Sunday, January 29, 2012

Mtunzi hana thamani

WENZETU wamejaliwa, nchi kuwaridhia,
Mshairi kwa sanaa, kazi muhimu kupewa,
Na ofisi kuingia, ushairi kuandaa,
Hathaminiwi mtunzi, hapa kwetu Tanzania !

Mtunzi huteuliwa, nafasi akachukua,
Mshairi namba moya, nchi ikamchagua,
Akatunga na kusia, nchi yanayosisimua,
Hathaminiwi mtunzi, hapa kwetu Tanzania !

Taifa humtambua, mashairi kuyalea,
Jamii yakaifaa, kwenye shibe na njaa,
Na watu kuwausia, yote yenye manufaa,
Hathaminiwi mtunzi, hapa kwetu Tanzania !

Uongo huushushua, na kweli kuing'amua,
Watu akawaongoa, na nchi kutengenea,
Amani ikaenea, na umoja kukomaa,
Hathaminiwi mtunzi, hapa kwetu Tanzania !

Mshairi Tanzania, ni kichafu kitambaa,
Kamasi cha kutolea, kuishia kwenye jaa,
Hakuna anayemjua, walal kumsaidia,
Hathaminiwi mtunzi, hapa kwetu Tanzania !

Vyuo vinaugua, kwa homa ya malaria,
Maruerue kujaa, jinamizi kaingia,
Nao watindikiwa, ushairi unavia,
Hathaminiwi mtunzi, hapa kwetu Tanzania !

Vyuo vatindikiwa, ushairi umepwaya,
Washindwa kuitumia, sanaa kufundishia,
Wakawasha mshumaa, na fikra kuzagaa,
Hathaminiwi mtunzi, hapa kwetu Tanzania !

Mengi wakayaibua, tungo na fikra pia,
Mawazo wakachimbua, nchi kujaa kufaa,
Chemchemi ikajaa, hekima kutopotea,
Hathaminiwi mtunzi, hapa kwetu Tanzania !

Vyombo vya habari baa, sanaa yanyanyapaa,
Ila vichache radhia, Radio tunazojua,
Vipindi huviandaa, malenga tukasikia,
Hathaminiwi mtunzi, hapa kwetu Tanzania !

Magazeti nayo pia, ushairi yaonea,
Ukurasa yakataa, tungo kuzikubalia,
Machache hutokea, nafasi inapokuwa,
Hathaminiwi mtunzi, hapa kwetu Tanzania !

Hakuna Mtanzania, wa kuhariri sheria,
Mashairi kuyajua, msasa akayatia,
Yeyote huchaguliwa, kazi hii akapewa,
Hathaminiwi mtunzi, hapa kwetu Tanzania !

Televisheni balaa, sanaa hazijajua,
Muziki washikilia, hata tuchoke sikia,
Sasa ni kama kinyaa, kelele zinavyojaa,
Hathaminiwi mtunzi, hapa kwetu Tanzania !

Watunzi tuombe dua, watu macho kufungua,
Sanaa kuangalia, vizazi ikavifaa,
Isije ikajifia, na hazina kupotea,
Hathaminiwi mtunzi, hapa kwetu Tanzania !


Januari 29, 2012,

Dar es salaam.

Uonevu ukizidi

BASHIRI macho hafungi, na huona kila jambo,
Msije kula mirungi, muone yasiyo tambo,
Ya mja hayamchengi, kwa sauti au wimbo,
Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Kinyonga kwake haringi, ndiye aliyempa umbo,
Humbadili kwa rangi, adawa kukwepa mkumbo,
Na kwa mapozi ni kingi, ashinda hata mgambo,
Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Viumbe walio wengi, ni wadogo kwa maumbo,
Na si watu wa mitungi, wala kwa wingi mapambo,
Hutafuta la msingi, mengine kwao vijambo,
Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Lakini mlangilangi, yao yaendayo kombo,
Hutafuta kama nungwi, yaumizayo matumbo,
Kunao wavuta bangi, wajifanyao ni Rambo,
Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Nao wenye mali nyingi, huwatumia mgambo,
Hawana chao kichungi, haki kuwa mtarimbo,
Watakayo ni shilingi, wengine kula vikumbo,
Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Tamaa hawajivungi, hukaa nawe kitambo,
Hutumia nguvu nyingi, kuzikuza zao tambo,
Hata wenye fungu jingi, huzama kwenye mkumbo,
Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Omwami na kina mangi, wanayaguna mafumbo,
Kadhalika na wasangi, na watani zao Rombo,
Hukiondoa kigungi, hata wakenda Urambo,
Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Mwana muulize Dingi, kama naye ana jambo,
Nawe uwe ni mchungi, kunusuru lako tumbo,
Na ukaushe matangi, kwa dhuluma yake chambo,
Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !


Januari 29, 2012
Dar es Salaam

Wakataa ukewenza, utaitwa mumesina !

Mariamu sikiliza, ushauri nakwambia,
Usijefanya kuiza, ukaja kuyajutia,
Mkataa ukewenza, sinamume hujakua,
Wakataa ukewenza, utaitwa mumesina !

Amri inaeleza, weye unaitania,
Mwenyewe wajimaliza, kesho kujiharibia,
Dini unaipuuza, kwa kukosa zingatia,
Wakataa ukewenza, utaitwa mumesina !

Ndoa hukupa makazi, kwa wazazi unakaa?
Ndoa hukupa malezi, mumeo kukuangalia,
Ndoa hukupa malazzi, libasi ukaijua,
Wakataa ukewenza, utaitwa mumesina !

Ndoa hukupa malazzi, libasi ukaijua,
Mwenzio kuwa pumzi, nawewe ukapumua,
Kitulizo chenye enzi, kila mmoja akawa,
Wakataa ukewenza, utaitwa mumesina !

Mola ukimkabidhi, moyoni yaliyokuwa,
Hakika huyahifadhi, nawewe ukajaliwa,
Akakupa wema wenzi, ndoa mkawa wabia,
Wakataa ukewenza, utaitwa mumesina !

Atakupa wema wenzi, ndoa mkawa wabia,
Mkawa wasaidizi, nyumba kuiangalia,
Mkapewa na uzazi, udugu mkachangia,
Wakataa ukewenza, utaitwa mumesina !

Na yakiwepo maradhi, wote kujihudumia,
Mkazigawa na kazi, na zamu kujipangia,
Pasiwe na kizuizi, kwa feli kuziamua,
Wakataa ukewenza, utaitwa mumesina !

Ni chuo chenye ujuzi, mengi mtakujayajua,
Na pawapo yake radhi, Mola huyaafikia,
Mkaipanda ngazi, wote peponi kwingia,
Wakataa ukewenza, utaitwa mumesina !


Januari 29, 2012
Dar es Salaam

Utukufu si mazazi

Utukufu sio kazi, wala haijawa ngazi,
Haunao mnunuzi, huchuuzwa mchuuzi,
Viumbe wana ajizi, hilo siyo yao hadhi,
Utukufu si mazazi, utukufu ni majazi!

Ukijisifu mkwezi, na sisi kuwa washenzi,
Liogope jinamizi, na nyuzi zake mkizi,
Mwana mkaa masinzi, majivu wake mpenzi,
Utukufu si mazazi, utukufu ni majazi!

Radhiannu ihifadhi, maisha utangulizi,
Cheo kidata cha ngazi, kung'oka wala si kazi,
Neema sio ujuzi, bali kudrati Muizzi,
Utukufu si mazazi, utukufu ni majazi!

Ninashiba kwazo tenzi, zisizo nayo maudhi,
Naona kama faradhi, kadri ninavyoenzi,
Unapendeza ujuzi, mkuu ukimuenzi,
Utukufu si mazazi, utukufu ni majazi!

Nafsi yangu teuzi, yakidhi masimulizi,
Na jaribu kudarizi, waja wakawa wajuzi,
Wajue pa kukabidhi, na wao wapate majazi,
Utukufu si mazazi, utukufu ni majazi!

Mtukufu mwenye enzi, anipe yake majenzi,
Niuambae ushenzi, udhalimu nao wizi,
Yanisubiri makazi, yenye milele hifadhi,
Utukufu si mazazi, utukufu ni majazi!

Na wala si uongozi, usihomhofu Mwenyezi,
Unaofanya ajizi, dhuluma pia na wizi,
Haki usiomaizi, ila yenye machukizi,
Utukufu si mazazi, utukufu ni majazi!

Haki usiomaizi, ila yenye machukizi,
Na kumuudhi Mwenyezi, kwa wanhyonge uchafuzi,
Nafuu hauongezi, ila madhambi na wizi,
Utukufu si mazazi, utukufu ni majazi!

Nafsi naikabidhi, aitwae mwenye enzi,
Kuiongoza Azizi, katika yake malezi,
Samawati na Ardhi, ipate maangalizi,
Utukufu si mazazi, utukufu ni majazi!


Januari 29, 2012
Dar es Salaam

Cheo kilicho aali

Cheo na mtu kupewa, huweza kukiondoa,
Ila kwa wanaopewa, na umma uloridhia,
Uongozi huutwaa, nao wakamjazia,
Cheo kilicho aali, wananchi wanachokupa!

Cha mtu sijalilia, chenu ninakingojea,
Daraja kunipatia, na hadhi kunigaia,
Kwa ninayowaambia, na macho kuwafungua,
Cheo kilicho aali, wananchi wanachokupa!

Ukweli wanaojua, vipofu wameshakuwa,
Ubaya wanidhania, kwa mazuri kuwazia,
Shetani kawaiangia, yawasumbua dunia,
Cheo kilicho aali, wananchi wanachokupa!

Wa kwao wawaibia, vipi nitaangalia,
Makosa washindilia, na nchi inapotea,
Ubaya wameanzia, mimi ninamalizia,
Cheo kilicho aali, wananchi wanachokupa!

Nafsi naikataa, ya kwenu nimechukua,
Sina hata kitambaa, na mtu nilichopewa,
Kikoi ninakivaa, hadimu nimeshakua,
Cheo kilicho aali, wananchi wanachokupa!

Wanizika napumua, na wala sijawalilia,
Ni nyie nawangojea, niliowakusudia,
Msiache nifukua, walipshanifukia,
Cheo kilicho aali, wananchi wanachokupa!

Kwa sasa naazimia, ukimya kutangazia,
Nchi kuiangalia, njia inayochukua,
Mema wanaonitakia, nukuu watatumia,
Cheo kilicho aali, wananchi wanachokupa!

Dua ninawasomea, walo wema kujaliwa,
Na wabaya wakapewa, wanayoyastahilia,
Na siku ikifikia, mizani wataijua,
Cheo kilicho aali, wananchi wanachokupa!

Januari 29, 2012
Dar es Salaam

Cheo kilicho aali

Cheo na mtu kupewa, huweza kukiondoa,
Ila kwa wanaopewa, na umma uloridhia,
Uongozi huutwaa, nao wakamjazia,
Cheo kilicho aali, wananchi wanachokupa!

Cha mtu sijalilia, chenu ninakingojea,
Daraja kunipatia, na hadhi kunigaia,
Kwa ninayowaambia, na macho kuwafungua,
Cheo kilicho aali, wananchi wanachokupa!

Ukweli wanaojua, vipofu wameshakuwa,
Ubaya wanidhania, kwa mazuri kuwazia,
Shetani kawaiangia, yawasumbua dunia,
Cheo kilicho aali, wananchi wanachokupa!

Wa kwao wawaibia, vipi nitaangalia,
Makosa washindilia, na nchi inapotea,
Ubaya wameanzia, mimi ninamalizia,
Cheo kilicho aali, wananchi wanachokupa!

Nafsi naikataa, ya kwenu nimechukua,
Sina hata kitambaa, na mtu nilichopewa,
Kikoi ninakivaa, hadimu nimeshakua,
Cheo kilicho aali, wananchi wanachokupa!

