hakuna cha kubakia,
Kafara ametolewa, kwa sheria za kuzua,
Na hii ndiyo tabia, wakuu wafurahia,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Hadi yanapotokea, kwenye zetu familia,
Ndipo macho hufungua, ukweli kujipenyea,
Shetani katwiingilia, ovyoovyo anaua,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Islamu kuhiniwa, sawa tukakubalia,
Bila ya kujitambua, kibao kugeuziwa,
Mwenzio akinyolewa, maji tumeyakataa,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Usafi tukajitia, mkorofi amekua,
Na nyimbo kuwatungia, zaidi kushindilia,
Huku tunafurahia, waumini tutazoa,
Muuaji akianza, hujui anayefata!

Tusipozidi wafaa, budi kutugeukia,
Na chote tulichopewa, huenda wakatukua,
Utupu kutuachia, tubaki tunayajutia,
Muuaji akianza, hujui anayefata!

Kifua ukimkingia, bei hukupandishia,
Walimu hawatakuwa, hilo wakakubalia,
Huanza kukuhesabia, kama huna wakuua,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Kibao hukugeuzia, kazi uliyewapatia,
Ndivyo ilivyo dunia, na huko mnaelekea,
Laiti mkijitambua, maafa mtazuia,
Muuaji akianza, hujui anayefata!

Fikra mkipakua, salama kujidhania,
Walokole mlokuwa, kuwa hamtajaribiwa,
Huishia kuyajutia, wakati ukiwadia,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Katika hii dunia, wajaa watu wabaya,
Nchi wakiichukua, hakuna cha kuambulia,
Hao ukisadia, mtegoni waingia,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Wauaji hutumiwa, kazi zao kuwafaa,
Shetani awatumia, kwa uhai kuutoa,
Wao wakifikiria, ndio eti wajikwamua,
Muuaji akianza, hujui anayefata!

Katoliki wadhania, ufalme wautwaa,
Kibao kugeuziwa, muda hautachukua,
Haya mtajayajuti, laiti mngelijua,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Sote panapotufaa, ni adili kulilia,
Haki tukaisimamia, na usawa kuridhia,
Vingine haitakuwa, wenyewe tutaumia,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Ni mafundi wa kugawa, vitani mkaingia,
Wenyewe kujiumbua, pasiwe cha kubakia,
Kisha hufurahia, usukani kuutwaa,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Shetani akiingia, nani wa kumridhia,
Kati yetu huchagua, Islamu na wasokuwa?
Au wote huvamiwa, imani kutuondoa?
Muuaji akianza, hujui anayefata!

Sauti mnatakiwa, viongozi kuitoa,
Dini mnaosimamia, la kwenu tukasikia,
Haya mkivumilia, pabaya twaelekea,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!

Nusura kwetu kwanzia, pengine haitatokea,
Ni bure tutajihadaa, watu hawa wanshalewa,
Vigumu kufikiria, iwe ndio kutambua ?
Muuaji akianza, hujui anayefata!

Hofu zinawachochea, za uongo zikitiwa,
Adui wakamdhania, hata yule asokuwa,
Risasi waziachia, kila mahala kupaa,
Kazi yake akianza, muuaji hachagui!


MTOTO AKIONGOZA





Yenyewe yajiendea, hakuna asiyejua,

Mwana akizawadiwa, maajabu atazua,

Njaa asiyeijua, na watu kupendelea,

Ukimkabidhi mtoto, nchi hii aongoza!



Kama kweli kalelewa, wananchi hatotwibia,

Chetu ataangalia, na kisha kukipigania,

Nafasi ikitokea, azidi kutuongezea,

Ukimkabidhi mtoto, nchi hii aongoza!



Umeme hatotuhadaa, kwa trilioni kufua,

Ujanja atatumia, njia zetu kuzijua,

Umeme tukakamua, kama vile ni maziwa,

Ukimkabidhi mtoto, nchi hii aongoza!



Fedha hatotuibia, Uswizi kujifichia,

Tamaa haitwamtaa, ukubwa kuulilia,

Utoto atatezea, ya kwetu yakawadia,

Ukimkabidhi mtoto, nchi hii aongoza!



Rushwa ataikataa, maana hana mazoea,

Takukuru kujifia, haki bado ikakua,

Akaondoa udhia, nchi ikarehemewa,

Ukimkabidhi mtoto, nchi hii aongoza!



Hatutakuwa na njaa, kilimo sio sanaa,

Masoko kuulizia, ndio mbegu akatia,

Mlaji akanunua, na sio kununuliwa,

Ukimkabidhi mtoto, nchi hii aongoza!



Michezo hatutafulia, uwanja kauchagua,

Kucheza ni mazoea, wala sio kujitia,

Jinsi anvyoshangilia, medali tutazivua,

Ukimkabidhi mtoto, nchi hii aongoza!



Amani atatambua, ulinzi hajaupewa,

Mungu katusaidia, kuitunza twatakiwa,

Hawezi kuichezea, kwa ukubwa kujifaa,

Ukimkabidhi mtoto, nchi hii aongoza!



Umoja ataujua, hustawi pasipo njaa,

Chakula atawania, bei zipate pungua,

Kama ulaya ikawa, chini ya kumi asilimia,

Ukimkabidhi mtoto, nchi hii aongoza!



Kama ulaya ikawa, chini ya kumi asilimia,

Kipato kinachoingia, kwa chakula kutumia,

Kingine kikabakia, tutaacha kuendelea?

Ukimkabidhi mtoto, nchi hii aongoza!



