Wednesday, November 28, 2012

Bibi msikilizeni


HEBU kitako kaeni, muwasikize wazee,
Hali zao taabani, nani wakamlillie,
Mwamsubiria nani, ya kwao awafanyie ?
Bibi msikilizeni, ana lake la kusema.

Bibi msikilizeni, na babu mkaongee,
Watu hawa si wageni, ndiko huko mtokee,
Muitunge afueni, kitaifa kuwafaa,
Bibi msikilizeni, ana lake la kusema.

Yao ni bure thamani, si ya kuwashinda nyie,
Ila muda hamuuoni, yao myafikitie,
Wanalilia vijijini, wazima mhurumie,
Bibi msikilizeni, ana lake la kusema.

Mia mbili ni hisani, kuipata ni ndotowe,
Wauliza nchi gani, yawa myaongozaye,
Mwawasemea kina nani, hadi leo mjisisfie?
Bibi msikilizeni, ana lake la kusema.

Maji hayapatikani,hadi mtu utembee,
Kilomita za uzani, na mzigo uchukuwe,
Inawavia imani, kwa maneno msiwapepee,
Bibi msikilizeni, ana lake la kusema.

Chakula chao utani, kwa njaa wajishibie,
Au mboga mgagani, maporini kuwafae,
Na majoka wa mwituni, hapo wasiwazuie,
Bibi msikilizeni, ana lake la kusema.

Uswizi zichukeni, vijiji zikawafae,
Huu ni unyama gani, kimya mjitangazie,
Hali kwamba vijijini, kizazi wakijutie ?
Bibi msikilizeni, ana lake la kusema.

Balaa tuepukeni, kwa kuwafaa wazee,
Tusiwe ni hayawani, sikuzote tulaaniwe,
Jitazameni moyoni, nchi isiwapotee,
Bibi msikilizeni, ana lake la kusema.

Huu wote hautoshi

Majeta tumejaliwa, viumbe wasioshiba,
Chote hujilimbikia, na njaa bado huwakaba,
Dunia hawajajua, watia kwenye viroba,
Huo wote hautoshi, wape nchi watashiba ?

Maneno wamuachia, ila vitendo ni haba,
Mgongo wamridhia, wajifiche kwazo toba,
Na nuksi na balaa, kisima chao chabeba,
Huo wote hautoshi, wape nchi watashiba ?

Tohara zao ubaya, na nyembe zenye unasaba,
Haya ukijiuzia, mahaba yako msiba,
Kila mjua tumbua, utumbuzi si janaba,
Huo wote hautoshi, wape nchi watashiba ?

Tartila sikujua, na ngazi za ukuruba,
Malimati yakiliwa, huliwa kwenye ujuba,
Na malezi machelewa, heri wasio na baba,
Huo wote hautoshi, wape nchi watashiba ?

Sunday, November 18, 2012

MJA KUDAI UHURU ...



Nani kasema makosa, mtu uhuru kudai,

Hata na wansiasa, hivi hili hawajui,

Kioja nakitomasa, ya rafiki na adui,

Mja uhuru kudai, hivi huwa ni makosa ?



Zama hizi za kunesa, rafiki huwa adui,

Pasina na kudodosa, mfu hugeuka hai,

Na hai ukamkosa, maiti kumsabahi,

Mja uhuru kudai, hivi huwa ni makosa ?



Maisha sio asusa, sio ndoa si nikahi,

Kuna saa na hamasa, na kutafuta uhai,

Wakati unapopasa, uhuru ni yako rai,

Mja uhuru kudai, hivi huwa ni makosa ?



Utumwa sio anasa, hali tu haizuii,

Dhiki ukishazitosa, usiwe hujitambui,

Hii swala sio misa, na wala si jinai,

Mja uhuru kudai, hivi huwa ni makosa ?



Kule na huku pepesa, kisha upate na rai,

Moyoni likikutesa, kulitoa si nishai,

Bali ndani ukisusa, moyo huwa hautulii,

Mja uhuru kudai, hivi huwa ni makosa ?



Maisha kupiga msasa, na kunoa maslahi,

Uso ukiupapasa, ikawa ni asubuhi,

Majini ukijitosa, hukurejea uhai,

Mja uhuru kudai, hivi huwa ni makosa ?



Kalipateni darasa, msiwe ni ndugu mui,

Msiozijua siasa, ila njaa kukinai,

Yapasayo kudodosa, dunia kutanabahi,

Mja uhuru kudai, hivi huwa ni makosa ?



Hii haijesha posa, wazazi hawatambui,

Yadaiwa kudodosa, zilizopo leo rai,

Ni bure kujitakasa, hali mchafu wajihi !

Mja uhuru kudai, hivi huwa ni makosa ?



Usultani wautaka


Hamnao visiwani, sasa bara wabakia,

Kama vile ni utani, vyamani wajipandia,

Ingawa siliamini, ndilo linalotokea,

Usultani wautaka, waliokuwa hawana !



Umeisha visiwani, bara ndio waingia,

Wanaupanda maweni, na mafuta kumwagia,

Kila nikitathmini, ninashindwa kuelewa,

Usultani wautaka, waliokuwa hawana !



Huu ni uafkani, kitu gani inakuwa,

Kina nani majinuni, hali wasiyoijua,

Watumia dira gani, huku wanakoelekea ?

Usultani wautaka, waliokuwa hawana !



Seyyid Said ngamani, omoni kesharejea,

Kafufukia Omani, mjini akaingia,

Ila sio visiwani, Mrima ametulia,

Usultani wautaka, waliokuwa hawana !



Na wameanza kuhani, mzimu kuillilia,

Nywele zao kichwani, kalkiti wanatia,

Zipate kuwa laini, umanga kukurubia,

Usultani wautaka, waliokuwa hawana !



Weusi wauzaini, weupe kukimbilia,

Wajipaka vihinani, ngozi wakajichibua,

Weupe wapate winii, heshima juu kupaa,

Usultani wautaka, waliokuwa hawana !



Ya wengine si amini, huwa yansiginiwa,

Roho haziwi laini, kwao wasichokizaa,

Ila hutia imani, kwa sadaka kutoa,

Usultani wautaka, waliokuwa hawana !



Huibia masikini, wenye shibe wakapewa,

Wajumbe wakaamini, nchi watawagawia,

Wasiache usukani, daima kushikilia,

Usultani wautaka, waliokuwa hawana !



Wajivukiza ubani, na marashi kujitia,

Wakageuza peponi, hii ya kwao dunia,

Wanajua hawaioni, ya kweli iliyokuwa,

Usultani wautaka, waliokuwa hawana !



Walalao amesheni, sultani kumpokea,

Katokea ugenini, nyumbani anaingia,

Ameona kitu gani, bado mimi sijajua,

Usultani wautaka, waliokuwa hawana !



NgazI zao waamini, imara zilizokuwa,

Waanzia vijijini, na mjini wakatua,

Na kisha wilayani, kufikia wa mkoa,

Usultani wautaka, waliokuwa hawana !



Kisha huja taifani, makungi kujigawia,

Kuuenzi Usultani, kwenye mpya Tanzania,

Wanatafuta waghani, sasa waje wasifia,

Usultani wautaka, waliokuwa hawana !







Mtumwa akishalewa


Mtumwa akishalewa, shairi hujitungia,

Pombe akaisifiwa, na mpishi kupambiwa,

Kisha akawarukia, uhuru wanaolilia,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Kicheko hukiangua, habari akisikia,

Kuna wanaolilia, uhuru kujipatia,

Ya kwao wakaamua, wapate kuendelea,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Senti imemlevyea, hawezi jielewa,

Kichwani imeingia, ya kutunzwa na kupewa,

Uimbaji anajua, bwanawe kumsifia,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Hii ni yenu dunia, mbingu sijaandikia,

Huku yao wnajua, uhuru walishapewa,

Ila nyie wa kuwia, msiowia raia,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Mtumwa anaridhia, bwanawe kumtumia,

Chakula akipatiwa, hanalo la kuamua,

Kutumwa anangojea, kwingine asokujua,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Shurubu huidhania, yeye ameandikiwa,

Ndivyo alivyozaliwa, lingine kutotegemea,

Mnyenyekevu huwa, hata panapo udhia,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Hujikunyata mkiwa, mama akitulkaniwa,

Uso akakumbatia, milizamu kuzuia,

Huwa anafikiria, haki yake inakuwa,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Haki yake inakuwa, yeye akatukaniwa,

Kisha akadhulumiwa, na budi kuitikia,

Vingine akiamua, ni mkosa yeye huwa,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Huituhumu dunia, kuwa inamuonea,

Kumbe yeye karidhia, kile kisichoridhiwa,

Na tokea kuzaliwa, ni huru aliyekuwa,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Dunia ihofia, kuwa itamchezea,

Akashindwa kutambua, akili katunukiwa,

Naza akizitumia, ufukara huua,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Wanaokung'ang'ania, kuna lao waambua,

Fika wanalitambua, hasara kukuachia,

Mwenye njaa wanjua, ni rahisi kutumiwa,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Ndivyo ilivyo dunia, wajinga hufurahia,

Hawajengi huezua, hata waliyojengewa,

Wa kale wangelikuwa, haya wangeliyakataa,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Mtumwa akishalewa


Mtumwa akishalewa, shairi hujitungia,

Pombe akaisifiwa, na mpishi kupambiwa,

Kisha akawarukia, uhuru wanaolilia,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Kicheko hukiangua, habari akisikia,

Kuna wanaolilia, uhuru kujipatia,

Ya kwao wakaamua, wapate kuendelea,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Senti imemlevyea, hawezi jielewa,

Kichwani imeingia, ya kutunzwa na kupewa,

Uimbaji anajua, bwanawe kumsifia,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Hii ni yenu dunia, mbingu sijaandikia,

Huku yao wnajua, uhuru walishapewa,

Ila nyie wa kuwia, msiowia raia,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Mtumwa anaridhia, bwanawe kumtumia,

Chakula akipatiwa, hanalo la kuamua,

Kutumwa anangojea, kwingine asokujua,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Shurubu huidhania, yeye ameandikiwa,

Ndivyo alivyozaliwa, lingine kutotegemea,

Mnyenyekevu huwa, hata panapo udhia,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Hujikunyata mkiwa, mama akitulkaniwa,

Uso akakumbatia, milizamu kuzuia,

Huwa anafikiria, haki yake inakuwa,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Haki yake inakuwa, yeye akatukaniwa,

Kisha akadhulumiwa, na budi kuitikia,

Vingine akiamua, ni mkosa yeye huwa,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Huituhumu dunia, kuwa inamuonea,

Kumbe yeye karidhia, kile kisichoridhiwa,

Na tokea kuzaliwa, ni huru aliyekuwa,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Dunia ihofia, kuwa itamchezea,

Akashindwa kutambua, akili katunukiwa,

Naza akizitumia, ufukara huua,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Wanaokung'ang'ania, kuna lao waambua,

Fika wanalitambua, hasara kukuachia,

Mwenye njaa wanjua, ni rahisi kutumiwa,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Ndivyo ilivyo dunia, wajinga hufurahia,

Hawajengi huezua, hata waliyojengewa,

Wa kale wangelikuwa, haya wangeliyakataa,

Mtumwa akishalewa, uhuru ataucheka !



Wajumbe tena hatuna



Wajumbe tumepoteza, watumwa wanabakia,

Viumbe wakujiuza, mfukoni wametiwa,

Kwa sasa ni kama viza, yai lisilotufaa,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Wajumbe wachiuza, uwakilishi kuua,

Nchi tunaipoteza, kama nguo kuivua,

Uchi kujitembeza, ikatucheka dunia,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Kazi wanaoongoza, wanasiasa Tanzania,

Vyama bila kutangaza, hakuna asiyejua,

Ujumbe sasa kujiuza, na kura ikanunuliwa,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena hatuna !