Wanizika napumua, na wala sijawalilia,
Ni nyie nawangojea, niliowakusudia,
Msiache nifukua, walipshanifukia,
Cheo kilicho aali, wananchi wanachokupa!

Kwa sasa naazimia, ukimya kutangazia,
Nchi kuiangalia, njia inayochukua,
Mema wanaonitakia, nukuu watatumia,
Cheo kilicho aali, wananchi wanachokupa!

Dua ninawasomea, walo wema kujaliwa,
Na wabaya wakapewa, wanayoyastahilia,
Na siku ikifikia, mizani wataijua,
Cheo kilicho aali, wananchi wanachokupa!

Januari 29, 2012
Dar es Salaam

Urithi ulio bora

Ukirithisa ukweli, watoto watajaliwa,
Kalitangaza Jalali, jaza anayeitoa,
Iwapo chako halali, neema hukujalia,
Urithi ulio bora, ni ukweli kurithisha!

Imani ukitawakali, Manani hukwangalia,
Hakika huwa aali, mazuri kukujalia,
Huepusha idhilali, salama nyumba ikawa,
Urithi ulio bora, ni imani kurithisha!

Busara kuinakili, vizazi hujavifaa,
Jamii kuifadhili, ikawa yasaidia,
Wote wasio akili, uchi waje kubakia,
Urithi ulio bora, ni busara kurithisha!

Hekima si kitu ghali, ila wachache hupewa,
Wengi wasio akili, wavivu kuitumia,
Wengine ni mabahili, uchoyo huwazuia,
Urithi ulio bora, ni hekima kurithisha!

Hukamilika jamili, hisani ukitoa,
Wanyonge kuwafadhili, afueni wakajua,
Ukiwa mkavu wali, bado husherehekea,
Urithi ulio bora, ni hisani kurithisha!

Wema ni yetu asili, viumbe tumeumbiwa,
Ilal shetani katili, moyoni hutupindua,
Tukafanya ujahili, na njia kuipotea,
Urithi ulio bora, ni mazuri kurithisha!

Huiambaa adili, katika hii dunia,
Mabaya tusikabili, na mazuri kuambaa,
Hukasirika Jalali, na adhabu kuitoa,
Urithi ulio bora, ni adili kurithisha!

Ukoo uso asili, kabila hulikimbia,
Huipoteza fasili, ikaisha historia,
Wakabaki ni kalili, ya kwao wasiyojua,
Urithi ulio bora, kuenzi utamaduni!

Nchi isiyo asili, msingi hujapotea,
Kadhalika mihimili, kusimama kufulia,
Ikaanguka kikweli, pasiwe wa kuinyanyua,
Urithi ulio bora, kuenzi yetu asili!

Mama wa yetu asili, Kiswahili kutambua,
Bila kukipa akili, tutageuka vichaa,
Tushindwe kuukabili, utandawazi wa dunia,
Urithi ulio bora, kuienzi lugha yetu !

Kufunzia Kiswahili, ndio tutaendelea,
Itazame Brazili, China na India pia,
Ni wasio na akili, ndio wasiolijua,

Maovu kwa Kiswahili, watu wanayalewa,
Desturi na asili, hapa tukichanganyia,
Rijali na wanawali, viumbe kamili huwa,
Urithi ulio bora, ni maovu kuepusha!

Januari 29, 2012
Dar es Salaam

Kiongozi roho mbaya

RAIA huwachukia, ukweli wanaomwambia,
Kiongozi roho mbaya, haishi kuchanganyikiwa,
Na kila akiamua, mkenge hachi kwingia,
Kiongozi roho mbaya, raia huwachukia !

Watu atawabagua, wema na wake wabaya,
Kama vile anajua, moyoni yaliyokuwa,
Umungu atajitia, kumbe shetani kamvaa,
Kiongozi roho mbaya, raia huwabagua!

Uongo huusikia, kisha akazingatia,
Kila akikosolewa, vibaya hujisikia,
Badala kuongolewa, hatoacha kupotea,
Kiongozi roho mbaya, ukweli huuchukia !

Nafsi humtangulia, roho ikafuatia,
Kujua akajitia, hata asiyoyajua,
Wenye hoja husinzia, nafasi wakamwachia,
Kiongozi roho mbaya, nafsi hutangulza!

Ujibari hujitia, dhihaka kukomalia,
Mafuu humdhania, akili waliokuwa,
Ila watamuambaa, ahadiye kutimia,
Kiongozi roho mbaya, yake huyafikiria!

Kisasi hukusudia, ukubwa kuutetea,
Hujeruhi na kuua, akachezea dunia,
Na Mola humuachia, madhambi kumwongezea,
Kiongozi roho mbaya, kisasi yake tabia!

Januari 29, 2012
Dar es Salaam

Huchota maji bahari, wakacha maji baridi !

Bahati wasiopewa, hupata kikapotea,
Yalo mema huitiwa, nao wakayakimbia,
Pepo hutengenezewa, moto wakauchagua,
Huchota maji bahari, wakacha maji baridi !

Asali huiambaa, shubiri wakachagua,
Neema huikemea, balaa wakaridhia,
Nusura huikimbia, maasi wakaingia,
Huchota maji bahari, wakacha maji baridi !

Chumvi huichagua, sukari ikitakiwa,
Maji huyazidishia, ukavu unapotakiwa,
Gia ya nyuma hutia, ya mbele ikitakiwa,
Huchota maji bahari, wakacha maji baridi !

Chini hujifukia, juu wanapotakiwa,
Gizani hukomelea, nuru nje imejaa,
Milioni hutumia, wakati yatosha mia,
Huchota maji bahari, wakacha maji baridi !

Uoni huwapungua, uongo ukiwavaa,
Ya kweli huyakataa, uzaini kuridhia,
Juto mjukuu huwa, Joti wakamuachia,
Huchota maji bahari, wakacha maji baridi !

Januari 29, 2012
Dar es Salaam

Unyonyaji ukikua

BASHIRI macho hafungi, na huona kila jambo,
Msije kula mirungi, muone yasiyo tambo,
Ya mja hayamchengi, kwa sauti au wimbo,
Unyonyaji ukikua, nafuu iko njiani!

Kinyonga kwake haringi, ndiye aliyempa umbo,
Humbadili kwa rangi, adawa kukwepa mkumbo,
Na kwa mapozi ni kingi, ashinda hata mgambo,
Unyonyaji ukikua, nafuu iko njiani!

Viumbe walio wengi, ni wadogo kwa maumbo,
Na si watu wa mitungi, wala kwa wingi mapambo,
Hutafuta la msingi, mengine kwao vijambo,
Unyonyaji ukikua, nafuu iko njiani!

Lakini mlangilangi, yao yaendayo kombo,
Hutafuta kama nungwi, yaumizayo matumbo,
Kunao wavuta bangi, wajifanyao ni Rambo,
Unyonyaji ukikua, nafuu iko njiani!

Nao wenye mali nyingi, huwatumia mgambo,
Hawana chao kichungi, haki kuwa mtarimbo,
Watakayo ni shilingi, wengine kula vikumbo,
Unyonyaji ukikua, nafuu iko njiani!

Tamaa hawajivungi, hukaa nawe kitambo,
Hutumia nguvu nyingi, kuzikuza zao tambo,
Hata wenye fungu jingi, huzama kwenye mkumbo,
Unyonyaji ukikua, nafuu iko njiani!

Omwami na kina mangi, wanayaguna mafumbo,
Kadhalika na wasangi, na watani zao Rombo,
Hukiondoa kigungi, hata wakenda Urambo,
Unyonyaji ukikua, nafuu iko njiani!

Mwana muulize Dingi, kama naye ana jambo,
Nawe uwe ni mchungi, kunusuru lako tumbo,
Na ukaushe matangi, kwa dhuluma yake chambo,
Unyonyaji ukikua, nafuu iko njiani!


Januari 29, 2012
Dar es Salaam

Saturday, January 28, 2012

Mkubwa ajifanyaye, kuliko ya wananchi

Wakwibao mamlaka, wao wakayachukua,
Na kisha dhima kushika, watumwa sisi tukawa,
Hao ninawaambia, maadui wanakuwa,
Mkubwa ajifanyaye, kuliko yao wananchi!
Hudhani watu wajinga!

Wajinga huwadhania, watu wakiitikia,
Uzaini ukajaa, na vyeo kujilimbikia,
Na halafu husanzua, hazina kilichokuwa,
Mkubwa ajifanyaye, kuliko yao wananchi!
Hudhani watu wajinga!

Katiba tulopokea, hata hili inajua,
Mkubwa anayekuwa, ni mwananchi kutambua,
Sio vingine ikawa, kuzuka maharamia,
Mkubwa ajifanyaye, kuliko yao wananchi:
Katu usimpe nchi!

Wananchi tumeridhia, wao juu wamekuwa,
Ila hawajatuondoa, sisi chini kutupia,
Na kisha kutufagia, kama taka tulokuwa,
Mkubwa ajifanyaye, kuliko yao wananchi:
Huuza nchi kwa fisadi!

Nchi huwauzia, fisadi na haramia,
Ndani na nje pia, kila kitu kuchukua,
Raia na wazawa, utumwani kuingia,
Mkubwa ajifanyaye, kuliko yao wananchi:
Huuza nchi kwa fisadi!

Ni mkubwa Mtanzania, hili tunawaambia,
Kilelleni amekaa, wengine ni waajiriwa,
Waweza kuwatimua, katiba vyema ikikaa,
Mkubwa ajifanyaye, kuliko yao wananchi:
Hugawa nchi kwa wageni!

Na nchi wataigawa, kwa wageni na adawa,
Rushwa wakaichukua, binafsi kutumia,
Wasijali ya raia, na nchi kuitetea,
Mkubwa ajifanyaye, kuliko yao wananchi:
Hugawa nchi kwa wageni!

Enzi za kujipalia, majivu nayo mkaa,
Kila kitu kukitwaa, hata visivyostahilia,
Mwisho zimeshafikia, upya tutaangalia,
Mkubwa ajifanyaye, kuliko yao wananchi:
Hulipa wengine tone!

Hulipwa wanaosinzia, sio macho walokuwa,
Nchi wanaoinua, huwa ndio vibarua,
Na nchi wanaoua, sultani wanakuwa,
Mkubwa ajifanyaye, kuliko yao wananchi:
Hulipa wengine tone!

Pulizo hujifutua, upepo ndani kujaa,
Fahari kujisikia, asichochuma kuliwa,
Matanuzi kutanua, hata yasiyomfaa,
Mkubwa ajifanyaye, kuliko yao wananchi:
Kazi kwake matanuzi!

Hunyonya waliokuwa, vijijini wanakaa,
Dhuluma kuitumia, maeneo kusinyaa,
Huduma kuwaambaa, hata za msingi zikiwa,
Mkubwa ajifanyaye, kuliko yao wananchi:
Vijiji huvidharau!

Ni mtu wa kujisikia, hatowatii raia,
Ni watumwa hudhania, kama enzi awalia,
Kutawala ni kugawa, na wananchi kuwaua,
Mkubwa ajifanyaye, kuliko yao wananchi:
Hujenga makundi nchini!

Ahadi atazitoa, kweli zisizotimia,
Wanachi wakaendelea, kila hali kuumia,
Huku akifurahia, kisicho faa furahiwa,
Mkubwa ajifanyaye, kuliko yao wananchi:
Huwachuuza raia!

Nchi kwa nje hung'aa, huku ndani inafubaa,
Raia hudhulumiwa, wanyonge waliokuwa,
Pasiwe wa kuwatetea, maisha wakadidimia,
Mkubwa ajifanyaye, kuliko yao wananchi:
Huwa mbabaishaji!