Mola tunamlilia, utoto wa kutufaa,

Si ukubwa wa nazaa, watu waliojichokea,

Nakisi yaendelea, na nafuu inapaa,

Ukimkabidhi mtoto, nchi hii aongoza!



Kisha wanajipikia, takwimu za kutungua,

Uongo zilizojaa, ukweli zinaoua,

Eti tunaendelea, huku twazidi fulia,

Ukimkabidhi mtoto, nchi hii aongoza!

TAIFA WENYE KUUA







UMUNGU akijitia, kutaka yote amua,

Hoja akazikataa, za kweli zilizokuwa,

Na uongo kutumia, umma akauhadaa,

Nchi anayeiua, ni viongozi wa nchi!



Hawezi kuwa raia, dola hii hakupewa,

Huyo anayeshilkilia, atakiwa kulijua,

Mamboye yanavyokuwa, ndivyo nchi nayo huwa,

Nchi anayeiua, ni viongozi wa nchi!



Dola akiitumia, wengine kuwachukia,

Kisha akapendelea, wa kwake waliokuwa,

Nchi huwa anaua, huku ashangiliwa,

Nchi anayeiua, ni viongozi wa nchi!



Akizidisha tamaa, na ukubwa kuutwaa,

Watu kutowaachia, uhuru wa kupumua,

Akajifanza wa kujua, hata asiyoyajua,

Nchi anayeiua, ni viongozi wa nchi!



Watu wakimtumia, walo nyuma ya pazia,

Yao akayasikia, bila kiini kujua,

Wala wana ipi nia, mbele iliyotangulia,

Nchi anayeiua, ni viongozi wa nchi!



Yakishindwa kutimia, aliyoyafikiria,

Ubaya akawatia, wabaya wasiokuwa,

Kisha kuwashambulia, kwa maneno na silaha,

Nchi anayeiua, ni viongozi wa nchi!



Hawezi kuwa raia, hii si yake himaya,

Hazina hawajapewa, kwa lolote kuitumia,

Wakiamua mabaya, basi maovu huzua,

Nchi anayeiua, ni viongozi wa nchi!



Mpinga demokrasia, kisirisiri akawa,

Huku anabwabwajia, mema anatutakia,

Ndumilakuwili huwa, vyema hivyo kumjua,

Nchi anayeiua, ni viongozi wa nchi!



Watu mwenye kuwagawa, visenti kuwapatia,

Wao wakishajaliwa, wengine watafatia,

Udokozi wakazua, nchi kujitafunia,

Nchi anayeiua, ni viongozi wa nchi!



Hakuna kinachobakia, uongo watauzua,

Huyu tumemmegea, hata na ndugu zako pia,

Na kinachofuataia, wengine kuwa wabaya,

Nchi anayeiua, ni viongozi wa nchi!



Hekima akiivua, ujinga ukawa kisiwa,

Busara akifukia, utoto kuogelea,

Roho huwa zajifia, aidha mioyo pia,

Nchi anayeiua, ni viongozi wa nchi!



Na wasiojitambua, hili watashingilia,

Kaburini huingia, huku wanachekelea,

Mumiani kumwamkua, machinjoni waingia,

Nchi anayeiua, ni viongozi wa nchi!



Ndio sana yatakiwa, katiba kutuamulia,

Dhima kumpunguzia, asitupeleke pabaya,

Mungu tukimdhania, Mola hatolifurahia,

Nchi anayeiua, ni viongozi wa nchi!

Akuvutaye kwa udi














KWA udi akuvutaye, mvujewe hukutoa,

Hapo ndipo yaishie, kwake yako yalokuwa,

Kiwewe asikutiye, ukweli ukamjua,

Akuvutaye kwa udi, hukufukuza kwa mvuje!



Wakati akutakaye, marashi atayatia,

Pumzi asiachie, kila kona kunukia,

Nasibu aingojee, wewe kumkumbatia,

Akuvutaye kwa udi, hukufukuza kwa mvuje!



Uoza ni afichaye, yake kutokuyajua,

Vingine usimfikirie, mkweli ukadhania,

Kumbe akuhadaa weye, yake akafanikiwa,

Akuvutaye kwa udi, hukufukuza kwa mvuje!



Ni mtu ajipambae, kwa sifa asiyokuwa,

Cheo juu ajipae, muhimu ukadhania,

Ili yoe yake yawe, bila ya wewe kujua,

Akuvutaye kwa udi, hukufukuza kwa mvuje!



Ni msafi ajifanyae, kama vile hana doa,

Ili kwa wamjuaye, waijua yake tabia,

Kabisa si wamtakaye, mbali naye wanakaa,

Akuvutaye kwa udi, hukufukuza kwa mvuje!



Uzuri kama kinyaye, hakika huutumia,

Ili wasimtambue, si kitu aliyekuwa,

Jamili yake ni koe, chambo chake kuvulia,

Akuvutaye kwa udi, hukufukuza kwa mvuje!



Kinda huwa avizie, kitu wasiotambua,

Mwepesi adanganyae, sura kutokufichua,

Wakaingia kiwewe, kwa bashasha kuwatia,

Akuvutaye kwa udi, hukufukuza kwa mvuje!



Si mtu afunuaye, ukweli huuchimbia,

Kamwe juu asitoe, mkaa akapalia,

Si nuru atakaye, nuru huwa akataa,

Akuvutaye kwa udi, hukufukuza kwa mvuje!



Mishtuko jiandae, ikiwa wamkurubia,

Na silaha uitwae, joka akigeukia,

Kisogo usimwachie, nondo atakuangushia,

Akuvutaye kwa udi, hukufukuza kwa mvuje!