Dini ilishapoteza, udini wakataliwa,

Ila roho wanauza, kuizuia dunia,

Wadhania waongoza, kumbe wanaangamia,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Ni samaki wameoza, kwenye tenga walojaa,

Vikundi wanavyokuza, vya njaa kujigangia,

Fedha wanatanguliza, Nyerere alohofia,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Siasa waendeleza, ufukara kuulea,

Wao wanavyoangaza, utumwa wasaidia,

Njaa watu ikiliza,mkubwa unabakia,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Hawataki kuongoza, umaskini kutoa,

Wajua haya wakifanza, uhutu twajipatia,

Na kuringa tutaanza, kurani kuwakataa,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Hivyo wanang'ang'aniza, ufukara kubakia,

Kwao ngao wanatunza, ukubwa kutopotea,

Ajabu ya muujiza, na ibra ya dunia,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Heshima waipoteza, wao wanajisifia,

Hata watoto wajuza, ni kicheko imekuwa,

Baba na mama kutunzwa, ardhi wakaiachia ?

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Na tena wanachotunzwa, ni chache zao rupia,

Thamani zimepoteza, kitu hazitosaida,

Laiti wangejitunza, tajiri wangelikuwa,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Mazoe kumbe kuoza, wachache wanaojua,

Kila unapoangaza, hali ukakubalia,

Kumbe juu ungeweza, aliye akuzuia,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Akili wanakuteza, na mitego kukwekea,

Wajua hujui tunza, wala kujitafutia,

Hivyo wanakulemaza, waweze kukutumia,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !









Fukara wa uongozi


Ni mkubwa masikini, akosaye uongozi,

Huishia taabani, asipate usingizi,

Raha awe haioni, nyumbani na matembezi,

Fukara wa uongozi, ni mkubwa masikini !



Ukiipanga thamani, kwanza upe uongozi,

Huu ukiwa makini, zote utapanda ngazi,

Dhaifu ukiauni, mazingira huyawezi,

Fukara wa uongozi, ni mkubwa masikini !



Huchahia akilini, pasiwe na mageuzi,

Wenyewe ukajihini, kwa kuukosa uwazi,

Chenga ukaziamini, magoli ni upandizi,

Fukara wa uongozi, ni mkubwa masikini !



Huathirika moyoni, hauwezi maamuzi,

Uliokuwa laini, kwa hariri vitambazi,

Na msingi huuini, kuja kufanza majenzi,

Fukara wa uongozi, ni mkubwa masikini !



Mipango hujizaini, ikawa na utatizi,

Mikakati kutahini, ikawa ni kubwa kazi,

Rasilimali kuhini, ni ajizi si ujuzi,

Fukara wa uongozi, ni mkubwa masikini !



Inapokufa imani, hukuambaa mwenyezi,

Akakuacha uwani, barazani kubarizi,

Ulicho nacho kichwani, tena kisiwe azizi,

Fukara wa uongozi, ni mkubwa masikini !



Atakaye jiamini, aloweza haliwezi,

Ajitiaye imani, anajua uongozi,

Hufulia hadharani, mafichoni ajienzi,

Fukara wa uongozi, ni mkubwa masikini !



Niepushie Manani, mimi kwako si mjuzi,

Pasina yako ilani, kazi hii siiwezi,

Niongoze mashakani, kivulini nibarizi,

Fukara wa uongozi, ni mkubwa masikini !



Watoto wanaoua




Naiuliza dunia, ukweli ikanambia,

Tofauti sijajua, watoto wanaoua,

Na Hitler mlaniwa, yahudi aliyeua,

Yahudi walioua, na watoto wanaoua:

Wana tofauti gani ?



Kila nikiangalia, tofauti sijajua,

Ninachokiangalia, ni mama waliofiwa,

Watoto wawalilia, nani faraja kutia?

Yahudi walioua, na watoto wanaoua:

Wana tofauti gani ?



Sabbu tena kwa mamia, wanaweza kuzitoa,

Ila hatutaelewa, huruma twajionea,

Kimbari kinatokea, watu wanaangalia ?

Yahudi walioua, na watoto wanaoua:

Wana tofauti gani ?



Rahmani yangu dua, siwachi kukuachia,

Haya umeyaachia, bado yanaendelea,

Sababu unaijua, mimi sijaigundua,

Yahudi walioua, na watoto wanaoua:

Wana tofauti gani ?



T U S U B I R I


Mimi mtu wa saburi, haraka naiachia,

Lenu lenye ushauri, siwezi kulikataa,

Na kama nikusubiri, hilo nimeliridhia,

Tungojee, tusubiri, nami nasubiri nanyi !



Hamwezi kuomba heri, shari nije wagaia,,

Ninalijua kaburi, na ndani kinachokuwa,

Hilo kwangu sio siri, uhai sijafulia,

Nanyi nami nasubiri, kifuatacho kujua !



Ishara mkidhamiri, siwezi waongopea,

Mimi sio mashuhuri, na utume sijapewa,

Hata huo ubashiri, ni yangu najisemea,

Nanyi nami nasubiri, kifuatacho kujua !



Hakika sina jeuri, ya nuru kukaribia,

Ila kinachodhihiri, huazimu kuwaambia,

Ila pali0o sifuri, duarani hubakia,

Nanyi nami nasubiri, kifuatacho kujua !



Ni mwepesi wa kupanga

Barri ni mwenye kujua, hata tusiyoyajua,

Na anapotangulia, wasiwasi hututoa,

Tusijifanye twajua, chicha tukaambulia,

Ni mwepesi wa kupanga, huwezi shindana naye !



Asili tunaijua, twakubali nunuliwa,

Mfukoni tukatiwa, ya wengine kuriddhia,

Hali fika tunajua, twaweza jitegemea ?

Ni mwepesi wa kupanga, huwezi shindana naye !



Yetu tukijipangia, mbele budi kusogea,

Kuna ndugu wangojea, mkono kutupatia,

Vigumu haitakuwa, dini yetu waijua,

Ni mwepesi wa kupanga, huwezi shindana naye !



Hadithi zasimuliwa, bara yaliyotokea,

Jerumani kashupaa, udini kuutambua,

Hisabu wakachafua, ili kwenda waridhia,

Ni mwepesi wa kupanga, huwezi shindana naye !



Ndio kisa kukataa, ubaya lisilokuwa,

Mbona leo twasikia, Marikani waridhia,

Kura walipojipigia, dini siri haikuwa,

Ni mwepesi wa kupanga, huwezi shindana naye !



Ujanja wakitumia, pabaya wanatutia,

Wajifanyao kujua, ikawacheza dunia,

Aibu yawaingia, hadi nje wahofia ?

Ni mwepesi wa kupanga, huwezi shindana naye !



Data kaziye kuzaa, yote nje kuanikwa,

Vingine haijakuwa, uongo unapotia,

Kazi hazitowafaa, hubakia kuchezewa,

Ni mwepesi wa kupanga, huwezi shindana naye !



Takwimu zakuchambua, kisha zikabanguliwa,

Zinakuwa na udhia, kupikwa huja kataa,

Chunguni kinachotiwa, kibichi kikabakia,

Ni mwepesi wa kupanga, huwezi shindana naye !



Mwizi wa fikira




Mwizi wa fikira mwizi, kingine hawezi kuwa,

Tabiaye udokozi, ya watu kuyachukua,

Kisha kwenda kuyahodhi, kuwa yake kujitia,

Fikra mwenye kuiba, sikuzote huwa mwizi !



Watazame waenezi, jinsi wanavyodokoa,

Hii ndiyo yao kazi, sasa wanaajiriwa,

Na utundu hawawezi, jema wakalipanua,

Fikra mwenye kuiba, sikuzote huwa mwizi !



Wageuka wachuuzi, wakubwa kuwauzia,

Wakaachia machozi, Baadi kuwaachia,

Mrahaba kuwaizi, ya kwao wakajilia,

Fikra mwenye kuiba, sikuzote huwa mwizi !



Anayaona mwenyezi, sadaka sasa watoa,

Kwake bado wana enzi, siku ya kuahidiwa,

Kisha wote majambazi, huko kwenda kudaiwa,

Fikra mwenye kuiba, sikuzote huwa mwizi !



Tutu, Kofi, Carter na Mary


Wazee mmechaguliwa, dunia kutumikia,

Heri ninawatakia, ya kwenu kufanikiwa,

Mola atawasaidia, kwa wengine kuwafaa,

Tutu, Kofi, Carter na Mary, Mola daim'awe nanyi !



Mwastahii radhia, heshima mliyopewa,

Kwani hamjapungukiwa, na jukumu mmetwaa,

Bila hata kulilia, zaidi juu kikawa,

Tutu, Kofi, Carter na Mary, Mola daim'awe nanyi !



Kote mnakotembelea,, baraka nawaombea,

Mguu wenu kuwa dawa, kila mnapoingia,

Na maneno nuru kuwa, wata njia wakajua,

Tutu, Kofi, Carter na Mary, Mola daim'awe nanyi !



Uzee watuzidia, inazeeka dunia,

Hili mkalitambua, na kati kuingilia,

Wengi sana twafulia, pasina wa kutwangalia,

Tutu, Kofi, Carter na Mary, Mola daim'awe nanyi !



Nchini mwetu wakaa, vya kwao wakajilia,

Pensehni wanapewa, nini kujihangaikia,

Ndipo walipofikia, mbali hawajaangalia,

Tutu, Kofi, Carter na Mary, Mola daim'awe nanyi !



Wazee wenzao pia, washindwa kuangalia,

Ila wawaachia wajanja kuwatumia,

Vizee vigange njaa, yao bila kutatuliwa,

Tutu, Kofi, Carter na Mary, Mola daim'awe nanyi !



Makubwa mkiaangalia, na madogo kuyajua,

Wanyonge wategemea, nafuu kujionea,

Dunia kuwasikia, kwenu nyie kupitia,

Tutu, Kofi, Carter na Mary, Mola daim'awe nanyi !



Dhaifu kusaidia, na wanyonge kuinua,

Wapate jitegemea, bila kuwategemea,

Uhai kumalizia, pasina ya kuumia,

Tutu, Kofi, Carter na Mary, Mola daim'awe nanyi !



Uhuru asiye nao



Hawi mtu wa busara, uhuru asiyekuwa,

Mtu huyo wa hasara, huwezi kumtumia,

Huwa ni simba marara, hata fisi hukimbia,

Uhuru asiye nao, hawi mtu wa busara!



Hawezi nukuu sura, wala aya kufatia,

Maisha yake kuchora, kuandika hatajua,

Duniani husowera, hawezi kutangulia,

Uhuru asiye nao, hawi mtu wa busara!



Uzee huwa madhara, na watu hatowafaa,

Akaingia ujura, viporo kuambulia,

Akillilia nusura, kwa kesho asiyeijua,

Uhuru asiye nao, hawi mtu wa busara!







TAIFA BILA YA BABA ...


UBABA waukataa, uchamawanalilia,

Hayo ndiyo majaliwa, mwanangu binti mkiwa,

Babu kakuondokea, na baba hukujaliwa,

Taifa bila ya baba, huwa ukiwa mkubwa !



Baba mwema ni ulua, wana wanajivunia,

Nyumbani akiingia, huwa wamkimbilia,

Na kicheko kuangua, shibe wakajishibia,

Taifa bila ya baba, huwa ukiwa mkubwa !



Na baba asipokuwa, nyumba huwa yatitia,

Ukimya ukajaa, na giza ndani ikawa,

Nuru yote hupotea, na unyevu kuingia,

Taifa bila ya baba, huwa ukiwa mkubwa !



Aali wastahili



Akili zikifulia, madoho huyaridhia,

Mbali hautoyajua, wala hutojionea,

Yako ukayadhania, ni makubwa yamekuwa,

Aali wastahili, tumeangusha wananchi !