Swahaba waliokuwa, Omari namfikiria,
Laiti tungejaliwa, na mfano nao tukawa,
Ingepaa Tanzania, wakawa huru raia,
Mkubwa ajifanyaye, kuliko yao wananchi:
Kazi huwa haiwezi!

Ni nuksi na balaa, hili yafaa kujua,
Ibada na nyingi dua, lazima kushikilia,
Zahama ikapungua, watu tuweze pumua,
Mkubwa ajifanyaye, kuliko yao wananchi:
Ataileta balaa!

Muua demokrasia

Anayefanya bidhaa, raia wa Tanzania,
Wanachama kununua, badala kujijengea,
Heshima ameishiwa, na utu umepungua,
Muua demokrasia, ni adui wa wananchi:
Mjinga ukimpa nchi!



Usimuonee haya, ukweli ni kumwambia,
Chake ukishachukua, kisha ukakitumia,
Na mwingine kuchagua, utu anaoujua,
Muua demokrasia, ni adui wa wananchi:
Wazimu ampaye nchi!

Ni bahau nakwambai, fedha imemuingia,
Ya ufisadi kujaa, na kichwani kuhamia,
Hana la kukufanyia, zaidi ya kukutumia,
Muua demokrasia, ni adui wa wananchi:
Kichaa ukimpa nchi!

Adawa demokrasia, sio wa kuaminiwa,
Mazuri hajakutakia, utumwa atakutiya,
Kisha akang'ang'ania, juu apate kukaa,
Muua demokrasia, ni adui wa wananchi:
Huona wote wajinga!

Watakiwa mhofia, ni mkoma keshakua,
Atakuambukizia, mbali nayeye kimbia,
Salama ubaki kuwa, kwa siha nayo afya,
Muua demokrasia, ni adui wa wananchi:
Mjinga ukimpa nchi!

Akili akuchezaya, na wanaomtumia,
Bei yako kuijua, apate kujiuzia,
Faida akapatia, kwake kubwa ilokuwa,
Muua demokrasia, ni adui wa wananchi:
Wazimu ampaye nchi!

Demokrasia ua, linapaswa kuchanua,
Madhila kuyaondoa, ukubwa wanaojitia,
Kisha kutusanzulia, tukabakia wakiwa,
Muua demokrasia, ni adui wa wananchi:
Kichaa ukimpa nchi!

Amkeni Watanzania, kataeni kutumiwa,
Wengine kunenepea, bungeni wakasinzia,
Hali nyie mwafa njaa, hakuna wa kuwasaidia,
Muua demokrasia, ni adui wa wananchi:
Huona wote wajinga!

Maisha kweli mafupi

Maisha mafupi kweli, nimekwishayachungua,
Ni hakika ujahili, vibaya kuyatumia,
Kasiye ya tasihili, kwa dakika hupotea,
Maisha kweli mafupi, ushikalo shikilia,
La, sivyo hujajutia!

Wakati sio kamili, na mwisho hutoujua,
Huwaka kama kandili, na kuzima kama jua,
Kila aliye akili, wahaka utamjaa,
Maisha kweli mafupi, ushikalo shikilia,
La, sivyo hujajutia!

Waishio kibahili, nguvu yao hupotea,
Vikaliwa kihalali, na haramu walokua,
Na mzika Kiswahili, Kingereza humuua,
Maisha kweli mafupi, ushikalo shikilia,
La, sivyo hujajutia!

Penda kilicho kamili, tena ni mia kwa mia,
Ukianza kunakili, fotokopi huungua,
Haitabaki asili, moyoni lililotimia,
Maisha kweli mafupi, ushikalo shikilia,
La, sivyo hujajutia!

Akheri naikabili, kesho yangu sijajua,
Haijanijia dalili, na mwishosijaujua,
Ila ni mustakabali, yafaa kujiandaa,
Maisha kweli mafupi, ushikalo shikilia,
La, sivyo hujajutia!

Ni wangapi marijali, wamekwishatangulai,
Wakiamini amali, baadaye watatoa,
Hakuyataka Adili, mapema kawanyakua,
Maisha kweli mafupi, ushikalo shikilia,
La, sivyo hujajutia!

Ni wangapi wanawali, ujana wameachia,
Walizima ja kandili, utambi kupupuliwa,
Imebakia jamili, hatuishi simulia,
Maisha kweli mafupi, ushikalo shikilia,
La, sivyo hujajutia!

Januari 28, 2012
Kibaha,
Mkoa wa Pwani

Hasira macho haina

Hasira kweli hasara, yafaa kuipuuza,
Huyu mkubwa kinara, kwa balaa kuongeza,
Kwako iwe ni king'ora, kikilia kunyamaza,
Hasira macho haina, nafusi huangamiza!

Watu hulewa chakara, kila wakiindeleza,
Wakageuka wakora, wenyewe kujichuuza,
Sio pwani wala bara, huyu ni wazimu pweza,
Hasira macho haina, nafusi huangamiza!

Waume wanadorora, kila ikiwadekeza,
Na wake wanazurura, walipoisindikiza,
Leo wote ni majura, wamebaki kupuuzwa,
Hasira macho haina, nafusi huangamiza!

Nyumbani ikisowera, masinzi hujayasanza,
Na wengine wakagura, utulivu kutukuza,
Vyote haviwi imara, hasira huteketeza,
Hasira macho haina, nafusi huangamiza!

Kazini kuiburura, shari unatengeneza,
Kama maiti hufura, kuzika ukikawiza,
Na harufu huvingira, kunusa hautoiweza,
Hasira macho haina, nafusi huangamiza!

Huyu mama wa hasara, inafaa kumuiza,
Anapoishi kugura, au la atakuchukiza,
Ni kubwa yake madhara, haivishi, huunguza,
Hasira macho haina, nafusi huangamiza!

Ninaiomba nusura, hasira niweze beza,
Anitunuku Ghafura, nimudu kujituliza,
Niwe mtu mwenye dira, nayakwangu  kutengeza,
Hasira macho haina, nafusi huangamiza!


Januari 28, 2012
Kibaha,
Mkoa wa Pwani

Huijui saa yako

Laiti tungelijua, wadanganya uhakika,
Mengi tungelitambua, yanaweza badilika,
Na safari ilokuwa, huenda hatutafika,
Huijui saa yako, huenda bila kwaheri!

Ahadi hatujapewa, hakuna kuyumkinika,
Twaingia kwenye njia, ramani hatujashika,
Hatuijui hatua, wapi itatupeleka,
Huijui saa yako, huenda bila kwaheri!

Mengi tunadhamiria, yasiyo na muafaka,
Ndoto nyingi hupotea, tupewalo tukashika,
Ikabidi kutulia, na kidogo kutosheka,
Huijui saa yako, huenda bila kwaheri!

Ila wapo wasojua, ilani nayo mipaka,
Kwingine hupindukia, nafsi ikawashika,
Wakajiona wajua, lolote kwa kufanyika,
Huijui saa yako, huenda bila kwaheri!

Manani huwainua, hadi juu wakafika,
Kisha hujawaachia, wabaki wanajiweka,
Ila hawatachelewa, kuyagundua mashaka,
Huijui saa yako, huenda bila kwaheri!

Kila akiachiliwa, mtu aja kuanguka,
Hawezi kujinyanyua, wala hatanyanyulika,
Mwisho umeshafikia, ndicho kilicho hakika,
Huijui saa yako, huenda bila kwaheri!

Usiifuate dunia, kwani utadanganyika,
Yafaa kujitambua, wewe sio kadhalika,
Uhai uliopewa, majukumu unataka,
Huijui saa yako, huenda bila kwaheri!

Nilinde katika njia, ninakusihi Rabuka,
Naogopa kupotea, si wakweli washirika,
Nisiwe wa kulaniwa, nikaikosa hakika,
Huijui saa yako, huenda bila kwaheri!


Januari 28, 2012
Kibaha,
Mkoa wa Pwani

Asili


 

Asili

Asiyejua

Asiwe cha kujivunia

Akashauriwa  na kuzainiwa

Asasi na fasili zao kuzitumia kama mkiwa,

Ashakum si matusi huyo keshapotea vigumu kuendeea:

Si hai

Ni mfu

Mumit

Ni mti unaonyauka ambao hautazaa tena tunda wala mbegu!

Friday, January 27, 2012

Uongozi si tamaa

Ukubwa wanaolilia, na juu kunyanyuliwa,
Inafaa wakajua, uongozi si hidaya,
Zawadi unaokuwa, kubaya utaishia,
Uongozi si kutaka, bali uwezo wa mtu!

Uongozi haijawa, na wala haitakuwa,
Mtu akateuliwa, na usukani kutwaa,
Lazima kuchaguliwa, ikawa wakubaliwa,
Uongozi si kupenda, bali kipaji cha mtu!

Uongozi si kung'aa, kwa rangi nje ukawa,
Na harufu kunukia, Uswizi zikitokea,
Wala sio matambaa, hata aghali yakiwa,
Uongozi si ukubwa, bali unachokifanya!

Uongozi sio njia, mtu kujineemeshea,
Huo ni ulafi huwa, mama yake ni tamaa,
Na uroho kuzidia, vitu kujilimbikia,
Uuongozi sio cheo, ila kukidhi matakwa!

Uongozi sio njaa, kwenda iganga ikawa,
Kila kitu kuchukua, hata akiba za wakiwa,
Wala si tumbo kujaa, kwa halali visivyokuwa,
Uongozi sio posho, bali watu kuwafaa!

Uongozi si nazaa, wengine kuwafagia,
Pembeni wao wakawa, ukaachiwa yote njia,
Hilo twaita balaa, na riha isiyofaa,
Uongozi si ving'ora, bali ni unyenyekevu!

Uongozi si kupewa, mamlaka kuchukua,
Ukubwa kujimegea, faida usiokuwa,
Na watu kuwaonea, hata usiowajua,
Uongozi si kutaka, bali uwezo wa mtu!

Ukubwa sio tamaa, kupenda kitu ikawa,
Huo ugonjwa wa ndaa, hukataliwa na ndia,
Kichwa huwa ni mkia, na mkia kichwa ikawa,
Uongozi si kupenda, bali kipaji cha mtu!

Uongozi si hisia, kitu kutozingatia,
Ikawa wa kutumia, kutafuta kutojua,
Uongozi hutanzua, matatizo kuondoa,
Uongozi si ukubwa, bali unachokifanya!

Uongozi hutambua, njia za kuendelea,
Sio kutoendelea, kisha ukajisifia,
Hata majuha wajua, hili hutowatania,
Uuongozi sio cheo, ila kukidhi matakwa!

Uongozi mashalaa, mkweli hatolilia,
Wenyewe utamjia, mtu alochagulia,
Chini kunyanyuliwa, juu akajajaliwa,
Uongozi sio posho, bali watu kuwafaa!

Uongozi si kupaa, bali kuyapalilia,
Taratibu kuingia, na juu kujipndia,
Mida ikishaingia, hodi utazisikia,
Uongozi si kunena, bali ni kujiandaa!

Uongozi si kupewa ubwabwa ukapokea,
Kwenye sahani kutiwa, uanze kujimegea,
Mwenyewe kuupakua, balaa huziondoa,
Uongozi si udenda, ni mbegu kujipandia!

Uongozi haujawa, nasibu kunasibia,
Kadiri inatakiwa, watu wakakufatia,
Nyumayo wakishakua, ndio vitani kwingia,
Uongozi si bahati, ni kadiri kuikuza!

Uongozi haujawa, wafuasi bila kuwa,
Au wanaokuchezaa, kama si kukupindua,
Jingine wasofikiria, ila urithi kuutwaa,
Uongozi si bahati, ni kadiri kuikuza!

Yarabi nipe nasaha, kusoma za kwangu dua,
Kuomba kinachofaa, sio mizigo kutwaa,
Baa kuniepushia, husuda nazo hadaa,
Uongozi si ving'ora, bali ni unyenyekevu!


