Wednesday, July 18, 2012

Mnyonge ana sauti






WAO ni kama maiti, nani wa kuangalia,

Waliokalia viti, mengine yawasumbua,

Mnyonge hana bahati, kaziye kuhujumiwa,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !



Hukisiwa afriti, mengi akitumumiwa,

Hata ndugu humsaliti, jaha kuikimbilia,

Akaishia makuti, na donge la kukandia,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !



Ya kwake hawayateti, wala kuzungumzia,

Yakitiwa kwenye hati, msaada watakiwa,

Fukara haumkuti, mifukoni huishia,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !



Wala hanayo kamati, yake yakafikiriwa,

Hakuna ya kweli dhati, umaskini kutoa,

Mambo yao hatihati, wenyewe kujipalilia,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !



Fukara haumkuti, mifukoni huishia,

Kwa wenye kuvaa suti, na ghorofa za kofia,

Maskini kibushuti, hana anachoambulia,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !



Mnyonge hana bahati, kaziye kusahauliwa,

Au kama kibiriti, hutumika kuwashia,

Na mezani hakiletwi, mtu kikishamfaa,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !



Ni mtumwa wa vicheti, na vya bure vibarua,

Zoezini humkuti, ila kwenye kuhesabiwa,

Anazo nyingi shuruti, vizuri kutawaliwa,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !



Mwanaye hali biskuti, wala kupewa halua,

Daraja la pili si kati, hilo kaishachaguliwa,

Hata akiwa 'smati', ndipo hapo huishia,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !



Yananiuma magoti, nashindwa kuendelea,

Ila wasia wa dhati, huu nishawaambia,

Mazuri hatuyakuti, mnyonge tumimuonea,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !



Mshairi siwasaliti, nazidi kuwatetea,

Hadi nipate mauti, na wengine kuachia,

Namuomba Muqsiti, daima kuangalia,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !

Z A N Z I B A R, Z A N Z I B A R !!!







Inna lillahi Alaa, waina illahi rajiuuni,

Visiwani tunalia, kwa kukosa tumaini,

Kila siku kufiliwa, kwenye njia baharini,

Zanzibar, Zanzibar, kila siku tunalia !



Ajali tumezoea, sera mpya twazibuni,

Kwa ajizi na udhia, nchi wamesharubuni,

Wenye fedha waachiwa, leseni za mumiani,

Zanzibar, Zanzibar, kila siku tunalia !



Ndugu ninawalilia, inaniuma moyoni,

Pole yao nakataa, naona kama uhuni,

Tunaweza kuzuia, amini usiamini,

Zanzibar, Zanzibar, kila siku tunalia !



Eti meli zatembea, ofisi hatuzioni,

Au ni za Liberia, au kutoka Japani,

Seagull yaelea, wenye mali kina nani?

Zanzibar, Zanzibar, kila siku tunalia !



Mitumba twaitumbua, nayo yatufanyanini?

Ndiyo sera na sheria, kukwaa na kujihini,

Kuna watu wachangia, twamsingizia shetani ?

Zanzibar, Zanzibar, kila siku tunalia !



La bidanamu kavaa, huyo jini mumiani,

Na uhuru amepewa, kuufanya uhaini,

Ndani nje kuchungua, yasifichwe asilani,

Zanzibar, Zanzibar, kila siku tunalia !



Fidia zetu nazaa, zinatushusha thamani,

Ndio ma'na inakuwa, wanakosa umakini,

Kitu kidogo wakiipewa, twaumia masikini,

Zanzibar, Zanzibar, kila siku tunalia !



Jalali twakulilia, kwa adha na usononi,

Ndiye uliyebakia, viumbe wavithamini,

Tulioishawachagua, wametuacha mataani,

Zanzibar, Zanzibar, kila siku tunalia !





Kwenye waongo na wezi








BALAA huzaliana, zikawa kadha wa kadhaa,

Tena zikafuatana, kama kunywesha mvua,

Hutupima Maulana, kuona kama twamjua,

Kwenye waongo na wezi, balaa huzaliana!



Yanawashinda mchana,kutafutia dawa,

Usiku wakachuana, gizani kuulizia,

Ajizi nyumba ya laana, na mkewe ni makiwa,

Kwenye waongo na wezi, balaa huzaliana!



Mitumba wamependana, ya meli watulettea,

Miaka hawajaiona, wala hawataijua,

Kufa kwao kufaana, mifuko huzidi jaa,

Kwenye waongo na wezi, balaa huzaliana!



Mengi sana watanena, tukio likishatukia,

Mipango hutoiona, sembuse zao hatua,

Mambo huwa yalandana, kama zama yatakuwa,

Kwenye waongo na wezi, balaa huzaliana!



Chozi la mamba lanona, uchungu hataujua,

Kina mama nao wana, ndio wanaoumia,

Wakitoweka mabwana, nani kuwaangalia ?

Kwenye waongo na wezi, balaa huzaliana!



Nywele ngumu na kitana, watawala wamekuwa,

Hakika hawatonena, simulizi watatoa,

Na mola washaachana, waabudu ya dunia,

Kwenye waongo na wezi, balaa huzaliana!