Yetu ukiangalia, sisi nyuma twabakia,

Sote tulipoanzia, sawasawa ilikuwa,

Kundi ukilichukua, twadorora Tanzania,

Aali wastahili, tumeangusha wananchi !



Ni bure kujisifia, kwa ukweli lisokuwa,

Ili wende hurumiwa, wembe ukiandaliwa,

Kinyozi hajajinyoa, naye huomba nyolewa,

Aali wastahili, tumeangusha wananchi !



Ila walioingia, mashine wanatumia,

Hiyo hiyo hutumia, na wao wakajinyoa,

Kisha wakatuzingua, na hasira kututia,

Aali wastahili, tumeangusha wananchi !



Mengine ni kunyamaa, sauti kutotoa,

Chumvi ukizidishia, chakula hakitaliwa,

Kwanza mngeliyajua, uzito kujipimia,

Aali wastahili, tumeangusha wananchi !



Pande mkaangalia, ni wapi imezidia,

Kama kwenu imekua, hayao yenu manufaa,

Wengine huangalia, kama wana manufaa,

Aali wastahili, tumeangusha wananchi !



Kitu wasipoambua, vipi watakusifia,

Mtu bora kujijua, na hadhara kuijua,

Wapo wa kushangilia, kwa malipo kugaiwa,

Aali wastahili, tumeangusha wananchi !







Umasikini uchafu



Sio la kuliringia, hili linapotokea,

Ni aibu hututia, na wengine kukimbia,

Haya ikawaingia, wote wanaojijua,

Umasikini uchafu, unafaa kufagiwa!



Nchi hutia madoa, na mabaka kuzagaa,

Watu yakawaumbua, kila walipotulia,

Mgeni kuwa udhia, haya akijionea,

Umasikini uchafu, unafaa kufagiwa!



Vya msingi vyatakiwa, waziri kutuambia,

Kwanini tunafulia, haviwezi tengamaa,

Ni ishara za balaa, wageni wazihofia,

Umasikini uchafu, unafaa kufagiwa!



Nchi isiyo maua, nani kuitembelea,

Kwa maji tunafulia, wapi yanakopitia,

Bustani zaugua, bima hazikujaliwa,

Umasikini uchafu, unafaa kufagiwa!



Nchi haina kung'aa, nani kuifurahia,

Ni vichaka imekua, na dampo ni majaliwa,

Mvuto unapotea, kipi cha kujionea ?

Umasikini uchafu, unafaa kufagiwa!



Ya msingi yatakiwa, kufanya Watanzania,

Na nyie wa kutembea, mnaoingia Ulaya,

Nchi mmejionea, usafi zinavyokuwa,

Umasikini uchafu, unafaa kufagiwa!



Mbona kwetu ni kinyaa, h ata tunajichukia,

Hili kweli latakiwa, nalo likasaidiwa,

Au kujipanga waa, na mwanawe ndiye jaa ?

Umasikini uchafu, unafaa kufagiwa!





Aali wastahili



Akili zikifulia, madoho huyaridhia,

Mbali hautoyajua, wala hutojionea,

Yako ukayadhania, ni makubwa yamekuwa,

Aali wastahili, tumeangusha wananchi !



Yetu ukiangalia, sisi nyuma twabakia,

Sote tulipoanzia, sawasawa ilikuwa,

Kundi ukilichukua, twadorora Tanzania,

Aali wastahili, tumeangusha wananchi !



Ni bure kujisifia, kwa ukweli lisokuwa,

Ili wende hurumiwa, wembe ukiandaliwa,

Kinyozi hajajinyoa, naye huomba nyolewa,

Aali wastahili, tumeangusha wananchi !



Ila walioingia, mashine wanatumia,

Hiyo hiyo hutumia, na wao wakajinyoa,

Kisha wakatuzingua, na hasira kututia,

Aali wastahili, tumeangusha wananchi !



Mengine ni kunyamaa, sauti kutotoa,

Chumvi ukizidishia, chakula hakitaliwa,

Kwanza mngeliyajua, uzito kujipimia,

Aali wastahili, tumeangusha wananchi !



Pande mkaangalia, ni wapi imezidia,

Kama kwenu imekua, hayao yenu manufaa,

Wengine huangalia, kama wana manufaa,

Aali wastahili, tumeangusha wananchi !



Kitu wasipoambua, vipi watakusifia,

Mtu bora kujijua, na hadhara kuijua,

Wapo wa kushangilia, kwa malipo kugaiwa,

Aali wastahili, tumeangusha wananchi !





Mambo ni kufatilia




UDHIBITI kipungua, tija nayo hupungua,

Kazi wanaopangiwa, budi kufuatiliwa,

Wafanyacho kukijua, na kinavyoendelea,

Mambo ni kufatilia, sio ovyo kuachia !



Ovyo ukiyaachia, hawezi kufanikiwa,

Lazima utafulia, wengine wakaogea,

Feli zataka hatua, mja zote kuzijua,

Mambo ni kufatilia, sio ovyo kuachia !



Vipimo kuvichukua, mambo ukalingania,

Kujaa ukakujua, pia hata kupungua,

Hasara na manufaa, iwe rahisi kujua,

Mambo ni kufatilia, sio ovyo kuachia !



Ndivyo ilivyo dunia, na maisha yatambua,

Vingine yakiachiwa, huw amkubwa udhia,

Kila mwenye kuyajua, ni akili hutumia,

Mambo ni kufatilia, sio ovyo kuachia !

Zanzibar bado lulu



SABABU haitokuwa, madaraka kuatiwa,

Yake ikayaamua, yawezayo kuifaa,

Vingine inapokuwa, utumwa utarejea,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Pacha wanatambuliwa, muungano kuridhia,

Ila bado ni jamaa, tofauti inakuwa,

Bara yao familia, kadhalika Zanzibar,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Kila mtu anajua, wadini hatujakuwa,

Kiwacho ni yetu njaa, chakula tunafulia,

Si uongo nawambia, hali yetu naijua,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Vyovyote waweza kuwa, bara wanavyoamua,

Ila sisi twajijua, Islamu twajaliwa,

Vingine haitakuwa, hadi mwisho wa dunia,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Dini wanaoichafua, nyie mmewaridhia,

Dawa yenu kuwatoa, tawba tukaivua,

Kesi kutotuachia, kwa ubaya kuanzia,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Usaliti haijawa, kutaka jitegemea,

Kama ndio ingekuwa, kusingekuwa na ndoa,

Watoto wakazuiwa, kwa nyumbani tu kukaa,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Ni nzuri hii nia, nchi kujitegemea,

Yake ukiyaamua, tasihili kwendlea,

La keshokutwa likawa, hivi leo latokea,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Mkoa haitakuwa, nchi huru tunajua,

Katiba inaridhia, malezi kujifanzia,

Mipango ikaibua, nchi ikainyanyua,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Viko vidogo visiwa, ubora vimejaliwa,

Seychelles wanapaa, sisi tunaogelea,

Mbeleko kutoitoa, kisiasa ni udhia,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Jana tungeliamua, kuuza na kununua,

Ndio kazi kubwa kuwa, Afrika kutufaa,

Fursa tunachezea, twangoja kusaidiwa ?

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Sadaka tunachukua, wazima tuliokuwa,

Dini hili lakataa, jasho budi kulitoa,

Fikirini maridhia, ujinga msioujua,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Macau waendelea, sisi nyuma twabakia,

Singapore nayo pia, nusu hawajafikia,

Baraka twazichezea, kw autoto kujitia,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Wakubwa tumeshakua, bara kuisadiia,

Na mojawapo ya njia, ni uhuru kuamua,

Yetu tukajifanyia, pande zote kutufaa,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Zanzibar iling'aa, mwanga bara kuingia,

Leo gizani twakaa, yatutania dunia,

Amkeni Wazanzibar, Afrika kuifaa,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Dubai kuifikia, sio kazi itakuwa,

Ila tukishaamua, mambo kujiandalia,

Pawe kweli na ubia, wa nchi kuinyanyua,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Sauti watasikia, wa Mrima walokuwa,

Zikaingia bidhaa, kwenda kote kusambaa,

Bei rahisi ikiwa, nasi juu tutakuwa,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Kiwanja kukipanua, kimataifa kikawa,

Mithili Dubai kuwa,ndege kwa wingi kutua,

Kubwa zilizokuwa, vikubwa kuvinyanyua,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Bandari kuitanua, manowari kuingia,

Na meli za abiria, malefu kutuletea,

Nchini kuja tumia, hazina yetu kujaa,

Na meli za abiria, maelfu kuingia,



Viwanja vinatakiwa, kukimbia motokaa,

Hiyo moja Formula, kwa Pemba pia Unguja,

Mashindano kwandaa, wageni tele kujaa,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Golfuu inatakiwa, upya kuifufua,

Viwanja tulivyoua, basi vipya kuzaliwa,

Ni mchezo maridhia, waucheza bilionea,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Viwili vyaweza kuwa, kwa Pemba na Zanzibar,

Sayakati kuingia, tuitingishe dunia,

Golfu ikasaidia, umaskini kuutoa,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Utalii watakiwa, wa wananchi ukawa,

Msaada kupatiwa, ya kwao kujifanyia,

Vibanda kujijengea, na hadhi vilivyokuwa,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Watalii wafurahia, nyumbani kuja kukaa,

Na wa jamii ukiwa, mgahawa utafaa,

Asili kujionea, na utamaduni pia,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Hili wanalokataa, uchumi wanafulia,

Wanashindwa kuelewa, inakokwenda dunia,

Aproni wang'ang'ania, kitu isiyowafaa,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!





Mola umenisikia, nilipoiomba dunia,

Zanzibar kujalia, ipate kuendelea,

Kwa yake kuyaamua, bara ikisaidia,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Watu kuwazidishia, dhiki zipate pungua,

Maisha yatuonea, furaha inakimbia,

Nawe unajionea, na ukweli waujua,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Sadaka ninaitoa, shairi kuwatungia,

Baraka lazingojea, ili kazi kufanziwa,

Kama zana kuja kuwa, nchi ipate jaliwa,

Kama nchi Zanzibar, yastahili kuamua!



Zanzibar

Novemba 14, 2012











DHAMANA



Ukubwa mkiupewa, wakubwa hamjakuwa,

Vibaya mwachukulia, hicho mnachoachiwa,

Madaraka huachiwa, sio ya kuyachukua,

Zirudisheni dhamana, sio yenu mamlaka !



Mwaachiwa kutumiwa, kwa haki inavyokuwa,

Nyenzo hii hutumiwa, walio wengi kufaa,

Ndipo sawa inakuwa, sio vingine kwamua,

Zirudisheni dhamana, sio yenu mamlaka !



Wewe ukiiutmia, mwenyewe kutumikiwa,

Ukapata manufaa, halali yasiyokuwa,

Ni wizi watumia, wala sawa haijawa,

Zirudisheni dhamana, sio yenu mamlaka !



Kaziyo kutumikia, na sio ya kutumiwa,

Kama hivyo inakuwa, unaianza balaa,

Vipi kukuchukulia, kiongozi ulokuwa ?

Zirudisheni dhamana, sio yenu mamlaka !



Yataka kujisimamia, la halali kulijua,

Muumba akakujua, uongozi wakufaa,

Sio ukanyenyekea, kile tusichokijua,

Zirudisheni dhamana, sio yenu mamlaka !



Mamlaka ya raia, haki inavyotambua,

Katiba inalijua, waziwazi linakuwa,

Ila huzuka hadaa, watu wakazainiwa,

Zirudisheni dhamana, sio yenu mamlaka !



Wenye vyeo kudhania, nchi yao imekuwa,

Ovyoovyo kuamua, na ya kweu kukataa,

Hilo mwisho lafikia, macho wameshayafungua,

Zirudisheni dhamana, sio yenu mamlaka !



Heri hili kutambua, tujenge demokrasia,

Ya kweli iliyokuwa, wala sio ya snaa,

Mida imeshaingia, mageuzi kuingia,

Zirudisheni dhamana, sio yenu mamlaka !