Januari 27,2012
Dar es salaam

Thursday, January 26, 2012

Yuraniamu Tanzania hapana...


I hate Uranium, marauders spare my people
1.
Laana twawaombea, waidhinishao hili,
kuchimbwa Uranium, hapa kwetu Tanzania,
Wakati haujafikia, na hatujajiandaa,
ha hatunavyo vifaa, tahadhari kuchukua:
Nchi inayolaaniwa,
Maajabu huamua,
Wizi wakishaujua,
Lolote watajifanyia,
Huongozwa na tamaa,
na mwisho sote twajua:
Uchu na zenu tamaa, tunawaonya wakubwa,
mauti mwatutakia!

2.
Laana twawaombea, waidhinishao hili,
kuchimbwa Uranium, hapa kwetu Tanzania,
Wakati haujafikia, na hatujajiandaa,
ha hatunavyo vifaa, tahadhari kuchukua:
Bungeni ukiangalia,
Watu wengi wasinzia,
Hawa ndio Watanzania,
Dhamana mtawaachia
Mengi wanayoamua,
kichefuchefu yatia:
Uchu na zenu tamaa, tunawaonya wakubwa,
mauti mwatutakia!

3.
Laana twawaombea, waidhinishao hili,
kuchimbwa Uranium, hapa kwetu Tanzania,
Wakati haujafikia, na hatujajiandaa,
ha hatunavyo vifaa, tahadhari kuchukua:
Wabunge wa kutegemewa,
Hofu sasa wanatutia,
Si wate wa kufikiria,
Bali ndiyo kuitikia,
Maamuzi yenye udhia,
Rahisi sana kuua:
Uchu na zenu tamaa, tunawaonya wakubwa,
mauti mwatutakia!

4.
Laana twawaombea, waidhinishao hili,
kuchimbwa Uranium, hapa kwetu Tanzania,
Wakati haujafikia, na hatujajiandaa,
ha hatunavyo vifaa, tahadhari kuchukua:
Ni wavivu waliokuwa
Vigumu kujisomea
Miswaada kuipitia
Sio linalotarajiwa
Bungeni mbumbumbu wawa:
Uchu na zenu tamaa, tunawaonya wakubwa,
mauti mwatutakia!

5.
Laana twawaombea, waidhinishao hili,
kuchimbwa Uranium, hapa kwetu Tanzania,
Wakati haujafikia, na hatujajiandaa,
ha hatunavyo vifaa, tahadhari kuchukua:
Marekani wakataa,
Makwao kuichimbua,
Kondomu na vyandarua
Sisi tukishapatiwa
Hili tunalikubalia?
Uchu na zenu tamaa, tunawaonya wakubwa,
mauti mwatutakia!

6.
Laana twawaombea, waidhinishao hili,
kuchimbwa Uranium, hapa kwetu Tanzania,
Wakati haujafikia, na hatujajiandaa,
ha hatunavyo vifaa, tahadhari kuchukua:
Katazameni dunia,
Kwingineko kulokuwa,
Yuraniamu inaua
Na ulemavu kusia
Viumbe wanazaliwa
Ajabu waliokuwa:
Uchu na zenu tamaa, tunawaonya wakubwa,
mauti mwatutakia!

6.
Laana twawaombea, waidhinishao hili,
kuchimbwa Uranium, hapa kwetu Tanzania,
Wakati haujafikia, na hatujajiandaa,
ha hatunavyo vifaa, tahadhari kuchukua:
Ni heri kilema kuwa
Wa mwili unaovia,
Kuliko kilema kuwa
Wa akili kutumiwa
Na wazungu wenye njaa
Uhai wasiotutakia:
Uchu na zenu tamaa, tunawaonya wakubwa,
mauti mwatutakia!

7.
Laana twawaombea, waidhinishao hili,
kuchimbwa Uranium, hapa kwetu Tanzania,
Wakati haujafikia, na hatujajiandaa,
ha hatunavyo vifaa, tahadhari kuchukua:
Ubepari wakolea,
Chamani unaenea
Wajamaa walokuwa
Uuaji wanadhamiria
Hakika nitawashangaa,
Yao mkiyasikia:
Uchu na zenu tamaa, tunawaonya wakubwa,
mauti mwatutakia!

8.
Laana twawaombea, waidhinishao hili,
kuchimbwa Uranium, hapa kwetu Tanzania,
Wakati haujafikia, na hatujajiandaa,
ha hatunavyo vifaa, tahadhari kuchukua:
Uranium balaa
Tuepuke kukaribia
Vipo tulivyojaliwa
Havifai kuvifukua
Ni mizimu iliyokuwa
Ukishika walipuliwa:
Uchu na zenu tamaa, tunawaonya wakubwa,
mauti mwatutakia!

9.
Laana twawaombea, waidhinishao hili,
kuchimbwa Uranium, hapa kwetu Tanzania,
Wakati haujafikia, na hatujajiandaa,
ha hatunavyo vifaa, tahadhari kuchukua:
Bado hatujafikia
Kuwa nayo kali njaa
Kama yao waheshimiwa
Ubinafsi walojaa
Mwenye njaa wasomjua
Mzigo wanaokuwa
Kwa nchi kutokuifaa:
Uchu na zenu tamaa, tunawaonya wakubwa,
mauti mwatutakia!

10.
Laana twawaombea, waidhinishao hili,
kuchimbwa Uranium, hapa kwetu Tanzania,
Wakati haujafikia, na hatujajiandaa,
ha hatunavyo vifaa, tahadhari kuchukua:
Hakimu twamgeukia
Mmiliki wa dunia
Haya tutamuachia
Uamuzi kufikia
Na tishio wanaokuwa
Kuhukumu linalofaa:
Uchu na zenu tamaa, tunawaonya wakubwa,
mauti mwatutakia!

Please Lord protect the ignorasmuses!

Tuesday, January 24, 2012

Utoto mtihani

Kuna watu wasokuwa, hata umri ukiwa,
Utotoni hubakia, utu uzima kupwaya,
Na wanayojifanyia, tazama utawajua,
Utoto nao mtihani, kuna watu wengi sana,
kabisa wasiokuwa !

Utoto unapoanzia, hukua na kukomaa,
Na siku ikifikiya, ya utoto huachia,
Ila ukiendeleya, vingine hukudhania,
Utoto nao mtihani, kuna watu wengi sana,
kabisa wasiokuwa !

Mtu mzima kulia, kubwa jinga tutajua,
Na mwanamme ukiwa, tena ni kubwa balaa,
Hulia bila kulia, chinichini kugumia,
Utoto nao mtihani, kuna watu wengi sana,
kabisa wasiokuwa !

Ovyo kutembeatembea, bila nalo lengo kuwa,
Jambo haujaazimia, wala shabaha kutiya,
Ukifika unakaa, hata usipotakiwa,
Utoto nao mtihani, kuna watu wengi sana,
kabisa wasiokuwa !

Midoli kuichezea, ukubwani haijawa,
Ila ukiendeleya, kasoro tutakutia,
Ukubwani hujaingia, bila haya kuachia,
Utoto nao mtihani, kuna watu wengi sana,
kabisa wasiokuwa !

Wanasesere nunua, watoto kuwagawiya,
Ila ukiwachezeya, tuhuma itaingiya,
Majinuni hudhaniwa, watu kukukimbiya,
Utoto nao mtihani, kuna watu wengi sana,
kabisa wasiokuwa !

Ukubwa ukiingia, vipo pia vyenye unaa,
Ni vitu navyo vifaa, wote tunavyovitumia,
Mmoja akizidishia, utoto hulalamikiwa,
Utoto nao mtihani, kuna watu wengi sana,
kabisa wasiokuwa !

Utoto nyingi tamaa, vitu kuvikimbilia,
Hata hatari vikiwa, hadi ajali ikawa,
Wazazi wawe walia, nuksi kujawavaa,
Utoto nao mtihani, kuna watu wengi sana,
kabisa wasiokuwa !

Ukubwa huutambua, uiyonapo kinaya,
Mtu kutochanganyikiwa, na lolote linalokuwa,
Ajua pa kutulia, na wakati kutumia,
Utoto nao mtihani, kuna watu wengi sana,
kabisa wasiokuwa !

Hakubali kudanganywa, kama mtoto akiwa,
Na aliye muelewa, hadanganyi wengine pia,
Ukubwa kuzingatia, ukweli kutochezea,
Utoto nao mtihani, kuna watu wengi sana,
kabisa wasiokuwa !

Saturday, January 21, 2012

Viongozi na Menejimnti

Viongozi walokuwa, haya kweli wanajua,
Wapi walikojifunzia, na kutia vitendoni,
Ni watu wa nadharia, au kazi watambua,
Si wanaobabia, na ujuzi kujitia,
Ya wengine kuvamia, kuacha wanayojua,
Kisha kuwaharibia, makosa kuwasingizia,
Haya ninayahofia, naamini yatokea,
Na wananchi wasojua, wazidi kuvumilia,
Laiti wangelijua, wangeishawasanzua,
Kwa kuwa si wanaojua, na nchi haitoendelea:

Kwanza kuna majukumu:
Kuna majukumu ya maingiliano na jamii;
Kiaha kuna majukumu ya habari na mawasiliano;
halafu kuna majukumu ya ufanyaji maamuzi bora!

Je, waziri wetu huyu, na katibu wake mkuu,
Mkuu wa mkoa huyu,na watumishi wadau,
Wanafahamu kazi zao ni pamoja na:

Uwakilishi:
Unatakiwa kuwakilisha waliokuchagua,
Na sio kujiwakilisha na kujilimbia,
Tajiri ukijakua, na sifa kujipatia,
Na unaowatumikia, umasikini wazidia,
Wewe sio kiongozi, bali dhulumati, mbinafsi, njaa kali,
Mhamishaji, mnywaji na mlaji tu !

Kiunganishi:
Watakiwa kuyajua, nchini yanayotokea,
Na eneo lako likawa, moyoni lakaririwa,
Hapana linalotokea, bila wewe kuyajua,
Ndivyo inavyotokea, kwa polisi na raia?
Tajiri ukijakua, na sifa kujipatia,
Na unaowatumikia, umasikini wazidia,
Wewe sio kiongozi, bali dhulumati, mbinafsi, njaa kali,
Mhamishaji, mnywaji na mlaji tu !

Kuongoza:
Kuongoza twatitia, hufanza tusiyojua
Elimu imepungua, bahati twategemea,
Hana wa kufikiria, jipya lililokuwa,
Nani kuonyesha njia, wakati wengi tunapotea?
Kwa maana hii nawaambia, kiongozi hajatokea:
Tajiri ukijakua, na sifa kujipatia,
Na unaowatumikia, umasikini wazidia,
Wewe sio kiongozi, bali dhulumati, mbinafsi, njaa kali,
Mhamishaji, mnywaji na mlaji tu !


Msemzaji:
Taasisi yatakiwa, na msemaji kuwa,
Yote anayoelewa, nchini yanayotokea,
Kadhalika na dunia, na hiyo yake tasnia,
Vinginevyo bogasi anakuwa, mapapai ya kuliwa:
Tajiri ukijakua, na sifa kujipatia,
Na unaowatumikia, umasikini wazidia,
Wewe sio kiongozi, bali dhulumati, mbinafsi, njaa kali,
Mhamishaji, mnywaji na mlaji tu !


Ukusanyaji:
Na habari kuzitoa, lazima kuzipokea,
Meneja anatakiwa, haya kufuatilia,
Habari zote zikawa, anajikusanyia,
Kisha akazitia, kwenye kompyuta kuwa,
Na chochote hunyanyua, akaweza kukupatia:
Tajiri ukijakua, na sifa kujipatia,
Na unaowatumikia, umasikini wazidia,
Wewe sio kiongozi, bali dhulumati, mbinafsi, njaa kali,
Mhamishaji, mnywaji na mlaji tu !