Yunusi alishaona, na siri anaijua,

Kwetu hawana maana, wajifanzao wajua,

Ni yanini kubishana, sineme kujionea,

Kwenye waongo na wezi, balaa huzaliana!



Huja yakajaumana, mioyo kuifufua,

Ikaondoka hiyana, na wakweli kujaliwa,

Imani waliyoshona, Muumba kumgeukia,

Kwenye waongo na wezi, balaa huzaliana!



Waache wenye kukana, ya kwao wanayajua,

Leo wana muamana, kesho huwatumbukia,

Nyongo zikawa suna, na faradhi papo pia,

Kwenye waongo na wezi, balaa huzaliana!



Mola wangu Maulana, hifadhi naililia,

Hawa wakwetu mabwana, yangu wameshafulia,

Umebakia utwana, na pekee majaliwa,

Kwenye waongo na wezi, balaa huzaliana!

Wanautaka ukubwa






WASUMBUKAO kwa njaa, ya ukubwa kuukwaa,

Fumbo nimelifumbua, kuongoza hufulia,

Wakawa wang'ang'ania, watu huku waumia,

Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !



Njaa yao kutumbua, vya umma wakajilia,

Wala si kusaidia, na watu kuwanyanyua,

Yao wamedhamia, siye nyie kuwafaa,

Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !



Ukubwa wanadhania, ni nafasi kuchukua,

Kichwani wakawa wang'aa, kwa utupu kuuvaa,

Hawana la kuamua, la wananchi kuwafaa,

Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !



Ni mzigo wanakuwa, mabegani mwa raia,

Badala kuendelea, huwa tunadidimia,

Lakiini watajisifia, eti twapiga hatua,

Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !



Kaitazame Malaysia, au nayo Indonesia,

Udhia utatambua, na dhihaka kuagua,

Kila mwenye kujisifia, kasoro nyingi kajaa,

Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !



Vya msingi twaachia, ugaidi tunalia,

Ya kwetu twayaachia, ya wazungu kuchukua,

Ila si yanayofaa, bali wao kuridhia,

Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !



Juu wanakobakia, ndiko wanaishilia,

Ya chini hawatajua, uongo watagawiwa,

Ajizi kupakuliwa, wakala na kucheua,

Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !



Ujinga unatuua, ya kwetu kutotambua,

Haya yanapotokea, watu tunawaaachia,

Na Mungu kumzulia, ya shetani yalokuwa,

Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !



Shetani achekelea, Mola kumsingizia,

Na namba anatutia, wajihini zikang'aa,

Hakika tutakijua, nachelea, nahofia,

Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !



Tupe nafuu jalia, uongozi wa kufaa,

Hali kuzia.ngalia, na kupungua nazaa,

Tuvute kukurudia, tukakimbia hadaa,

Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !





FIDIA YETU UHUNI




Ndio ma'na wanaua, fidia zetu dhihaka,

Maisha ya Mtanzania, thamani hatujaweka,

Vishilingi twalipia, mpewa akajicheka,

Fidia zetu dhihaka, ndio ma'na tunaaua !



Watazungumza wanaa, na Mola kumzulia,

Ila wa mtu ukiwa, mkono tunaujua,

Muhyi huwasaidia, wanaojisaidia,

Fidia zetu dhihaka, ndio ma'na tunaaua !



Tajiri watutania, ni wa kufa na kuzika,

Thamani waitambua, milioni kutofika,

Vijisenti watambua, hawawezi pepesuka,

Fidia zetu dhihaka, ndio ma'na tunaaua !



Wakubwa wamewatia, mfukoni kuwaweka,

Yao wanayaelewa, wana njaa za kunuka,

Nani wa kuwatishia, thamani kuongezeka ?

Fidia zetu dhihaka, ndio ma'na tunaaua !



Mahakama wazishika, rahisi zitaamua,

Hawawezi filisika, biashara kwendlea,

Wao hawana mashaka, ni Mungu ameamua !

Fidia zetu dhihaka, ndio ma'na tunaaua !



Hawa ni Waafrika, ndiyo yao kugundua,

Ukija umefyatuka, yaweza kukutokea,

Bila kanuni kuweka, na wageni watalia,

Fidia zetu dhihaka, ndio ma'na tunaaua !



Safari zetu mashaka, na ajali majaliwa,

Tajiri hatoteseka, masikini huumia,

Kisha huzuka vizuka, ya uongo wakalia,

Fidia zetu dhihaka, ndio ma'na tunaaua !



Wanga watadaamka, na machozi kuyatoa,

Kumbe wao ndo mahoka, kisa kilichochangia,

Maiti wakasifika. pengo wametuachia,

Fidia zetu dhihaka, ndio ma'na tunaaua !



Pengo likaelezeka, na wasifu kuutoa,

Hawawezi kuzuzuka, kazi wameizoea,

Ya mnyonge patashika, ndiyo aliyojaliwa,

Fidia zetu dhihaka, ndio ma'na tunaaua !