Pepo zinakurubia, nafasi kuichukua,

Ombwe nje kulizoa, la haki kuzingatiwa,

Mwaka hautoishia, mengi tutayasikia,

Zirudisheni dhamana, sio yenu mamlaka !





VIJIJI



Vijiji mkipuuza, mijini kutakalika ?

Si watu mwawakimbiza, mijini kuja furika ?

Ajizi mnayofanza, vigumu kueleweka,

Mkipuuza vijiji, kutakalika mijini ?



Jambo hili lashangaza, mipango 'kiangalia,

Ghafla tulijaikwaza, katikati kuachia,

Hivi leo tunaiza, hata kwenda tembelea ?

Mkipuuza vijiji, kutakalika mijini ?



Twashindwa kujieleza, upacha uliokuwa,

Vijiji Kulwa mpuuzwa, na Doto muweza njia ?

Usawa tusiposambaza, udugu utaachia,

Mkipuuza vijiji, kutakalika mijini ?



Tukajazua ya viza, uhuni na mabalaaa,

Wakashtuka ajuza, na shaibu kujikwaa,

Wataraji miujiza, uovu ukazuia,

Mkipuuza vijiji, kutakalika mijini ?





Mshairi sikuhizi



Waliozoea hadhi, kwa ubwabwa na mandazi,

Washairi sikuhizi, huwa haviwapendezi,

Waelimika wajuzi, kuyatafuta azizi,

Mshairi sikuhizi, kaziye si kusifia,

Wanasonya viongozi, sasa wamnyanyapaaa !



Wanaotafuta mapenzi, wale sifa za Muizzi,

Kitu hawaokotezi, wakataa ubazazi,

Hali mashehe wa enzi, wafulia kwa hirizi,

Mshairi sikuhizi, kaziye si kusifia,

Wanasonya viongozi, sasa wamnyanyapaaa !



Ajijua si mkazi, majoho hayadarizi,

Wala siye muamuzi, ya watu hayatatizi,

Ajijua kiongozi, njia bora msimamizi,

Mshairi sikuhizi, kaziye si kusifia,

Wanasonya viongozi, sasa wamnyanyapaaa !



Huyu ni muangalizi, kuukataa ushenzi,

Tukamhofu Mwenyezi, na dunia kutoenzi,

Wala hanayo ajizi, yakitua mageuzi,

Mshairi sikuhizi, kaziye si kusifia,

Wanasonya viongozi, sasa wamnyanyapaaa !



Hakika ni muenezi, ya ovyo hayatangazi,

Asiyekwaza uwazi, iwe jana au juzi,

Ya umma ni mdowezi, haumalizi utenzi,

Mshairi sikuhizi, kaziye si kusifia,

Wanasonya viongozi, sasa wamnyanyapaaa !



Mipango ni msimamizi, mizuri si ya kichizi,

Kuyaleta mapinduzi, vya msingi kuvienezi,

Maji yakawa utenzi,usioisha simulizi,

Mshairi sikuhizi, kaziye si kusifia,

Wanasonya viongozi, sasa wamnyanyapaaa !



Chakula kikawa dozi, hakikosi mwanagenzi,

Vijiji wakapalizi, na mjini kuhifadhi,

Pakafanzwa na makuzi, uuzaji na uzuzi,

Mshairi sikuhizi, kaziye si kusifia,

Wanasonya viongozi, sasa wamnyanyapaaa !



Nyumba zataka ujenzi, kama la kwanza zoezi,

Watu ukiwahifadhi, mengine watafaridhi,

Pakiwa nayo ajizi, ufukara uko wazi,

Mshairi sikuhizi, kaziye si kusifia,

Wanasonya viongozi, sasa wamnyanyapaaa !



Hapanao utetezi, ila siasa chukizi,

Zitakazo kujienzi, na wengine kuwaizi,

Kwangu mimi machukizi, walal hazina hifadhi,

Mshairi sikuhizi, kaziye si kusifia,

Wanasonya viongozi, sasa wamnyanyapaaa !

MPITO


Ndivyo ilivyo dunia, wakati unafikia,

kwa nchi kujapitia, nafasi ya kujizaa,

Kamampya ikawa, au mbovu kuchakaa,

Kipindi hiki cha mpito, kazi kujilimbikizia !



Tumeacha ujamaa, ubepari twakumbatia,

Na mpito inakuwa, vya watu kuvichukua,

Kwa halali ya kuzua, na haramu ya kulea,

Kipindi hiki cha mpito, kazi kujilimbikizia !



Kiwewe wameingia, watu sasa kusifiwa,

Kwa ukubwa kuzidia, na fahari kuenea,

Kila mpenda dunia, yakini ni yake njia,

Kipindi hiki cha mpito, kazi kujilimbikizia !



Waililia dunia, udugu wakidhania,

Na milele watakaa, hawawezi kuugua,

Ila yawanyanyapaa, na wao hawajajua,

Kipindi hiki cha mpito, kazi kujilimbikizia !



Haiwapendi dunia, yawaona ni udhia,

Na hasa mnaokua, watukufu mmekua,

Kila siku inalia, lini mtaondolewa ?

Kipindi hiki cha mpito, kazi kujilimbikizia !



Yataka badilishiwa, wa heri ikapatiwa,

Si laana kuchukua, kitu isiyosaidia,

Muumba wamuambia, ni nini watufanyia ?

Kipindi hiki cha mpito, kazi kujilimbikizia !



Dhaifu twahitajia, dhalili waliokuwa,

Wanaokusujudia, na sifazo kuzitoa,

Hadi machozi kulia, kila wakikukumbukia ?

Kipindi hiki cha mpito, kazi kujilimbikizia !



Mizigo watuachia, kitu isiyotufaa,

Rabana twakulilia, hima kutupunguzia,

Mpito ukiishia, tuje wema kujaliwa,

Kipindi hiki cha mpito, kazi kujilimbikizia !





MIUNGU WATU


WALE na waitumie, waliokwishajaliwa,

Katu wasinihurumie, wala kuja nigawia,

Razaki nimjuae, yangu atanipatia,

Mola wanaojifanya, sitaki fadhila yao !



Ya kwao niwaachia, yangu nitajifanyia,

Pamwe na maruerue, wala siwezi sinzia,

Sintokihofu kiwewe, cha njaa na kuishiwa,

Mola wanaojifanya, sitaki fadhila yao !



Naomba nihurumiwe, yangu nikijifanyia,

Riziki nijipatie, ya halali ilokuwa,

Kivulini nijile, hata ni kavu ikiwa,

Mola wanaojifanya, sitaki fadhila yao !



Bure usijisumbue, vinono kuniletea,

Nenda navyo katumie, wewe kukusaidia,

Kiporo changu nachie, kukila naendelea,

Mola wanaojifanya, sitaki fadhila yao !



Mola wangu sio wewe, wala hauwezi kuwa,

Hili bora uelewe, vingine kutodhania,

Na moyo uufunguwe, ujue unaugua,

Mola wanaojifanya, sitaki fadhila yao !





JAMBAWAZI WA UKWELI


Huyo huwa ni kibaka, jambawazi hatokuwa,

Mchana anayecharuka, jirani kuwaibia,

Uteja unampika, hamu budi kuridhia,

Jambawazi wa ukweli, haibii masikini !



Haibii masikini, jambawazi wa ukweli,

Huona ni uhaini, mkubwa uso mithali,

Wenzie hawamwamini, budi kumshtakia,

Jambawazi wa ukweli, haibii masikini !



Awajua masikini, vipi atawaibia,

Awanyime afueni, mautini kuwatia,

Kafiri na muumini, huiona ni hatia,

Jambawazi wa ukweli, haibii masikini !



Ukiwaona mjini, fukara wawaibia,

Uwajue kwa yakini, ni mateja walokuwa,

Kamwe hawana thamani, masikini kuibia,

Jambawazi wa ukweli, haibii masikini !



Wakatia mafichoni, Uswizi kwenda chimbia,

Huku njaa taabuni, kila mtu analia,

Ya kwao madhumuni, hakika ni kutuua,

Jambawazi wa ukweli, haibii masikini !



Wanatuona ni nyani, thamani wanatutoa,

Na vyao waamini, ndivyo vilivyojaliwa,

Hakika ni hayawani, wenda uchi pasi 'jua?

Jambawazi wa ukweli, haibii masikini !



Wa ukweli ajijua, kwa watu ataka nini,

Si kununua udhia, au wengine kuwahini,

Maisha ayaelewa, na uhai athamini,

Jambawazi wa ukweli, haibii masikini !





KIONGOZI WA UKWELI


ZAMA za kujilimbia, zafaa wasiojijua,

Karibu wa kuangalia, wasiojua dunia,

Kitu wasiosikia, ila kujaliwa raha,

Kiongozi wa ukweli, hatojishibisha kwanza:

Huwashibisha raia.



Wa kweli anayekua, kula atajachelewa,

Mbele hatakimbilia, na sinia kachukua,

Ila nyuma atakaa, kikombe kakumbatia,

Kiongozi wa ukweli, hatojishibisha kwanza:

Huwashibisha raia.



Hatopenda kutumia, kwa kuwa nchi yatoa,

Mbali hatakimbilia, karibu kuangalia,

Watu hatosaidia, ila uwezo kuvua,

Kiongozi wa ukweli, hatojishibisha kwanza:

Huwashibisha raia.



Si wa kusimulia, ya watu kuyasikia,

Huchuja kwa hilo kawa, na vichujio kadhaa,

Yote akaangalia, kwa pembe zenye kuzua,

Kiongozi wa ukweli, hatojishibisha kwanza:

Huwashibisha raia.





Vichache huvichagua, vya haraka kuchanua,

Mkazo akatilia, kazi viweze fanziwa,

Hivyo vikishakua, vingi sana huvizaa,

Kiongozi wa ukweli, hatojishibisha kwanza:

Huwashibisha raia.



Watu wake huwajua, sio kuwasingizia,

Ugomvi wetu ni njaa, malau pia balaa,

Na dharau za mkaa, mweupe zisizofdaa,

Kiongozi wa ukweli, hatojishibisha kwanza:

Huwashibisha raia.



Kama vile motokaa, gia zake hutambua,

Ya kwanza ikishaingia, zingine zinafatia,

Ndivyo ilivyo dunia, yapo ya kutangulia,

Kiongozi wa ukweli, hatojishibisha kwanza:

Huwashibisha raia.



Halisi ninatambua, lipo hili lenye njaa,

Bei ukizitanzua, maisha nafuu huwa,

Wala si kujisifia, milioni wafulia,

Kiongozi wa ukweli, hatojishibisha kwanza:

Huwashibisha raia.



Tukaishi vijijini



Vijiji twavikimbia, sana mbali vimekaa,

Hakuna kwenda kukaa, sikuzote kutembea,

Kwalo ninalishangaa, vipi vitaendelea ?

Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !



Kila mtu kaamua, mjini kukimbilia,

Serikali na jamaa, yao moja limekuwa,

Sasa watu waingia, na jioni kuambaa ?

Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !



Kila nikiangalia, hduuma nazigundua,

Sana zimeshafulia, na kisha kuchafuliwa,

Hali yadharauoiwa, kukaa wanakataa,

Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !



Maji safi nahofia, kwingi yameshapotea,

Bomba zimeshachakaa, ardhini yakimbilia,

Palipo nalo jipya, kuti kavu wakalia,

Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !



Umeme wahadithiwa, lini kuja kuingia,

Mahala ukitokea, watu washerekea,

Miaka ingelikuwa, tayari unatolewa ?

Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !



Huduma za kutitia, kwa elimu na afya,

Kiwango chini watoa, mizania yakataa,

Kila ukifikira,kizazi kinaonewa,

Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !



Sasa nimeshaamua, kijijini kwelekea,

Na karibu naitoa, kwa wanaofatilia,

Naenda kusaidia, viwango kuvinyanyua,

Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !



Pwani naenda anzia, vijiji kuzungumzia,

Hoja nimejipangiwa, udhaifu naujua,

Kama wakinisikia, pamoja kuendelea,

Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !



Naitaka jumuiya, ya kwake kuangalia,

Akili kuzitanzua, tuanzapo kupajua,

Na kisha kuvichambua, vifaavyo kujifanzia,

Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !



Maji la kwanza likawa, kijijini kuingia,

Kisha nyumba kuandaa, mkakati wa kuzua,

Kufumba na kufumbua, kijiji kipate ng'aa!

Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !



Huduma zikafatia, ili kilimo kukua,

Usafiri kuutia, urahisi kuridhia,

Kisha tukaangalia, wengine kuwavutia,

Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !



Utalii kutumia, kipato kuongezea,

Huku ninajisomea, na vitendo kuvizua,

Naikataa nadharia, feli nimeziamua,

Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !



Mola ninamlilia, ndoto zangu kuridhia,

Kusoma huku kukawa, kunaleta manufaa,

Jamii ikichanua, na moyo wangu kuchanua,

Tukaishi vijijini, kuyaleta mapinduzi !







MIZIZI JABALINI

MBEGU wamezitupia, katika mawe kuota,


Miye nimeangalia, na ugumba kuusuta,

Kama vile ni ruia, bado ningali naota,

Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !



Yao walikimbilia, na wakanipita puta,

Nyuma hawakuangalia, ya mbele wakiyafata,

Chini hawakuangalia, niendapo waokota,

Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !



Wafata historia, inayozidi wasuta,

Yamebakia mazoea, umeanguka ukuta,

Nao wanaegemea, huku wangali watweta,

Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !



Mambo wameyapangua, wabaki cheza karata,

Kesho inawachachia, wanatifua matuta,

Vyanzo wanakovijua, sasa ufuta wateta,

Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !



Hali ninaihofia, inanukia matata,

Mwanzo itapaanzia, kuongezeka ukata,

Watu wakajinunua, acha wa kununuliwa,

Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !



Mbata wataziangua, na miembe kupukuta,

Na mbichi zilizokuwa, moto ziende kuota,

Hali ikishafikia, watalitwanga pepeta,

Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !



Mizizi mkitifua, mtake tena kuota,

Ardhi huikataa, vya chini vikatokota,

Chinichini kutambaa, juu yashindwe kupita,

Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !



Mkikota mimea, na watu kuwaokota,

Lipi la kujipandia, hadi hadhi kuipata,

Miaka itaamua, yaishe ya kumetameta,

Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !



Mti hauwezi kua, wala tunda kulipata,

Mizizi ikijifia, huwa vigumu kuota,

Taratibu hujifia,ikabakia kutweta,

Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !



Mliyoyakimbilia, ikawa sasa kunyata,

Na kilichowazuzua, kikabakia kiota,

Mahame yakabakia, na njia zilizotota,

Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !

NAULIZA TANZANIA ?



Swali najiandikia, na sitaki kujibiwa,

Niacheni kuzubaa, na kisha nikapumbaa,

Ni ligumu ninajua, sio mnavyofikiria,

Itajengwa Tanzania, na wanaonunuliwa ?



Wenyewe wameridhia, na makofi kupigiwa,

Kuuza na kunnua, ni halali imekuwa,

Nini unatarajia, kwa tunakoelekea ?

Itajengwa Tanzania, na wanaonunuliwa ?



Bidhaa tumeshakua, nani wa kulikataa,

Wakubwa wameamua, biashara kuingia,

Wao wajifagilia, wengine ubaya kuwa,

Itajengwa Tanzania, na wanaonunuliwa ?



Rushwa imetunukiwa, nani wa kuikimbia,

Chama kimenakshiwa, rangi zake kuzivaa,

Ukitaka kung'amua, tafsiri kuijua,

Itajengwa Tanzania, na wanaonunuliwa ?



Wahaka umenijaa, anzali nimeshakuwa,

Kila nikifikiria, nashindwa kujitambua,

Watu niliowadhania, wamegeuzwa bidhaa ?

Itajengwa nchi hii, na wanaonunuliwa ?



Yangu hayana maana




Mimi daima mtwana, wala sijawa ni bwana,

Huo nilishaukana, kuritadi sina dhana,

Hunena ya kufanana, viumbe yakalingana,

Yangu hayana maana, ya kwao ndio yafaa !



Huwaachia mabwana, propaganda kuchuna,

Roho zao za ujana, bado zajaa hiana,

Wamkana maulana, utukufu kuuvuna,

Yangu hayana maana, ya kwao ndio yafaa !



Kwa yao ninapingana, uongo unaposana,

Kweli wakaitafuna, si ya leo siyo ya jana,

Ikawa yalia jana, kabla kila adhana,

Yangu hayana maana, ya kwao ndio yafaa !



Ikawalani amana, na kuiteza dhamana,

Yawarudi na wana, pasiwe na uungwana,

Mengine kutabanana, kwa usiku na mchana,

Yangu hayana maana, ya kwao ndio yafaa !





Chema utakitambua




Hauachi kukijua, wema kilichojaliwa,

Ishara utazijua, ukianza na tabia,

Huziangalia hatua, kila anapotembea,

Chema utakitambua, kwa imani na tabia !



Mkamilifu radhia, kwa hulka na tabia,

Na moyoni ana hawa, wanyonge kusaidia,

Kujikweza hukataa, chini hutaka bakia,

Chema utakitambua, kwa imani na tabia !



Si wa kujitangazia, wala wa kujisifia,

Utumwa kauridhia, watu kuwatumikia,

Suti atazikimbia, na kanzu kujivalia,

Chema utakitambua, kwa imani na tabia !



Hariri hatochagua, ila pamba hutumia,

Daladala kupakia, gari akalikimbia,

Watu huwaangalia, si mali kukimbilia,

Chema utakitambua, kwa imani na tabia !



Anaijua dunia, kioo cha kutambia,

Kuvunjika yake njia, na vingine haijawa,

Yenyewe yabakia, watu hawatabakia,

Chema utakitambua, kwa imani na tabia !



Huishi akitambua, maisha kutumikia,

Kama watumikiwa, utumwa unaingia,

Mwenyewe atayavaa, na kisha akajivua,

Chema utakitambua, kwa imani na tabia !



Daima hujichekea, pasina kumtambua,

Tabasamu lake poa, vigumu kujionea,

Na anachokichekea, mwenyewe anakijua,

Chema utakitambua, kwa imani na tabia !



Dunia aishangaa, upepo kukimbilia,

Akili wanaopewa, wanashindwa jitambua,

Huko huko kuishia, hadi mvi kupaua,

Chema utakitambua, kwa imani na tabia !



Utani ajionea, jinsi tulivyoumbiwa,

Hakuna cha kubakia, majivu tu yabakia,

Kisha hujiangalia, akacheka na kulia,

Chema utakitambua, kwa imani na tabia !





Yako yaweje aghali


Raia ukiachia, ovyo ya kwao yakawa,

Yako ukaangalia, ya ndugu nao jamaa,

Ninashindwa kutambua, vipi bora utakuwa,

Yako yaweje ni ghali, ya kwetu kama rahisi ?



Rahisi yao yakiwa, hivi ghali yako kuwa,

Dharau ukiitia, utakuwa mheshimiwa,

Fakiri wakijikwaa, ukwasi utafurahia,

Yako yaweje ni ghali, ya kwetu kama rahisi ?



Bado najiulizia, na jibu sijapatiwa,

Juu anayeingia, zaidi ataendelea,

Au hapo kafikia, mwisho palipoishakuwa,

Yako yaweje ni ghali, ya kwetu kama rahisi ?



Leo mnaowaabudu


KAENI mkitambua, ukweli utabakia,

Nasi tuliwaambia, hamkutaka sikia,

Miungu mnaozaa, watakuja waumbua,

Leo mnaowaabudu, watakuja kuwakana !



Sauti naisikia, ya saba inatokea,

Kukana mlilozua, kuwa yeye amezaa,

Uchuro aukataa, na wala hakuzaliwa,

Leo mnaowaabudu, watakuja kuwakana !



Warumi wawahadaa, yak wao kuyafatia,

Miungu wengi tabia, ndio wao walozua,

Wapenda kuwashindilia, kikapuni wakakaa,

Leo mnaowaabudu, watakuja kuwakana !



Kunaye wao wa mvua. na kisha kuna wa jua,

Huba naye kajaliwa, ana wake kawekewa,

Na wa mavuno hupewa, sadaka akaachiwa,

Leo mnaowaabudu, watakuja kuwakana !



Mola asikitikia, wasomi wasiosomea,

Hata kitu kukijua, na yakini kuitia,

Kama wana mnakuwa, uzushi ukawafaa ?

Leo mnaowaabudu, watakuja kuwakana !



Mola awahurumia, vitabu msiojua,

Moja mkajishikia, hakika lisilokuwa,

Kama vipofu kupewa, nafasi tembo kumjua,

Leo mnaowaabudu, watakuja kuwakana !



Yupo aliyeringia, tembo ni kama sinia,

Na mwingine kaingia, ujuzi ajivunia,

Kama shina anakuwa, tembo ninayemjua,

Leo mnaowaabudu, watakuja kuwakana !



Wote walijipatia, sehmu waliyoachiwa,

Zaidi hawakujua, kwingine kuyagundua,

Na Alamu muelewa, ndivyo anatufanzia,

Leo mnaowaabudu, watakuja kuwakana !









Kumbe si hivyo wajinga



SIO watu wa kupinga, maguvu wakatumia,

Hawa watu wa kupanga, akili wakatumiya,

Kufungua na kufunga, hii ni yao tabia,

Wapole Watanzania, si kumbe hivyo wajinga !



Sio watu wa kuringa, wangalia hatua,

Sura sio za kuchonga, asili waichukua,

Hapa wameweka nanga, nani wa kuwaondoa ?

Wapole Watanzania, si kumbe hivyo wajinga !



Hawa watu wa kulenga, lengo wakakadiria,

Shabaha wakiinyonga, palepale kwenda kuwa,

Upinde hautapinga, tunduni kwenda ingia,

Wapole Watanzania, si kumbe hivyo wajinga !



Hawa waut wa kusonga, wajua kujipikia,

Ya kwao kutabananga, bila ngao wala gia,

Hawauhofu ukunga, mkubwa akiachia !

Wapole Watanzania, si kumbe hivyo wajinga !



Hawa watu wa kukonga, nyoyo ukawaridhia,

Maguvu ukiyapunga, mwenyewe hukurudia,

Nani wa kutangatanga, na nyumbani akujua,

Wapole Watanzania, si kumbe hivyo wajinga !



Katika ardhi na anga, asili tunaijua,

Visiwa hivi vyalonga, dini vilishaipewa,

Wageni wakitusonga, yetu hatutawaachia,

Wapole Watanzania, si kumbe hivyo wajinga !



Wanaotumwa ukunga, ukafiri kuuzaa,

Ndhimi zao wangechunga, na miili kuaangalia,

Wachamungu wanatanga, na Mola wamlilia,

Wapole Watanzania, si kumbe hivyo wajinga !



Imani hii kupinga, kiini wakichezea,

Huo mkubwa ushonga, hauwezi kubaliwa,

Ya kwenu kutangatanga, hayawezi chini tua,

Wapole Watanzania, si kumbe hivyo wajinga !



Kamba msipojiunga, wazi mkaiachia,

Wenyewe mnajinyonga, ni bora kujiondoa,

Twataka nchi kujenga, Mungu akafurahia,

Wapole Watanzania, si kumbe hivyo wajinga !

Taifa bovu



Watu wakinunuliwa, kuviwakilisha vyama,

Huwa mkubwa ukiwa, wa kukubali utumwa,

Kwani anayenunua, naye amenunuliwa,

Uwakilishi mbovu, huzaa taifa bovu!