Utawanyaji:
Na inavyoruhusiwa, watu hujawagtuimia,
Habari za historia, na zinazoendelea,
Hakuna litakalowia, ni gumu kulitambua,
Sayansi yanuia, vidoleni haya kuwa,
Maamuzi ukaamua, sahihi yaliyokuwa:
Tajiri ukijakua, na sifa kujipatia,
Na unaowatumikia, umasikini wazidia,
Wewe sio kiongozi, bali dhulumati, mbinafsi, njaa kali,
Mhamishaji, mnywaji na mlaji tu !


Kugawa rasilimali:
Kugawa rasilimali, kiongozi atakiwa,
Ulimbikaji ajali, laana hulaaniwa,
Hata ukipata mali, mafunza huja kujilia,
Ukafa wewe bahili, hujui kuyatumia,
Na dhuluma kutumia, wana huwa ni vichaa,
Kizazi kikapotea, na jina kusahauliwa:
Tajiri ukijakua, na sifa kujipatia,
Na unaowatumikia, umasikini wazidia,
Wewe sio kiongozi, bali dhulumati, mbinafsi, njaa kali,
Mhamishaji, mnywaji na mlaji tu !



Upatania masuala:
Shughuli kupatania, na watu kupatanisha,
Yataka kuvumilia, na watu kuunganisha,
Ubia ukauandaa, kuwafaa kimaisha,
Wao kuja kutambua, ustawi warahisisha:
Tajiri ukijakua, na sifa kujipatia,
Na unaowatumikia, umasikini wazidia,
Wewe sio kiongozi, bali dhulumati, mbinafsi, njaa kali,
Mhamishaji, mnywaji na mlaji tu !


Mshindania bei nafuu na ubora wa vitu:
Mwenyewe ukijifaa, na hasara watu kutia,
Nuksi zitakufua, na kuzioga balaa,
Umri hujapungua, na neema kusinyaa,
Ikawa usiyefaa, katika pepo na dunia,
Na moto kukungojea, kwa nafuu kutoitoa:
Tajiri ukijakua, na sifa kujipatia,
Na unaowatumikia, umasikini wazidia,
Wewe sio kiongozi, bali dhulumati, mbinafsi, njaa kali,
Mhamishaji, mnywaji na mlaji tu !


Mfanya maamuzi:
Maamuzi yatakiwa, haraka kujakutolewa,
Kusinzia ni nazaa, na kusahau balaa,
Kiongozi akijua, hili kwake ni dunia,
Na asipokulijua, ajipalia mkaa,
Viumbe hawakuuzaliwa, milele kujakaa,
Hamsini ikitua, wengi budi kujifia:
Na usipoamua, ukawa unachelewa,
Watu wakijifia, lawama wazichukua,
Huwezi mtu kumfaa, kama akishajifia:
Tajiri ukijakua, na sifa kujipatia,
Na unaowatumikia, umasikini wazidia,
Wewe sio kiongozi, bali dhulumati, mbinafsi, njaa kali,
Mhamishaji, mnywaji na mlaji tu !


mwisho/2012.o1.21

Kawa lisipokuwepo

Kawa ninakuulizia, wapi umepotelea,
Mambo kwa leo balaa, waziwazi vyabakia,
Hata vinavyotakiwa, watu kutokuvijua,
Lisipokuwepo KAWA, kila kitu njenje!

Kila kitu wazi huwa, toka kawa kupotea,
Dhahiri vyote hujua, hata siri vya kutiwa,
Ni sinema ilokua, watu wanajionea,
Lisipokuwepo KAWA, kila kitu njenje!

Mama nilivyomjua, kawa alilitumia,
Watoto hatukujua, baba tukimpelekea,
Hadi akalifunua, nasi tukaruhusiwa,
Lisipokuwepo KAWA, kila kitu njenje!

Sasa vyabebwa huria, njenje vimekuwa,
Aina unaijua, na ukubwa kukadiria,
Na rangi utazijua, zote zilizonakshiwa,
Lisipokuwepo KAWA, kila kitu njenje!

Siyaoni maridhia, haya yanayotokea,
Ninaona ni udhia, na raha inapotea,
Wazee nawalilia, mila hii kurudia,
Lisipokuwepo KAWA, kila kitu njenje!

Uswahili majaliwa, desturi maashallaa,
Uzungu twakimbilia, hadi nguo kujivua?
Hakika nawashangaa, viumbe mliokuwa,
Lisipokuwepo KAWA, kila kitu njenje!

Utamu unapungua, kila kinachovuliwa,
Ndio maana zajaa, ndoa zinazojifia,
Yakizidi mazoea, haraka huwa udhia,
Lisipokuwepo KAWA, kila kitu njenje!

Watu wanaililia, sapraizi mwajua,
Wazungu waliokuwa, ni mila imeenea,
Mojawapo ndilo kawa, tunapaswa kutumia,
Lisipokuwepo KAWA, kila kitu njenje!

Maneno nawaambia, kazi ni kufikiria,
Mazuri mkiyajua mtayashughulikia,
Likajarejea kawa, kama tulivyoanzia,
Lisipokuwepo KAWA, kila kitu njenje!

Kupika sasa gharama

Nahamia hotelini, kupika sasa gharama,
Bado twateta chumbani, kuhusu hii azma,
Twahofia inflesheni, njaa kuja tusakama,
Kupika sasa gharama, nahamia hotelini!

Kupika sasa gharama, nahamia hotelini!

Ingawa nautamani, wali wa nazi kuwama,
Robo yazidi thamani, mshahara siku nzima,
Siwezi nimebaini, sintofika mwezi mzima,
Kupika sasa gharama, nahamia hotelini!

Majirani kwaherini, hotelini nahamia,
Mtu kuwa mashakani, naona hii dhuluma,
Hali hii si utani, kama hauna neema,
Kupika sasa gharama, nahamia hotelini!

Hotelini kuhamia, sahani nusu twagawa,
Mchuzi huongezewa, japo maji wametia,
Na siku itaingia, na kesho kuamkia,
Kupika sasa gharama, nahamia hotelini!

Mkaa sintanunua, elfu tatu kwa fungu,
Nyanya nitaachia, wahindi nao wazungu,
Na hayo mafuta taa, redioni kuyasikia,
Kupika sasa gharama, nahamia hotelini!

Mafuta ya kupikia, nitayakwepa kabisa,
Ila kwa kujipakia, badala yenye anasa,
Na chumvi sintonunua, ila kwa kujichulia,

Harufu mbaya nyumbani, sasa itajapungua,
Na nzi watabaini, wenyewe wakaishia,
Usafi tutauwini, nuru nyumba ikajaa,
Kupika sasa gharama, nahamia hotelini!

Mwana kuja kuungua, tena siwezi hofia,
Nitazikwepa balaa, nyingi zinazotokea,
King'amuzi kukivaa, hata mchana ikiwa,
Kupika sasa gharama, nahamia hotelini!

Kisu niache tumia, na makali kuhofia,
Ila matunda yakiwa, shambani yametokea,
Kumenya nitamuambia, mama watoto kuzua,
Kupika sasa gharama, nahamia hotelini!

Na kisha kujisomea, muda sintopungukiwa,
Shahada kuiwania, ufukara kukataa,
Ni heri iliyokuwa, wengi hatujaijua,
Kupika sasa gharama, nahamia hotelini!

Bei zikijapungua, nitakuwa niahapoa,
Huko tena kurudia, ni vigumu itakuwa,
Mteja nitabakia, kwa raha kuizoea,
Kupika sasa gharama, nahamia hotelini!

Haweshi jipendekeza

Kiongozi wa kuchagua, na sio kuteuliwa,
Mtumwa hutumikia, cheo anayemfaa,
Hata vibaya ikawa, aitumia sheria,
Haweshi jipendekeza, wote wa kuteuliwa!

Kiongozi wa mkoa, watu wanayemchagua,
Hawezi nguvu tumia, mikutano kuzuia,
Au mabomu kulipua, watu ovyo wakalia,
Haweshi jipendekeza, wote wa kuteuliwa!

Ila kula alopewa, roboti hujifyatua,
Otomatiki akawa, hata hatari kutia,
Nchi huja kuchukiwa, ukiwa na watu hawa,
Haweshi jipendekeza, wote wa kuteuliwa!

Ni vifuu vya kujaa, si nazi za kukomaa,
Na akili kutumia, mashaka makubwa huwa,
Lambalamba hujakua, bendera ya kupepewa,
Haweshi jipendekeza, wote wa kuteuliwa!

Ndio maana mikoa, kazi kujaendelea,
Hayana wa kuiimua, washindani kuja kuwa,
Hekima ikaingia, na busara kutumiwa,
Haweshi jipendekeza, wote wa kuteuliwa!

Haweshi jipendekeza, wote wa kuteuliwa!

Mkoloni kaanzia, watu wake kuteua,
Ni sera iliyovia, wakubwa wang'ang'ania,
Ukubwa wanahofia, utakujakuwapotea,
Haweshi jipendekeza, wote wa kuteuliwa!

Ukubwa wanahofia, utakujakuwapotea,
Mikoa wakiachia, kujiongoza ikawa,
Makubwa watayazua, na aibu kuwatia,
Haweshi jipendekeza, wote wa kuteuliwa!

Daktari na mbunge, nani alipwe zaidi?

Kati yao watu hawa, nani haki itakuwa,
Mshahara kuchukua, mwingi uliotoshea,
Asiwe kupungukiwa, huduma bora kutoa?
Daktari na mbunge, nani alipwe zaidi?

Kisomo alichosomea, kwanza hebu fikiria,
Na kazi aliyopewa, muhimu ilivyokuwa,
Na muda anaokaa, watu kushughulikia,
Daktari na mbunge, nani alipwe zaidi?

Na maisha kuokoa, watu hai kubakia,
Hali wanaoumia, upya kuwatengenea,
Na afya kuangalia, siha wakajipatia,
Daktari na mbunge, nani alipwe zaidi?

Elimu wanaotoa, ubunge ukajapewa,
Maarifa wanaogawa, ujanja ukajaliwa,
Macho wanaokufungua, ukweli ukatambua,
Daktari na mbunge, nani alipwe zaidi?

Uchafu wanaotwaa, na usafi kukutia,
Choo wanaochukua, na mkojo kuwavaa,
Kusinzia wasiojua, na kulala kwa kubabia,
Daktari na mbunge, nani alipwe zaidi?

Njia wasojipatia, vingine kujichumia,
Teni pasenti wasopewa, wala rushwa kugaiwa,
Mtaji wasiokuwa, jasiriamali wakawa,
Daktari na mbunge, nani alipwe zaidi?

Nchi wasiojilia, ila wao wanaliwa,
Ukubwa wasiotumia, wengine kunyanyapaa,
Juu wanaowafaa, na chini kusaidia,
Daktari na mbunge, nani alipwe zaidi?

Mwalimu na mbunge, nani alipwe zaidi?

Kati yao watu hawa, nani haki itakuwa,
Mshahara kuchukua, mwingi uliotoshea,
Asiwe kupungukiwa, huduma bora kutoa?
Mwalimu na mbunge, nani alipwe zaidi?

Kisomo alichosomea, kwanza hebu fikiria,
Na kazi aliyopewa, muhimu ilivyokuwa,
Na muda anaokaa, watu kushughulikia,
Mwalimu na mbunge, nani alipwe zaidi?

Na maisha kuokoa, watu hai kubakia,
Hali wanaoumia, upya kuwatengenea,
Na afya kuangalia, siha wakajipatia,
Mwalimu na mbunge, nani alipwe zaidi?

