Sunday, March 3, 2013

WATAKA KUNIUNGUZA ?



MKONO sintanyanyua, kukufanyia ubaya,
Ila moyo nafungua, dua nikajisomea,
Ukinitakia baya, zuri nitakuombea,
Wataka kuniangusha, usijeanguka wewe!

Ku'ngua waniombea, moto sintokuombea,
Maji unanimwagiwa, kutozama nakwombea,
Ila ulimi zuia, laana kutoitoa,
Wataka kuniunguza, utajiunguza wewe!

Wanitakia balaa, mie nipate umia?
Mwili ninakuachia, ila roho nakataa,
Hayo yako mazoea, siwezi kukuzuia,
Wataka kuniumiza, utaumia mwenyewe!

Wapuliza kwa ghasia, kuzimwa wanitakia,
Pumzi nakuachia, utambi najishushia,
Kwa tufani na mvua, kuzimwa nikakataa,
Wataka kunizimisha, usijezimika wewe!

Kuzama waniombea, chombo ninakuachia,
Mashimo ungefukua, bahari kuongezea,
Chewa ataniokoa, nchi kavu kurejea,
Wataka kunizamisha, usijekuzama wewe!

Kama mti wanivaa, na shoka kushambulia,
Kisa unaniombea, kuanguka natembea,
Nyayo sijashadidia, mlio hutosikia,
Wataka kuniangusha, usijeanguka wewe!

Wataka nikaaangiza, na upate niunguza,
Na masinzi kunitunza, mkaa kunieneza,
Kisha ukanipakiza, na majivu kunikwaza,
Wataka kuniunguza, utajiunguza wewe!

Kila ukikusudia, majidi akuumbua,
Sio njema yako nia, na yeye ameshaijua,
Mwenyewe namuachia, zawadi kukupatia,
Wataka kuniumiza, utaumia mwenyewe!

Kwani yeye ni mtoa, tena ndio mchukuwa,
Mgawaji maridhia, daima anayebakia,
Kila mwenye kujitia, mwishowe anaujua,
Wataka kunizimisha, usijezimika wewe!

Miye nimemridhia, yangu kan