IKiwatawala njaa, hamtojali uzima,

Chochote mtachukua, tumbo lipate heshima,

Ila utu hujivua, ukabakia mnyama,

Uwakilishi mbovu, huzaa taifa bovu!



Yote tumeyasikia, na wengine kutazama,

Watu wanawazomea, ukweli wanaosema,

Huko tunakoeleka, kuna ufu si uzima,

Uwakilishi mbovu, huzaa taifa bovu!



Taifa limeshapotea, hakuna wa kulitazama,

Wakubwa waliokuwa, nao kimya wanyamaa,

Nami ninajiulizia, kama wana nia njema ?

Uwakilishi mbovu, huzaa taifa bovu!



Vijana nawahofia, meli yao kwenda zama,

Hawa walionunuliwa, watawaacha salama,

Au nyie mwamjua, ni nini yake azma ?

Uwakilishi mbovu, huzaa taifa bovu!



Uwakilishi wa njaa, kazi yake ni kuzoma,

Akili unaishiwa, ukabaki kuzizima,

Twendako hawajajua, ni lipi tutalokwama,

Uwakilishi mbovu, huzaa taifa bovu!



Siasa wanadhania, ni sherehe kurindima,

Mapambo ya kuzingua, na rangi za kuparama,

Bila watu kuwalea, nchi hii itazama,

Uwakilishi mbovu, huzaa taifa bovu!



Wengine wanunuliwa, ya pombe kuyaegema,

Kauli za kupakua, ila kupika hukwama,

Nyuso wakazinyanyua, zisizofaa tazamwa,

Uwakilishi mbovu, huzaa taifa bovu!



Tambara hujiachia, halifai kulifuma,

Kelel zikizagaa, wapi uone hekima,

Vigezo visipotakiwa, wengine sio wazima,

Uwakilishi mbovu, huzaa taifa bovu!



Shangwe zikiendelea, taifa huwa kilema,

Mkongojo kuutwaa, ya heri kurudi nyuma,

Mbele ninayohofia, iliyojaa tuhuma,

Uwakilishi mbovu, huzaa taifa bovu!



Baraka zitapotea, na kukongoka rehema,

Watu wakadhulumiwa, ikapotea huruma,

Haki tukachuuziwa, na siasa za kichama,

Uwakilishi mbovu, huzaa taifa bovu!



Nyumba tunaibomoa, tena haina salama,

Macho ninayafumbua, kuzingojea zahama,

Nahofu kushtukia, nikakiona kiyama,

Uwakilishi mbovu, huzaa taifa bovu!





Sherehe zingine baa


Hali usipoangalia, mwenyewe ukajifaa,

Waweza kushangilia, ujikute wazomewa !

Na hasa palipo njaa, uhitaji na ukiwa,

Sherehe zingine baa, zinajenga kuchukiwa !



Hali ukiangalia. busara zinatakiwa,

Sahihi kuliamua, kwa wakati kutambua,

Mengine ukiyazua, lawama wajitakia,

Sherehe zingine baa, zinajenga kuchukiwa !



Hata uwezo ukiwa, watakiwa achilia,

Shida ukairidhia, kwa mithili kuitia,

Mnyonge kutougua, na laana kufyatua,

Sherehe zingine baa, zinajenga kuchukiwa !



Jirani hawezi fiwa, wewe ukashereheka,

Mchawi hukudhania, kama hilo hujajua,

Hekima ukijaliwa, mapema huligundua,

Sherehe zingine baa, zinajenga kuchukiwa !

Wanaokula vya wezi



Swali nimelisikia, mjini lauliziwa,

Wezi wakishakwapua, mfukoni kuvitia,

Kisha wakakugawia, na wewe ukatumia,

Wanaokula vya wezi, hivi wao wezi pia ?



Japo wewe ulipewa, kwa nguvu hukuchukua,

Ni haramu yabakia, budi hilo kutambua,

Dhahiri ikishakuwa, kundini namo hutiwa,

Wanaokula vya wezi, hivi wao wezi pia ?



Halali haitakuwa, hicho ulichochukua,

Ni haramu hubakia, vingine haitakuwa,

Na madhambi wagawiwa, kama hilo hukujua,



Mama yahadhithiwa, vya mwana akipokea,

Wala hakuulizia, kule vinakotokewa,

Yeye akatamkiwa, mwana akamsifia,

Wanaokula vya wezi, hivi wao wezi pia ?



Akadai kwongezewa, utamu ulivyokolea,

Kasri akavamia, mwana vingi kuvitwaa,

Sultani kagundua, ndani mwana akatiwa,

Wanaokula vya wezi, hivi wao wezi pia ?



Hukumu haikuchelewa, kunyongwa kahukumiwa,

Mwana machozi kalia, mamaye kutokumlea,

Fursa alipopewa, kaomba mama kwitiwa,

Wanaokula vya wezi, hivi wao wezi pia ?



Mama alipoitiwa, kamwita kusogea,

Mama alipojongea, na sikio kumpatia,

Mwana akaliratua, kisiki kikabakia,

Wanaokula vya wezi, hivi wao wezi pia ?



Sababu aliyoitoa, ni mama kumuachia,

Wizi akaendelea, na vinono kufurahia,

Uchungu kamgawia, katika hii dunia,

Wanaokula vya wezi, hivi wao wezi pia ?

Halali na haramu



YA halali na haramu, viumbe mmeumbiwa,

Mkapewa na fahamu, tofauti kuijua,

Kafiri na Islamu, wote hili walijua,

Mwatakiwa kuyajua, ya halali na haramu !



Kukumbusha yangu zamu, wote mnaofatia,

Nisiwe wa kudhulumu, kuwa hili sikwambia,

Nalijua, situhumu, ukweli nauridhia,

Mwatakiwa kuyajua, ya halali na haramu !



Kumbukeni Jahanamu, muweze kuikimbia,

Mkijitia muhimu, na hili kutohofia,

Maisha ni madhulumu, huruma hayajapewa,

Mwatakiwa kuyajua, ya halali na haramu !



Yakuuliza kalamu, miaka ulivyotumia,

Kama una elimu, hesabu utadaiwa,

Na ujana wa hanjamu, kizaazaa huzua,

Mwatakiwa kuyajua, ya halali na haramu !



Mali ukitakadamu, nayo itauliziwa,

Na cheo ukikihimu, kuna deni wadaiwa,

Mchungi huna utamu, hadi hesabu kuijua,

Mwatakiwa kuyajua, ya halali na haramu !



Niepushe na haramu, halali kunijalia,

Nakuomba Mukadamu, dua yangu kusikia,

Sijaliwi ufahamu, ila unaonijalia,

Mwatakiwa kuyajua, ya halali na haramu !

Binadamu sio hai



Watu wasiofikiri, kazi yao kuitika,

Kwa muda huwa mazuri, yao yanapofanyika,

Ili wakati hutua, mambo yakaharibika,

Binadamu sio hai, fikra zinapozikwa!



Ukiuua kufikiri, na wewe unajiua,

Huo sio umahiri, hakika ni kulemaa,

Hulikimbia la heri, shari ukaivamia,

Binadamu sio hai, fikra zinapozikwa!



Watu watayakariri, yale ya kushangilia,

Wasiwe na itihari, misingi kuitambua,

Hujichimbia kaburi, huku waangalia,

Binadamu sio hai, fikra zinapozikwa!



Baharini husafiri, bila kinga kuchukua,

Wao wakatafsiri, chama kilishaamua,

Na papa wawasubiri, mrama wakiingia,

Binadamu sio hai, fikra zinapozikwa!



ASIYETAKA K UKOSOLEWA



Nimeioina tabia, makosa wayakimbia,

Rushwa waliochukua, wakataa kuambiwa,

Kazi yao kuzomea, tumbo wakashtakia,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Hii ndiyo Tanzania, inakotawalal njaa,

Tumbo linanunuliwa, na akili kuzitoa,

Moyo wakautumia, haramu kuvichagua,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Kilio anayelia, kiungo ameungiwa,

Sura ukiangalia, watu utawadhania,

Nyuma ukichungulia, mkia unatokea,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Watu changa wawatia, machoni limeingia,

Hao hao walokuwa, tofauti wajitia,

Kuna wanalokusudia, na Mola analijua,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Akili mkifungua, siri mtaigundua,

Si wengine walokuwa, haohao mwawajua,

Roho wamezifulia, kulemaza Tanzania,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Nayo mkiyaachia, vijana kuangamia,

Zuri hamtoambua, balaa inawajia,

Hakika mkichelewa, ng'ombe wayo mwawauziwa,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Ng'ombe wayo mwauziwa, katu nchi haitakuwa,

Miti ikendazolewa, mkaa ukabakia,

Vito mkahujumiwa, na mashimo kubakia,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Kitu hamtajaliwa, bali dhiki na udhia,

Heri itawakimbia, shari kuwaingilia,

Akili msipotumia, wenyewe mtaumia,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Wachunguzi wanambia, mzungu wanaujua,

Nyumba imeshachafuliwa, na mto unatakiwa,

Maji yake kuingia, makazi safi yakawa,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Kazi kubwa itakuwa, mwaweza kuikimbia,

Ila isipozingatiwa, makubwa yatatokea,

Mkisimama radhia, dosari mtafagia,

Asotaka kosolewa, hivi huyo mtu mzima ?



Tusingoje ya U.S.S.R.


U.S.S.R. jua, ilishaaga dunia,

Jambo hili latwambia, kitu tusichotambua,

Vigumu kufikiria, na gumu kuaminia,

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Ni vipande imekua, hadithi twazisikia,

Waloleta ujamaa, walipojipendelea,

Ukweli ulipotua, wakaonwa ni wabaya,

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Sasa stani zajaa,na kina Bylorussia,

Wapo kina Georgia, watu kunakozingua,

Pia nayo Chechnyia, watu wanayohofia,

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Palikuwa na Rhodesia, hivi leo twasikia,

Zimbabwe na Zambia, ndizo hizo zilikuwa,

Kumbe nchi hujifia, kiyamache kikingia ?

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Ndivyo ilivyo dunia, yake inavyomboa,

Na asiyejitambua, hutaka kung'ang'ania,

Shauri asiposikia, haachi kujiumbua,

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !

Si mbaya ujamaa, bali watu wa dunia,

Ujanja wakiutmia, matope hukupakaa,

Kizuri kilichokuwa, kuonekana kibaya,

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Nchi zinakufa pia, ukitawala udhia,

Ngapi umezisikia, zimeiacha dunia,

Kumbuka Babylonia, zama ikihadithiwa,

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Kunayo Mesopotamia, ilitawala dunia,

Uyunani nayo pia, wote tulishaelezewa,

Makuu waliyazua, mashine pasi gundua,

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Misri twahadithia, ya zama ilivyokuwa,

Leo taka imekua, watu waona kinyaa,

Farao hajatokea, nchi kuja inyanyua,

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Palikuwa na Persia, michezo twaisikia,

Mabinti waliong'aa, hadi wakapiganiwa,

Watu roho wakatoa, ili kwenda zawadiwa,

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Palikuwa na himaya, Afrika twazijua,

Wachamungu kuwazua, kama Mali nasikia,

Hivi leo nayojua, si kitu ila balaa,

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Marikani kulikuwa, na kubwa pia himaya,

Wahindi wakupakawa, huko walizinyanyua,

Dhahabu wakatumia, nyumba zao kujengea,

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Tanganyika tuliua, mochwari hatukutoa,

Nimekwenda angalia, naona inapumua,

Na sauti kusikia, 'nawe utanipigania? '

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Naam, nikaitikia, bila ya kujitambua,

Labda nilihofia, maiti kuangalia,

Au baridi kukoa, kitu sikukitambua,

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Kungi wanihadithia, mapenzi yanavyokuwa,

Mwana ukishamridhia, kambaye ni kumuachia,

Hunenda akatembea, au mbali kwenda kaa,

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Ila kwawe kumuachia, huru atajisikia,

Ngamani atarejea, hema akalichimbia,

Na penzi juu likawa, hatolishusha radhia,

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Kama ukimshikilia, na wivu tele kujaa,

Huyo atakukimbia, na wala hatarejea,

Ndivyo ilivyo dunia, mamboye ni kuyaachia,

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Hili nilipogundua, mwepesi wa kuatia,

Usumaku nakataa, sitaki kung'ang'aniwa,

Biriani napindua, na kisha kuuachia,

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Rangize kujitanua, chembe mojamoja kuwa,

Siniani kitulia, siriye hutoijua,

Sikio ukifungua, hunong'onezwa na jua,

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Mrima na Zanzibar, nadhani mwanisikia,

Uziwi sijaujua, hiyo nyingine balaa,

Naomba kutojaliwa, ili sote kujaliwa,

Hata nchi hufa pia, ukitawala udhia !