Elimu wanaotoa, ubunge ukajapewa,
Maarifa wanaogawa, ujanja ukajaliwa,
Macho wanaokufungua, ukweli ukatambua,
Mwalimu na mbunge, nani alipwe zaidi?

Uchafu wanaotwaa, na usafi kukutia,
Choo wanaochukua, na mkojo kuwavaa,
Kusinzia wasiojua, na kulala kwa kubabia,
Mwalimu na mbunge, nani alipwe zaidi?

Njia wasojipatia, vingine kujichumia,
Teni pasenti wasopewa, wala rushwa kugaiwa,
Mtaji wasiokuwa, jasiriamali wakawa,
Mwalimu na mbunge, nani alipwe zaidi?

Nchi wasiojilia, ila wao wanaliwa,
Ukubwa wasiotumia, wengine kunyanyapaa,
Juu wanaowafaa, na chini kusaidia,
Mwalimu na mbunge, nani alipwe zaidi?

Udhalilishaji maiti

Kuna dhifa mwazijua, hakuna asiyeingia,
Kama choo kuingia, hata mkubwa akiwa,
Na chakula kinaliwa, na hai wanaokua,
Udhalilishaji maiti, wote twajidhalilisha!

Na ng'ambo mnapokwenda, tembeleeni mochwari,
Ili mpate jifunda, ujenzi ulio kheri,
Mkirudi kuyatenda, aibu yanayoghairi,
Udhalilishaji maiti, wote twajidhalilisha!

Mwageuka mijipoda, hamuishi kuosheka,
Hamna mnaloganda, akilini kukalika,
Ndio twakosa kuwanda, sasa yayumkinika,
Udhalilishaji maiti, wote twajidhalilisha!

Chumba hiki maalumu, sote lazima kutua,
Mmezishika hatamu, mwashinda kulitambua,
Ufu tambiko muhimu, na staha yatakiwa,
Udhalilishaji maiti, wote twajidhalilisha!

Marehemu kwangalia, wazima hubarikiwa,
Humpendeza alokuwa, juu akiangalia,
Na daraja hunyanyua, kwa ya kesho kuelewa,
Udhalilishaji maiti, wote twajidhalilisha!

Suti leo mwazivaa, chuenlai mlokuwa,
Ila mmezidi fubaa, na utu kupungukiwa,
Wenyewe mwajiangalia, na siyo jumuiya?
Udhalilishaji maiti, wote twajidhalilisha!

Dhahabu ndoo ikiwa, mochwari zaweza jaa,
Nchini zikaenea, hadi vijijini pia,
Ila kinachotokea, maiti twawatania,
Udhalilishaji maiti, wote twajidhalilisha!

Cheichei Tanzania, na nyinyi Watanzania,
Hivi mmeshaambiwa, mochwari hamtaingia?
Nje sinema zatoa, fahari kujivunia,
Udhalilishaji maiti, wote twajidhalilisha!

Zetu ukiziangalia, hutamani kukimbia,
Maiti chini wajaa, na ovyo kufunuliwa,
Laana kubwa sikia, hili ninawaambia,
Udhalilishaji maiti, wote twajidhalilisha!

Fedha tunazitumia, kule kusikotufaa,
Thawabu twazikimbia, jua juu limekuwa,
Machweo yakiingia, jangwani tukaishia,
Udhalilishaji maiti, wote twajidhalilisha!

Makaburi tumeweza, angalau kuwekeza,
Sasa ni kuendeleza, na matunzo kuongeza,
Walotangulia kwanza, haya yatawapendeza,
Udhalilishaji maiti, wote twajidhalilisha!

Rabana tupe jamala, kurehemu walokuwa,
Kitaifa ni suala, lataka walokwishakua,
Wanaojua risala, na amri zilokuwa,
Udhalilishaji maiti, wote twajidhalilisha!

Daktari na mbunge, nani alipwe zaidi?

Kati yao watu hawa, nani haki itakuwa,
Mshahara kuchukua, mwingi uliotoshea,
Asiwe kupungukiwa, huduma bora kutoa?
Daktari na mbunge, nani alipwe zaidi?

Kisomo alichosomea, kwanza hebu fikiria,
Na kazi aliyopewa, muhimu ilivyokuwa,
Na muda anaokaa, watu kushughulikia,
Daktari na mbunge, nani alipwe zaidi?

Na maisha kuokoa, watu hai kubakia,
Hali wanaoumia, upya kuwatengenea,
Na afya kuangalia, siha wakajipatia,
Daktari na mbunge, nani alipwe zaidi?

Elimu wanaotoa, ubunge ukajapewa,
Maarifa wanaogawa, ujanja ukajaliwa,
Macho wanaokufungua, ukweli ukatambua,
Daktari na mbunge, nani alipwe zaidi?

Uchafu wanaotwaa, na usafi kukutia,
Choo wanaochukua, na mkojo kuwavaa,
Kusinzia wasiojua, na kulala kwa kubabia,
Daktari na mbunge, nani alipwe zaidi?

Njia wasojipatia, vingine kujichumia,
Teni pasenti wasopewa, wala rushwa kugaiwa,
Mtaji wasiokuwa, jasiriamali wakawa,
Daktari na mbunge, nani alipwe zaidi?

Nchi wasiojilia, ila wao wanaliwa,
Ukubwa wasiotumia, wengine kunyanyapaa,
Juu wanaowafaa, na chini kusaidia,
Daktari na mbunge, nani alipwe zaidi?

Mwalimu na mbunge

Kati yao watu hawa, nani haki itakuwa,
Mshahara kuchukua, mwingi uliotoshea,
Asiwe kupungukiwa, huduma bora kutoa?
Mwalimu na mbunge, nani alipwe zaidi?

Kisomo alichosomea, kwanza hebu fikiria,
Na kazi aliyopewa, muhimu ilivyokuwa,
Na muda anaokaa, watu kushughulikia,
Mwalimu na mbunge, nani alipwe zaidi?

Na maisha kuokoa, watu hai kubakia,
Hali wanaoumia, upya kuwatengenea,
Na afya kuangalia, siha wakajipatia,
Mwalimu na mbunge, nani alipwe zaidi?

Elimu wanaotoa, ubunge ukajapewa,
Maarifa wanaogawa, ujanja ukajaliwa,
Macho wanaokufungua, ukweli ukatambua,
Mwalimu na mbunge, nani alipwe zaidi?

Uchafu wanaotwaa, na usafi kukutia,
Choo wanaochukua, na mkojo kuwavaa,
Kusinzia wasiojua, na kulala kwa kubabia,
Mwalimu na mbunge, nani alipwe zaidi?

Njia wasojipatia, vingine kujichumia,
Teni pasenti wasopewa, wala rushwa kugaiwa,
Mtaji wasiokuwa, jasiriamali wakawa,
Mwalimu na mbunge, nani alipwe zaidi?

Nchi wasiojilia, ila wao wanaliwa,
Ukubwa wasiotumia, wengine kunyanyapaa,
Juu wanaowafaa, na chini kusaidia,
Mwalimu na mbunge, nani alipwe zaidi?

Mkunga na mbunge, nani alipwe zaidi?

Kati yao watu hawa, nani haki itakuwa,
Mshahara kuchukua, mwingi uliotoshea,
Asiwe kupungukiwa, huduma bora kutoa?
Mkunga na mbunge, nani alipwe zaidi?

Kisomo alichosomea, kwanza hebu fikiria,
Na kazi aliyopewa, muhimu ilivyokuwa,
Na muda anaokaa, watu kushughulikia,
Mkunga na mbunge, nani alipwe zaidi?

Na maisha kuokoa, watu hai kubakia,
Hali wanaoumia, upya kuwatengenea,
Na afya kuangalia, siha wakajipatia,
Mkunga na mbunge, nani alipwe zaidi?

Elimu wanaotoa, ubunge ukajapewa,
Maarifa wanaogawa, ujanja ukajaliwa,
Macho wanaokufungua, ukweli ukatambua,
Mkunga na mbunge, nani alipwe zaidi?

Uchafu wanaotwaa, na usafi kukutia,
Choo wanaochukua, na mkojo kuwavaa,
Kusinzia wasiojua, na kulala kwa kubabia,
Mkunga na mbunge, nani alipwe zaidi?

Njia wasojipatia, vingine kujichumia,
Teni pasenti wasopewa, wala rushwa kugaiwa,
Mtaji wasiokuwa, jasiriamali wakawa,
Mkunga na mbunge, nani alipwe zaidi?

Nchi wasiojilia, ila wao wanaliwa,
Ukubwa wasiotumia, wengine kunyanyapaa,
Juu wanaowafaa, na chini kusaidia,
Mkunga na mbunge, nani alipwe zaidi?

Daktari na waziri, nani alipwe zaidi?

Kati yao watu hawa, nani haki itakuwa,
Mshahara kuchukua, mwingi uliotoshea,
Asiwe kupungukiwa, huduma bora kutoa?
Daktari na waziri, nani alipwe zaidi?

Kisomo alichosomea, kwanza hebu fikiria,
Na kazi aliyopewa, muhimu ilivyokuwa,
Na muda anaokaa, watu kushughulikia,
Daktari na waziri, nani alipwe zaidi?

Na maisha kuokoa, watu hai kubakia,
Hali wanaoumia, upya kuwatengenea,
Na afya kuangalia, siha wakajipatia,
Daktari na waziri, nani alipwe zaidi?

Elimu wanaotoa, ubunge ukajapewa,
Maarifa wanaogawa, ujanja ukajaliwa,
Macho wanaokufungua, ukweli ukatambua,
Daktari na waziri, nani alipwe zaidi?

Uchafu wanaotwaa, na usafi kukutia,
Choo wanaochukua, na mkojo kuwavaa,
Kusinzia wasiojua, na kulala kwa kubabia,
Daktari na waziri, nani alipwe zaidi?

Njia wasojipatia, vingine kujichumia,
Teni pasenti wasopewa, wala rushwa kugaiwa,
Mtaji wasiokuwa, jasiriamali wakawa,
Daktari na waziri, nani alipwe zaidi?

Nchi wasiojilia, ila wao wanaliwa,
Ukubwa wasiotumia, wengine kunyanyapaa,
Juu wanaowafaa, na chini kusaidia,
Daktari na waziri, nani alipwe zaidi?

Tuesday, January 17, 2012

Pepo kuwa Jehanamu

Pepo iwezayo kua, nchi ikahujumiwa,
Hatimaye kujakuwa, Jehanamu ya dunia ,
Wapo wa kulaumiwa:
Na huwezi kukosea,
Ni fisadi walokuwa,
Na waliowasaidia,
Mengineyo ni hadaa!


Pepo iwezayo kua, nchi ikahujumiwa,
Hatimaye kujakuwa, Jehanamu ya dunia ,
Wapo wa kulaumiwa:
Mamlaka kuibiwa,
Raia walopewa,
Na katiba ilokuwa,
Na wengine kuzomewa!

Pepo iwezayo kua, nchi ikahujumiwa,
Hatimaye kujakuwa, Jehanamu ya dunia ,
Wapo wa kulaumiwa:
Ni wanaojimegea,
Nchi wanayotakiwa,
Vizuri kuiangalia,
Kama shamba la bibi kuwa!

Pepo iwezayo kua, nchi ikahujumiwa,
Hatimaye kujakuwa, Jehanamu ya dunia ,
Wapo wa kulaumiwa:
Wanaojilimbikia,
Kushoto pia kulia,
Wanyonge wanaoonea,
Na vya kwao kuchukua!

Pepo iwezayo kua, nchi ikahujumiwa,
Hatimaye kujakuwa, Jehanamu ya dunia ,
Wapo wa kulaumiwa:
Ni rushwa wanaopokea,
Na matumbo kuwajaa,
Na dola kuwaangalia,
Kama si kuwatetea!

Pepo iwezayo kua, nchi ikahujumiwa,
Hatimaye kujakuwa, Jehanamu ya dunia ,
Wapo wa kulaumiwa:
Wajenzi wasofatia,
Ubora unaotakiwa,
Hadi wanakabidhiwa,
Kibovu kilichokua!


Pepo iwezayo kua, nchi ikahujumiwa,
Hatimaye kujakuwa, Jehanamu ya dunia ,
Wapo wa kulaumiwa:
Posho wanaopokea,
Bila ya kujionea,
Bora walichofanyia,
Umma wa Tanzania!


Pepo iwezayo kua, nchi ikahujumiwa,
Hatimaye kujakuwa, Jehanamu ya dunia ,
Wapo wa kulaumiwa:
Mgeni anayepewa,
Cha wenyeji walokuwa,
Mkubwa akachukua,
Na wenyeji kuibiwa!


Pepo iwezayo kua, nchi ikahujumiwa,
Hatimaye kujakuwa, Jehanamu ya dunia ,
Wapo wa kulaumiwa:
Polisi anayeua,
Aso hatia raia,
Na vyake kuvichukua,
Na kazi kuendelea!

Pepo iwezayo kua, nchi ikahujumiwa,
Hatimaye kujakuwa, Jehanamu ya dunia ,
Wapo wa kulaumiwa:
Mwizi anayetumia,
Mbwa wake kumwibia,
Asokuwa na hatia,
Aibiwaye akafungwa!

Pepo iwezayo kua, nchi ikahujumiwa,
Hatimaye kujakuwa, Jehanamu ya dunia ,
Wapo wa kulaumiwa:
Ni hakimu kupokea,
Amri toka kulikokuwa,
Uamuzi kuutoa,
Haki usiozingatia.


Pepo iwezayo kua, nchi ikahujumiwa,
Hatimaye kujakuwa, Jehanamu ya dunia ,
Wapo wa kulaumiwa:
Tofauti kuzidia,
Baina yake mikoa,
Wengine juu wapaa,
Wengi chini watambaa!


Pepo iwezayo kua, nchi ikahujumiwa,
Hatimaye kujakuwa, Jehanamu ya dunia ,
Wapo wa kulaumiwa:
Umeme kuwa hadaa,
Na ahadi ni sanaa,
Kuigiza yote kuwa,
Sadifu ikapotea!


Pepo iwezayo kua, nchi ikahujumiwa,
Hatimaye kujakuwa, Jehanamu ya dunia ,
Wapo wa kulaumiwa:
Ni maji kuyafukia,
Badala ya kutumia,
Na kiu ikasambaa,
Kila kona Tanzania!

Pepo iwezayo kua, nchi ikahujumiwa,
Hatimaye kujakuwa, Jehanamu ya dunia ,
Wapo wa kulaumiwa:
Rasilimali kuzoa,
Wasiokuwa wazawa,
Katika wao ubia,
Na wakubwa walokuwa!

Pepo iwezayo kua, nchi ikahujumiwa,
Hatimaye kujakuwa, Jehanamu ya dunia ,
Wapo wa kulaumiwa:
Tofauti ikikua,
Kati ya wetu raia,
Masikini muishiwa,
Na tajiri tumbojaa!

Iktisadi

Ikifika ya ahadi, jaribu iktisadi,
Hili lina ushahidi, ataudai Ahadi,
Nawe ukijalikaidi, vinginevyo kujinadi,
Yatakusibu jadidi, yasiyo nawe mradi,
Huyachelea Wadudi, kwa waje wake abdi,
Ila ijapo kubidi, ndio hutoa ahadi!
Na huyu ndiye Maajidi, Mwenye lengo na kusudi,
Usifanze ilimradi, ukakosa tawhidi,
Komalia zake sudi, uje nawe kufaidi,
Bidii nazo juhudi, acha ziwe yetu jadi!

Itihari

ITA wanaokusifu, kilemba ukashonewa,
Uongo watakwambia:
Yumkini huamua, uongo ukitumia,
Dhihaka wakadhania, raia waliokuwa,
Na heshima hufifia, na utu ukapungua.

ITA wanaokusifu, kilemba ukashonewa,
Mazuri watakwambia:
Watayaficha mabaya, usipate kuyajua,
Rangi nje huipakaa, hali ndani kumevia,
Uoza huufukia, marashi wakayatia.

ITA wanaokusifu, kilemba ukashonewa,
Hadithi wataitoa:
Ndefu isiyotulia, na sababu kukwambia,
Na kisha utaamua, kwa uliyosimuliwa,
Abunuwasi ukawa, kila wakikusikiya.

ITA wanaokusifu, kilemba ukashonewa,
Halali watakwambia:
Ufalme umepewa, unaweza kuamua,
Hata mabaya yakiwa, ni budi kuitikiwa,
Dhalimu utaishia, kizazi kikalaaniwa!

ITA wakuzomeao, ya kwao ukasikia,
Ukweli wakakwambia:
Utaweza kuamua, ukweli unaujua,
Ukichemsha twajua, haukuwa nayo nia,
Kila mtu majaliwa, hupewa alojaliwa.

ITA wakuzomeao, ya kwao ukasikia,
Uongo hawatafukia:
Haki watazingatia, na ukweli kukwambia,
Msimamo kubakia, ushahidi kujapewa,
Na utakaloamua, Mola budi nawe kuwa!


ITA wakuzomeao, ya kwao ukasikia,
Mbaya watakutajia:
Unaowategemea, kichinichini hubwia,
Yao wakajifanyia, sio uliyoyaamua,
Haya hujawaumbua, wenyewe kujiondoa!


ITA wakuzomeao, ya kwao ukasikia,
Dhuluma huikataa:
Na mnyonge huridhia, hukumu utayotoa,
Haki ikikutangulia, hauwezi kupotea,
Na hapo ndipo hukaa, Mola anayesifiwa!

Mizigo tunayobeba

IBRA kusaidia, mizigo tunayobeba,
Jamala ukishatoa, panda jengine jaruba,
Hata nao wa kuzaa, waweza fata mraba,
Mizigo tunayobeba, ibra kukusaidia !

Chukua vya kuchukua, bali tija si nasaba,
Wajibu watu kufaa, ndugu pia na swahiba,
Lakini haitokuwa, ni yako kesho akiba,
Mizigo tunayobeba, ibra kukusaidia !

Nii uchafu wa kutoa, pamwe kukoga janaba,
Ili kutolaumiwa, dhahabu ikiwa shaba,
Sahani sio sinia, sembuse kuwa kiroba?
Mizigo tunayobeba, ibra kukusaidia !

Mtoa si mpungukiwa, isihesabu vibaba,
Na mitihani ni njia, huweza fika Kaaba,
Yeye akisharidhia, hakuna wa kukukaba,
Mizigo tunayobeba, ibra kukusaidia !

Nani wa kumtegemea, kuliko yeye HIsaba,
Mrabaha aujua, tena hanayo ghiliba,
Kwani akishaamua, chako chote utabeba,
Mizigo tunayobeba, ibra kukusaidia !

Kwako kinachokufaa, utafute ukuruba,
Kwa ibada nazo dua, na vingine vya mahaba,
Naye hujapendezewa, akakutunza hiba,
Mizigo tunayobeba, ibra kukusaidia !

Sahani naiondoa, ijapo haujashiba,
Nenda wengine kugea, njaa iliyowakaba,
Wewe nikikurudia, kilichobaki kubeba,
Mizigo tunayobeba, ibra kukusaidia !

Nchi ya wanasesere

KATIKA hii dunia, ya wajinga wasojua,
Ya vijinga kujifia, moto visivyochukua,
Ni rahisi kutambua, kwanini tunadidimia,
Nchi ya wanasesere, daima huchezwa shere!

Watu waliolemaa, wasoweza jisomea,
Akili wasiojua, jinsi ya kuzitumia,
Ujinga wanaooa, kisha nao wakazaa,
Nchi ya wanasesere, daima huchezwa shere!

Na wanaotegemea, ya mzungu kuwafaa,
Walokufa kuvumbua, wakabaki kuchimbiwa,
Huna la kutarajia, ila kuja kufukiwa,
Nchi ya wanasesere, daima huchezwa shere!

Pipo wanaoogaiwa, vito wakaviachia,
Shanga wanaopokea, almasi wakatoa,
Na mitumba kuchukua, dhahabu wakaachia,
Nchi ya wanasesere, daima huchezwa shere!

Watu waliojaliwa, bila wao kujijua,
Kwingine wanaohemea, badala chao kutwaa,
Chao wasichojivunia, ila kukishindilia,
Nchi ya wanasesere, daima huchezwa shere!

Wavunao na kutoa, wengine kwenda tumia,
Migumba isiyozaa, wao kinachowafaa,
Huwezi acha kulia, jinsi wasivyojijua,
Nchi ya wanasesere, daima huchezwa shere!

Misingi wasiojua, wapi pa kusimamia,
Nasibu kukadiria, hakika lililokuwa,
Neema wanayoua, na nuksi kuzivaa,
Nchi ya wanasesere, daima huchezwa shere!

Railimali zavia, kwa motisha kupumbaa,
Chao wasichoringia, na ghali kukusudia,
Na ndani wanaojua, ndiko kuanza pafaa,
Nchi ya wanasesere, daima huchezwa shere!

Nchi ya wafao njaa, hali ardhi imejaa,
Ilo asili mbolea, na rutuba ya kumea,
Hila zinazowaumbua, na mikenge kuingia,
Nchi ya wanasesere, daima huchezwa shere!

Watu wasiovumbua, kazi yao kwagizia,
Vijavyo wasobagua, takataka zikajaa,
Wapendao jisifia, kwa sifa za kununua,
Nchi ya wanasesere, daima huchezwa shere!

Nchi ninayoililia, macho bure kuyatoa,
Watu wasiosikia, huku wadhani wajua,
Ufu wanaoupokea, hali hai wamekua,
Nchi ya wanasesere, daima huchezwa shere!

MIzani huzitumia, zilizokwishakataliwa,
Na sheria zenye njaa, uporo zinazopewa,
Mambo hayana kikoa, na udugu hautokuwa,
Nchi ya wanasesere, daima huchezwa shere!

Hila wanaotumia, ya kwao kujipatia,
Vya wengi wanaoua, vya kwao kujichumia,
Akhera wasiojua, na laana wallilia,
Nchi ya wanasesere, daima huchezwa shere!

Kizazi chao huua, kabla hakijazaliwa,
Kwa laana kulaniwa, matumboni kuingia,
Heri kujawakimbia, yatima wanapokua,
Nchi ya wanasesere, daima huchezwa shere!

Ni wanasesere wawa, vingine haitakuwa,
Yanatisha majaliwa, kwao yatakayokuwa,
Toba tusipoitoa, na kuisahihisha njia,
Nchi ya wanasesere, daima huchezwa shere!

Rabana nakulilia, mchana uliokuwa,
Na usiku nao pia, hadi utaponisikia,
Nchi yangu Tanzania, upate kuiongoa,
Nchi ya wanasesere, daima huchezwa shere!

Marafiki kutokuwa

Pengine nimejaliwa, marafiki kutokau,
Ingenipata balaa, na mikosi kuingia,
Ningeweza jizuzua, kufa nikatangulia,
Marafiki kutokuwa, baraka yaweza kuwa!

Roho ningeisumbua, na wakati kupotea,
Hasara nikaingia, bila cha kujivunia,
Fakiri ningelikuwa, pasiwe wa kunijua,
Marafiki kutokuwa, baraka yaweza kuwa!

Nje ungeniumbua, na aibu kuivaa,
Mji nikaukimbia, na shamba kujahamia,
Jina nikalikataa, na lingine kulitwaa,
Marafiki kutokuwa, baraka yaweza kuwa!