Wednesday, November 14, 2012

Sura za televisheni -2


IMEKUWA yumkini,sasa kwao ofisini,

Wanayagawa mapeni, kucha wajae kiooni,

Msipowakosa machoni, watabakia moyoni,

Sura za televisheni, wananchi ziogopeni !



Hatuwaoni shambani, hiyo kazi ya maskini,

Ni watu wa vijijini, kuteseka maishani,

Hiyo ndiyo yao shani, hawawezi ya mjini,

Sura za televisheni, nyuma zina uzaini !



Chini hawana thamani, ameamua manani,

Wao watafanya nini, kuwapandisha uzani ?

Na sura zao si shani, kwonyesha televisheni,

Sura za televisheni, uongo sera yamini !



Huwaoni machungani, ila ni televisheni,

Kishake magazetini, wakkitoa auni,

Wenye njaa wathamini, walioficha bilioni,

Sura za matangazoni, huwa zanunua nini !



Hawaendi baharini, huko sawa machakani,

Tena ni mashenzini, miji ya Uswahilini,

Riziki ya mtihani, kwa wenye elimu duni,

Sura za machapishoni, zinauza kitu gani !



Habari ni yao nuni, haifai masikini,

Mkakati wao kuni, na moshi mkali machoni,

Maisha ya vijijini, nani anayathamini ?

Sura za televisheni, zingine za mumiani !



Zinawekwa mafichoni, hatuoni uwanjani,

Mkitia hesabuni, jibu lake katoeni,

Wa shule sio chuoni, ubishi wako wa nini ?

Sura za taarifani, zinamlaghai nani !



Umma msiziamini, wanadhamini utani,

Kiilo kwao huwa tani, waseme wamewapeni,

Huwa wauza hisani, na haitoki rohoni,

Sera zza televisheni, umma msiziamini !



Kiini mtathmini, vilivyopo gazetini,

Kuna mengine dukani, yatangaza udhamini,

Yanunuliwa kwa tini, hayajali bwana gani,

Sera za magazetini, kiini mtathmini!



Wakwaza utamaduni, kuthamini vya kigeni,

Na nchi iko shakani, kizazi wanakihini,

Tutavizaa vigeni, visikalike nchini,

Sura za utamaduni, hivi huwa ni wa nani !



Yakini ichungueni, wasemayo mkutanoni,

Mengi yao ya kihuni, si fursa kuwapeni,

Matatizo wachiani, aje amalize nani ?

Sura za mtandaoni, yakini angalieni !



Kuna wengine shetani, hata pia mumiani,

Vampaya waitwani, 'dracula' adhamini,

Wanafurika nchini, wa nje pia wa ndani,

Sura zitakazo shani, anazipenda shetani !



Hubadilika gizani, wakayeyuka nuruni,

Huishi majenezani, hadi usiku wa manani,

Mbalamwezi huadhini, ya kwao misikitini,

Sura za mikutanoni, maswala ziulizeni !



Hupigania yamini, uzazi wake amani,

Hali hawana moyoni, ila wanayoyatamani,

Huachia usukani, kwa kutazama pembeni,

Sura za mahekaluni, kazipimeni amani!



Bidhaa kazijueni, ladha zichanganyeni,

Wajiuza watu gani, na mnunua ni nani ?

Kisha na huko sokoni, hivi kabakia nani?

Sura za maguioni, bidhaa kazijueni !



Wachungani chungueni, walozika ardhini,

Au kilicho hewani, kinachopaa angani,

Usijekuta motoni, ni papa hapa duniani,

Sura zenye mitihani, chungueni umakini !



Salama mtathmini, na kama mwayaamini,

Kuna wazushi nchini, waiweka mfukoni,

Kama h auna mapeni, vigumu kuiauni,

Sura za usalamani, salama katathminini !



Pitieni vitabuni, sura za mahesabuni,

Udhinbiti watiani, ukaleta afueni,

Au wote wamo kundini, aliwaye masikini ?

Sura za mahesabuni, udhibiti kafanzeni



Sikillizeni uani, yaimbwayo akilini,

Nani shida atamani, kama sio afkani,

Na wetu umajinuni, vipi watusaidiani ?

Sura humu vikaoni, sikizeni akilini !



Wajazanapo vitini, waila hesabu gani,

Na nafuu yao nini, walio madarakani,

Au twatumia tani, tukavuna nusu tani ?

Sura za utumishini, kutumwa kayaoneni !



Nimefika tamatini, kwangu hapo ni mwishoni,

Kuzidi sijatamani, nikabakia juani,

Mbegu nawaachieni, mtakako kapandeni,

Sura za taasinini, ukweli kaubaini !



Sura za televisheni -2


IMEKUWA yumkini,sasa kwao ofisini,

Wanayagawa mapeni, kucha wajae kiooni,

Msipowakosa machoni, watabakia moyoni,

Sura za televisheni, wananchi ziogopeni !



Hatuwaoni shambani, hiyo kazi ya maskini,

Ni watu wa vijijini, kuteseka maishani,

Hiyo ndiyo yao shani, hawawezi ya mjini,

Sura za televisheni, nyuma zina uzaini !



Chini hawana thamani, ameamua manani,

Wao watafanya nini, kuwapandisha uzani ?

Na sura zao si shani, kwonyesha televisheni,

Sura za televisheni, uongo sera yamini !



Huwaoni machungani, ila ni televisheni,

Kishake magazetini, wakkitoa auni,

Wenye njaa wathamini, walioficha bilioni,

Sura za matangazoni, huwa zanunua nini !



Hawaendi baharini, huko sawa machakani,

Tena ni mashenzini, miji ya Uswahilini,

Riziki ya mtihani, kwa wenye elimu duni,

Sura za machapishoni, zinauza kitu gani !



Habari ni yao nuni, haifai masikini,

Mkakati wao kuni, na moshi mkali machoni,

Maisha ya vijijini, nani anayathamini ?

Sura za televisheni, zingine za mumiani !



Zinawekwa mafichoni, hatuoni uwanjani,

Mkitia hesabuni, jibu lake katoeni,

Wa shule sio chuoni, ubishi wako wa nini ?

Sura za taarifani, zinamlaghai nani !



Umma msiziamini, wanadhamini utani,

Kiilo kwao huwa tani, waseme wamewapeni,

Huwa wauza hisani, na haitoki rohoni,

Sera zza televisheni, umma msiziamini !



Kiini mtathmini, vilivyopo gazetini,

Kuna mengine dukani, yatangaza udhamini,

Yanunuliwa kwa tini, hayajali bwana gani,

Sera za magazetini, kiini mtathmini!



Wakwaza utamaduni, kuthamini vya kigeni,

Na nchi iko shakani, kizazi wanakihini,

Tutavizaa vigeni, visikalike nchini,

Sura za utamaduni, hivi huwa ni wa nani !



Yakini ichungueni, wasemayo mkutanoni,

Mengi yao ya kihuni, si fursa kuwapeni,

Matatizo wachiani, aje amalize nani ?

Sura za mtandaoni, yakini angalieni !



Kuna wengine shetani, hata pia mumiani,

Vampaya waitwani, 'dracula' adhamini,

Wanafurika nchini, wa nje pia wa ndani,

Sura zitakazo shani, anazipenda shetani !



Hubadilika gizani, wakayeyuka nuruni,

Huishi majenezani, hadi usiku wa manani,

Mbalamwezi huadhini, ya kwao misikitini,

Sura za mikutanoni, maswala ziulizeni !



Hupigania yamini, uzazi wake amani,

Hali hawana moyoni, ila wanayoyatamani,

Huachia usukani, kwa kutazama pembeni,

Sura za mahekaluni, kazipimeni amani!



Bidhaa kazijueni, ladha zichanganyeni,

Wajiuza watu gani, na mnunua ni nani ?

Kisha na huko sokoni, hivi kabakia nani?

Sura za maguioni, bidhaa kazijueni !



Wachungani chungueni, walozika ardhini,

Au kilicho hewani, kinachopaa angani,

Usijekuta motoni, ni papa hapa duniani,

Sura zenye mitihani, chungueni umakini !



Salama mtathmini, na kama mwayaamini,

Kuna wazushi nchini, waiweka mfukoni,

Kama h auna mapeni, vigumu kuiauni,

Sura za usalamani, salama katathminini !



Pitieni vitabuni, sura za mahesabuni,

Udhinbiti watiani, ukaleta afueni,

Au wote wamo kundini, aliwaye masikini ?

Sura za mahesabuni, udhibiti kafanzeni



Sikillizeni uani, yaimbwayo akilini,

Nani shida atamani, kama sio afkani,

Na wetu umajinuni, vipi watusaidiani ?

Sura humu vikaoni, sikizeni akilini !



Wajazanapo vitini, waila hesabu gani,

Na nafuu yao nini, walio madarakani,

Au twatumia tani, tukavuna nusu tani ?

Sura za utumishini, kutumwa kayaoneni !



Nimefika tamatini, kwangu hapo ni mwishoni,

Kuzidi sijatamani, nikabakia juani,

Mbegu nawaachieni, mtakako kapandeni,

Sura za taasinini, ukweli kaubaini !



Wote adawa wakiwa


Wote adawa wakiwa, rafiki awe ni nani ?

Hivi unafikiria, au sasa hayawani ?

Kuua na kuuliwa, iwe ndio yako shani ?

Wote adawa wakiwa, utachukia dunia !



Unaweza kupagawa, ukaingia kichaa,

Mafuu ukishakuwa, huna utalotambua,

Utaabiri mitaa, makopo kuyaepua,

Wote adawa wakiwa, utachukia dunia !



Shuruti yakutumia, kama maji ni kupoa,

Kuna njia hufikia, pemeni kujikalia,

Hali ukaichungua, wapi unaelekea,

Wote adawa wakiwa, utachukia dunia !



Ndipo unapogundua, binadamu ni hadaa,

Machoni kajifichia, na moyoni kuitia,

Akaifua na haya, na aibu kuitoa,

Wote adawa wakiwa, utachukia dunia !



Hutaka kukutumia, na wala si kumtumia,

Kila akikusadia, lake anafikiria,

Aweza akalichopoa, haraka kujiondoa,

Wote adawa wakiwa, utachukia dunia !



Mwema nawakubalia, watunzi waliyozua,

Hakika hajazaliwa, ila waovu wajaa,

Hii ni yetu dunia, ndio mambo yake haya,

Wote adawa wakiwa, utachukia dunia !



Waongo hukuzidia, ndiyo juu wakakaa,

Wewe ukawadhania, ndio wanaokufaa,

Kumbe wanakutumia, wende walikokukusudia,

Wote adawa wakiwa, utachukia dunia !



Yako ukenda fulia, hilo halitosumbua,

Ya kwanza kuangalia, ndio ahadi watiya,

Vingine haitakuwa, laiti ungelijua ?

Wote adawa wakiwa, utachukia dunia !









Sera za Watanzania

Nani kalifikiria, na chama kukigawia,

Iweje sera ikawa, chama inazinunua,

Na sote twatarajia,, kwa yake tukajaliwa,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Labda rushwa kutoa, hiyo ya kwao twajua,

Ufukara kuzidia, ndipo hapa tumekaa,

Na upofu kujitia, kitu halijasaidia,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Kwa uziwi kusifiwa, haya tungeishajua,

Ya msingi yamejaa, kufanza tunatakiwa,

Hapo tukishafikia, sera twaweza ibua,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Nani amekuambia, kwenye hii Tanzania,

Kuna watu wakataa, kilimo kutuhudumia,

Na vyama tumevizua, chakula kutotumia ?

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Nani amekuambiwa, kunao Watanzania,

Gizani waazimia, sikuzote watakaa,

Vijinga wakatumia, mwangaza kujipatia,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Na eti wa kuwatoa, budi mchama akawa ?

Kama mtu hujifia, hicho cha kutegemewa ?

Na mumiani kikiwa, ndio hofu kinatia,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Nani amekuambia, chama fedha kimejaa,

Wapi kinajipatia, kama si hazina pia,

Kingi wakakumbatia, kidogo wakaachia,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Serikali kuzifua, lazima inatakiwa,

Leo moja ukavaa, kesho nyingine kutwaa,

Nguo moja kitumia, fukara utadhaniwa,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Serikali ni kuvaa, na kisha ukaivua,

Unapoing'ang'ania, inazidi kuchakaa,

Uzuri haitakuwa, ikianza kufubaa,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Jana kijani kutia, leo bluu watumia,

Rangi nyingi zimejaa, moja tu unachagua,

Kuna zingine balaa, bahati hukukimbia,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Nani amekuambia, njia wanazikimbia,

Wazihofu Tanzania, kuwaletea mabaa,

Maporini wapitia, salama kujisikia?

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Sera ni kama bidhaa, vitu hivyo hutumiwa,

Vitu vinapomfaa, kila mtu hutumia,

Ila kama vya rushuwa, muumini hukataa,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Sera kama vile hewa, kila mtu hupumua,

Mazuri kuyachagua, binadamu ni tabia,

Hawezi akaparamia, baya yeye kuchagua,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Nani amekuambia, elimu haitatufaa,

Hivyo wajinga wang'aa, elimu kuitania,

Na mikopo kuzuia, wenetu kutowafaa?

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Nani amekuambia, ataka lima kinjaa,

Pamba akijivunia, soko kutotengenea,

Akasikiza umbeya, na hadithi kupigiwa ?

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Nani amekuambia, afya ni kitu balaa,

Huduma bure kutoa, watu wengi wahofia,

Ila ujira wa njaa, ukawa wapalilia,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Ila ujira wa njaa, ukawa wapalilia,

Dau wakalizindua, sasa milioni kuwa,

Senti zikishapungua, huondoka wako dia,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Nani amekuambia, eti nyumba twakataa,

Manyata twakumbatia, na porini kutulia,

Mjini twakuhofia, hatutaki kwendelea,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Kama sio yenu nia, fahari kujionea,

Neema kujisikia, nyie mliojaliwa,

Vyote kuwatiririkia, wote mliobarikiwa,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Siri wameigundua, mwahofu kukataliwa,

Binti ukimjengea, aweza nje kukutoa,

Mwingine kukubaliwa, na kitu asiyekuwa,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Kwenu ni Watanzania, wanajua kuchagua,

Nyumba wakijipatia, wengine watachangua,

Uhuru kujipatia,, hamwezikuwaswagia,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Nani amekuambia, wageni ndio wafaa,

Kukopa tukijazia, mabenkini zikajaa,

Ila akiwa mzawa, shuruti anaekewa ?

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Nani amekuambia, hatutakiwi Ulaya,

Pasi mkazizuia, wenyeji kujipatia,

Ila wa Somalia, raia wao wakawa ?

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Nani amekuambia, juujuu ukijua,

Mweledi umeshakua, bila ya kuyachunua,

Ng'ombe wayo huuziwa,mjini ukaingia,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Nani amekuambia, hisa tumeshazikataa,

Ila palipo udhia, utani pia mzaha,

Oksijeni kwishiwa, bado najiulizia ?

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Nani amekuambia, madini yamilikiwa,

Na wachache walokuwa, matofali wakapewa,

Nani anayetumia, ujira akishapewa ?

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Langu ninamalizia, kwa uchama kukataa,

Mengi yanayotakiwa, hayo ya wote yakawa,

Programu kuridhia, nchini kufumuliwa,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



Serikali ya pamoya, akili iliyojaa,

Hiyo nitafurahia, na sio ya kutumiwa,

Uhuru iliyokuwa, yake inayaamua,

Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:

Hasa vya msingi vikiwa !



SIKU HII Tanzania

KIU wengi wazidiwa, maji wanayalilia,


Na wanayoyasikia, miradi wakipangia,

Ila hat alile la dawa, maji hayajaingia,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Waishi Watanzania, hata kando ya maziwa,

Nako ni kizaazaa, maji pia yapotea,

Wengine wayachukua, kwenda kwao kuwafaa,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Maji wengi twafulia, sio kwa kusafishia,

Ila nayo kutokuwa, na uchafu unajaa,

Sasa dhiki imekua, hata ua kunyweshea,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Chakula chazidi paa, bei twashindwa fikia,

Na hali ukiangalia, ukali waendelea,

Itakuja kufikia, mlo kutoambulia,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Shangwe ninazihofia, zisijekuwa kulia,

Matumbo yakiadhiriwa, hifadhi kutopatiwa,

Vijijini wakavia, zaidi kudhulumiwa,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Gizani tunaingia, asubuhi kuamkia,

Na nyimbo tunasikia, tatizo kuliondoa,

Miezi inaishia, hadithi yaendelea,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Mashine wazilipua, katakata kwendelea,

Hakuna wa kufidia, mtenzi azawadiwa,

NI za kichizi sheria, laiti wangezijua,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Kweli wapo wa kung'aa, njia zao wazijua,

Hawa ukijionea, pepo utaidhania,

Ila wengi ninajua, hali leo zawaua

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Siwezi jihurumia, afadhali naijua,

Nyuma sijaangalia, naitafuta afua,

Ninamsihi Jalia, hili kujaniridhia,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Gharama zazidi paa, kwa elimu na afya,

Mikopo yatukimbia, wakubwa kuwafatia,

Kile tunachobakiwa, yabidi kupigania,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Ni huzuni imekuwa, tena mkubwa ukiwa,

Kesho tunaihofia, jinsi itakavyokuwa,

Utabiri nakimbia, mimi siwezi kutoa,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !



Mola ninamuachia, kadari kuiangalia,

Dhiki kutuepushia, toba zetu kisikia,

Nasi tuongeze dua, tupate kuhurumiwa,

Leo hii Tanzania, sio nchi ya furaha !





WAJINGA WAKIAMKA

Walolala wakiamka, usingizi wakatoa,

Bongo zitahamanika, ukungu kuundoa,

Na yasiyoeleweka, yakaanza kuhojiwa,

Wajinga wakiamka, watamjua muongo !



Miaka wataitaka, hadithi kuhadithiwa,

Wengine walikofika, wapi walikoanzia,

Na nyie kilichoshindika, sababu mkaitoa,

Wajinga wakiamka, watamjua mjanja !



Malaysia wasifika, hata nasi twakujua,

Watoto twawapeleka, kwenda huko kusomea,

Mngefanza ya hakika, na sisi tungelikuwa

Wajinga wakiamka, watamjua mmbeya !



Indonesia wawika, vitenge tunanunua,

Na mashati kujivika, bichi tunapotumbua,

Haya hayakueleweka, wala hamkuyapania ?

Wajinga wakiamka, watamjua mnafiki!



Korea wamegawika, wa kwanza tunamjua,

Tulienda na dhihaka, njaa sasa wanalia,

Tukaachia hakika, leo walioendelea,

Wajinga wakiamka, watamjua mkweli !



Uchina tulikotoka, tofauti haikuwa,

Leo wanatuzunguka, mkiani twabamia,

Halafu wanawehuka, ustawi waujua ?

Wajinga wakiamka, watamjua muongo !



Yawapi ya Tanganyika, siku ilipoanzia,

Wakati tulipowika, dunia kutusikia,

Vipanya twatambulika, nani wa kutusikia ?

Wajinga wakiamka, watamjua mjanja !



Maji yanaadimika, hata kuliko maziwa,

Wakaishi kwa mashaka, maji kuyaaangalia,

Hata bomba kuchipuka, kazi kubwa imekuwa?

Wajinga wakiamka, watamjua mmbeya !



Pampu zimeshindika, wenyewe kujiundia,

Maji chini yalofika, nani aweza kutoa ?

Kisha unadanganyika, eti umeendelea ?

Wajinga wakiamka, watamjua mnafiki!



Umeme twaadhirika, kuzima na kuzimua,

Asilimia ya shaka, ndiyo tuliyojipatia,

Kwingine walazimika, gizani kuangalia ?

Wajinga wakiamka, watamjua mkweli !



Vijiji vimeuzika, kuzaa na kufulia,

Yao kwao tumepoka, giza tukawaachia,

Na dharau twaiweka, nani kuvitembelea ?

Wajinga wakiamka, watamjua muongo !



Barabara zaanguka, madaraja kutitia,

Reli zimeshakatika, vipande twajiungia,

Huko China wanawaka, umeme wanatumia ?

Wajinga wakiamka, watamjua mjanja !



Nani huyo alimaka. twaweza kuendelea,

Pasinapo kuuweka, umeme ukatumiwa,

Vijijini kujengeka, na miji ipate kua?

Wajinga wakiamka, watamjua mmbeya !



Mshamba yatalimika, kisegerrema kutumia ?

Majembe mliyonyaka, takataka yamekua,

Kilimo kwanza cha shaka, mbali hakitafikia,

Wajinga wakiamka, watamjua mnafiki!



Cha mwisho kitasifika, tusipoyaangalia,

Maana yaaminika, sipo tulipoanzia,

Kama kweli tengetaka, kuzalisha twatakiwa,

Wajinga wakiamka, watamjua mkweli !



Kama kweli tungetaka, kuzalisha twatakiwa,

Zana zenye uhakika, zikatoka Tanzania,

Mitambo ikajengeka, vifaa kufyatulia,

Wajinga wakiamka, watamjua muongo !



Vya msingi tukiweka, wenyewe twajiundia,

Itakuwa ni hakika. papo hapo twatokea,

Ila tukidanganyika hutajirisha dunia,

Wajinga wakiamka, watamjua mjanja !



Nyumba tunadanyanyika, watu kutowajengea,

Kazi hii ya hakika, haraka inatakiwa,

Kazi ikishamalizika, kujenga nchi inakuwa,

Wajinga wakiamka, watamjua mmbeya !



Madini twahadaika, wengine kuwaachia,

Sheria hatujaweka, wenyewe kujichimbia,

China yangelifanyika, wasingeliendelea,

Wajinga wakiamka, watamjua mnafiki!



Wajinga wakiamka, watataka kuelewa,

Mbona hamkushaurika, watu kwanza kuinua,

Kisha ndio mkazuka, ya kwenu kujifanzia,

Wajinga wakiamka, watamjua mkweli !



Mafisadi watataka, wote wakahesabiwa,

Na huko walikoyaweka, Uswizi tukakujua,

Porojo hawatataka, kwani waliishamua,

Wajinga wakiamka, watamjua mkweli !



Ninakumba Rabaka, kuyaondoa mashaka,

Siki ya watu kunyanyuka, rehema kutozizuia,

Kote zikamiminika, ubaya wema ukawa,

Wajinga wakiamka, watamjua mkweli !



Wote tukasalimika, kwa haki kuzingatia,

Yako yakakamilika, kati yaliyozuia,

Na wote walioponzeka, ya kwao waje fidiwa,

Wajinga wakiamka, watamjua mkweli !