Maradhi ungenitia, mwili yakanibomoa,
Watu kuninyanyapaa, ugonjwa wasiojua,
Sinema nikabakia, kizazi kunishangaa,
Marafiki kutokuwa, baraka yaweza kuwa!

Twafunza kwetu kutoa, shukrani ni tabia,
Na kisha kuhimidia, allahamdulillahi pia,
Si wenye kujayua, Mola aliyotupangia,
Marafiki kutokuwa, baraka yaweza kuwa!

Punje moja

Punje moja ukipewa, unaweza kujaliwa,
Hiyo moja kuja kuwa, eflu za magunia,
Na aliyepewa gunia, kitu kutokuambulia,
Punje moja hujazaa, ikazidi elfu moja.

Viumbe hujaribiwa, kwa hayo wanayopewa,
Vipaji huzawadiwa, tofauti vilokua,
Na kila mshikilia, njia hawezi potea,
Punje moja hujazaa, ikazidi elfu moja.

Kila anayejijua, na mpaji kumwazia,
Shukrani akatoa, na Razaki kumwimbia,
Hana kitachopungua, ila tu kuongezewa,
Punje moja hujazaa, ikazidi elfu moja.

Natunza nilichopewa, uzazi sijaujua,
Mughini namlilia, kustawi vikakua,
Na mimi kuhesabiwa, kati ya waliobarikiwa,
Punje moja hujazaa, ikazidi elfu moja.

Pendo ni mwili na roho

KAMA hili hujajua, macho ninakufungua,
Pendo kulikhudumia, likazidi kuchanua,
Mizani kuitumia, ni jambo linalofaa,
Pendo ni mwili na roho, vingine huwa pungufu !

Pendo la mwili likiwa, hufa mwilii ukipoa,
Au ukija lemaa, mwenzio hukukimbia,
Na mzee unapokuwa, hukurithi Changudoa,
Pendo ni mwili na roho, vingine huwa pungufu !

Roho isiporidhia, sudusi vigumu kua,
Huwa wenzi wana ndoa, au ni wenye ubia,
Hili, lile wachangia, siku zikajipitia,
Pendo ni mwili na roho, vingine huwa pungufu !

Tendo mkijifanzia, uchafu mnautoa,
Ila roho ikiwia, ni ibada yatambua,
Muumba huwajalia, mpate cha kujivunia,
Pendo ni mwili na roho, vingine huwa pungufu !

Roho na mwili vikiwa, kitu kimoja mnakuwa,
Ukicheka hatolia, ukiumwa huugua,
Raha yake yako huwa, upendacho hukijua,
Pendo ni mwili na roho, vingine huwa pungufu !

Pendo hili huwa ua, waridi la kuchanua,
Kila siku hunukia, kunyauka kutojua,
Na rangize hubakia, kama lilivyozaliwa,
Pendo ni mwili na roho, vingine huwa pungufu !

Ni libasi huivaa, mme, mke walokuwa,
Nayo huishikilia, hadi kuaga dunia,
Na wengine hukataa, mwingine kujamjua,
Pendo ni mwili na roho, vingine huwa pungufu !

Pendo huwa maridhia, mizani ikitulia,
Roho na mwili vikawa, vitu vilivyo sawia,
Kilele hukifikia, wengi wasiokijua,
Pendo ni mwili na roho, vingine huwa pungufu !

Nistahi Ewe Tawba, watu unayewaongoa,
Dhalili niliyekuwa, amani ndani kujaa,
Na kizazi kufatia, kinachokutegemea,
Pendo ni mwili na roho, vingine huwa pungufu !

Tatizo kabila lako

Na watu niliambiwa, sio watu wa kushika,
Ni wanaokunyenyekea, kwenye yako madaraka,
Juu wakinyanyukia, vya chini huvinyapaa,
Tatizo si lako wewe, tatizo kabila lako.

Mbio zao za mvua, hukaribia masika,
Huwa ni za kubagua, vya kuacha na kushika,
Roho haitoangaliwa, ila unachokishika,
Tatizo si lako wewe, tatizo kabila lako.

Ni watu wa kuwatoa, sio wa kujumlika,
Mioyo hawakupewa, ila bidhaa waweka,
Viumbe wa kutumiwa, hawanayo ya kushika,
Tatizo si lako wewe, tatizo kabila lako.

Ni watu wa kuezua, wachache wa kuezeka,
Ni watu wa kuhamia, kugura bado rauka,
Viumbe wasiojua, kwao kilicho hakika,
Tatizo si lako wewe, tatizo kabila lako.

Si watu wa kuamua, vyema yanayoeleweka,
NI chui wakijivua, juu kilichofunika,
Kondoo humdhania, kumbe jibaba la paka,
Tatizo si lako wewe, tatizo kabila lako.

Si watu wa kutambua, pendo linapopandika,
Huishia ya kulea, na sio ya kuleleka,
Shinikizo huwajia, balaa nayo mizuka,
Tatizo si lako wewe, tatizo kabila lako.

Ni watu wa kubabia, huiba wasiyopika,
Kisha huja kupakua, wajidai wamepika,
Ni chombo cha kutumia, yakiisha huvunjika,
Tatizo si lako wewe, tatizo kabila lako.

Asante kunifungua, macho yaliyofungika,
Nililchodhania chang'aa, kumbe jaa lakunuka,
Shukrani kwepushiwa, wala sintosikitika,
Tatizo si lako wewe, tatizo kabila lako.

WAJINGA KUWAACHIA

Mahitaji ya msingi,
Hamsini kutimia,
Watu wetu bado wengi,
Kukosa watahiniwa?
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!


Usanii wazidia,
Iliyo sanaa mbaya,
Vipi ukiangalia,
Akili hutoijua:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Maji yameshapotea,
Miji yote ilokuwa,
Visingizio kadhaa,
Viongozi huvitoa:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Nyumba haki yake mtu,
Roho zetu bado kutu,
Twaona kwenye misitu,
Wanafaa kutupiwa:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Vijiji vinasinyaa,
Hali mali vingekuwa,
Nchi kuiingizia,
Milioni zilokuwa:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Ugumu sijaujua,
Ila usanii wawa,
Wangelijipunguzia,
Haya yangelitokea:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Wakubwa wataka shiba,
Kwa wadogo kuwakaba,
Njaa zinawaziriba,
Muhali kuendelea:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Umeme wanawakaba,
Koo waliokwishakabwa,
Umeme au ubwabwa,
Maamuzi sasa kuwa:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!


Hamsini yatimia,
Ni tano asilimia,
Umeme inayopewa,
Tena kwa kusuasua:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!


Kwengine ingelikuwa,
Nchi nzima ingekuwa,
Bei zikajishukia,
Nuru kuwa Tanzania:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Reli ninawaambia,
Ni shule kuifungua,
Profesa wa Ulaya,
Wasokazi kutumia:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Vijana kujitolea,
Posho wakachangiwa,
Huku kisomo wapewa,
Reli tutazifufua:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Ruia wanazootea,
Za kitajiri tambua,
Na hawa nawaambia,
Kwao tutanyong'onyea:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Wao wanafikiria,
Trilioni kumwaa,
Katu hazitoingia,
Njiani zitaishia:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!


Na hata zikiingia,
Wengine zitawafaa,
Na nchi ikalemaa,
Kama si nyuma kuvia:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Barabara nazo pia,
Twaweza kujipatia,
Shule zikiandaliwa,
Elimu kazi ikawa:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Hatuwezi endelea,
Wengine kutegemea,
Mweupe wa kumwangalia,
Mweusi haitokuwa:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Weupe wamezidiwa,
Ndugu wanawaangalia,
Kwao kinachobakia,
Wenyewe wakitumia:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Kwanza ninawashangaa,
Madini kuyaachia,
Kisha kujakupokea,
Vijisenti vilivyokuwa:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Kama babu mmekua,
Mjerumani kumwachia,
Mali kubwa zilokuwa,
Kwa kupewa lawalawa?
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!


Madaraja nayo pia,
Na viwanja vya kufaa,
Michezo iliyokuwa,
Hadi tukajichumia:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Sindano ya Tan zania,
Ingali inatakiwa,
Aibu kuinunua,
Toka nje ya Afrika:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Mbona mnatembea,
Na Ulaya kuingia,
Vipi mnapofuliwa,
Ujanja kutoujua?
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Pampu mwaagizia,
Mbovu ziliziokuwa,
Na hasara kuingia,
Kila mwaka kwa mamia:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Msumbiji wachipua,
Wareno kuwatumia,
Kwao wasioajiriwa,
Sasa wajitengenezea:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!


Hata uzi na samani,
Zijetoka Marekani,
Huu si uhayawani,
Aibu pia fedheha?
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Meli mmeshaazimia,
Makaburi kuchukua,
Paseni kuichukua,
Baharini kuzikiwa:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Hadhi mmeshaamua,
Mitumba inatufaa,
Uhai si manufaa,
Wingi mnaukataa:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Ndege mmeazimia,
Mitumba kuzichukua,
Mbayuwayu akitua,
Nasi chini tuje tua:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Trekta mwatapeliwa,
Bei mbaya mwanunua,
Badala kujitengezea,
Imara zilizokuwa:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Mabasi tukiamua,
Si kioja yote kuwa,
Yatengenezwa Tanzania,
Mafundi wazidi jaa;
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Malori nayo pia,
Babu alishaaisisia,
Kutengezwa Scania,
Hapa kwetu Tanzania:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!


Mafundi wazidi jaa,
Ulaya walikozaliwa,
Kazi zimewakimbia,
Riziki wajisakia:
Mashaveli kumjua, hata mimi huchukua,
Rahisi vilivyokuwa, magumu kujitia,
Tukayashughulikia, utata yaliyokuwa,
Hutamani kujitoa, katika hii dunia:
Wajinga kuwaachia!

Januari Ikifika

Elimu sasa sokoni, bajeti yahitajika,
Mwaka huisha taabani, mwanzo wafilisika,
Ila wenye tumaini, pahala wanaposhika,
Januari ikifika, huwa mshikemshike!

Chekechea wamo ndani, fedha inahitajika,
Na msingi kitalini, mikono imenyanyuka,
Sekondari yumkini, nao watingishika,
Januari ikifika, huwa mshikemshike!

Wakiwemo wa Chuoni, na mkopo warauka,
Huwa tena mashakani, mkopo usiposhika,
Huingia akibani, au rehani kuweka,
Januari ikifika, huwa mshikemshike!

Mameneja mashuleni, wenzenu twataabika,
Hebu mpango fanyeni, tarehe zikaachika,
Mbalimbali kubaini, fedha ikagawanyika,
Januari ikifika, huwa mshikemshike!

Katikati naamini, bora kuliko mwanzoni,
Aidha nako mwishoni, sio pa kupaamini,
Nafuu hapo tupeni, tusiwe ovyo nyumbani,
Januari ikifika, huwa mshikemshike!

Mke gani umuoe?

Utaoa mke gani, swali umeniuliza,
Awe kwako afueni, akili kukutuliza,
Atayekupa hisani, na daima kukutunza,
Nami mwana nakwambia, bila yoyote ajizi:


Oa aliyelelewea,
Hakika akaleleka,
Adabu anayejua,
Na utu kukamilika!

Oa anayemjua,
Muumba wake Rabuka,
Dini anayeijua,
Na ibada kuzishika!

Oa asiye udhia,
Rahisi wa kuchafuka,
Kinyaa anayejaa,
Ashindwe kutazamika!

Oa aliyejaliwa,
Ubongo kukamilika,
Na akili nazo kua,
Kizazi chema kutoka!

Oa asiye bandia,
Ovyo anayetumika,
Wakubwa kukusaidia,
Waezua, waezeka!

Oa aliye radhia,
Pendo aliyelishika,
Kasoro usiyemjua,
Na nuksi kuziruka!

Oa asiyesumbua,
Kwa kelele kumtaka,
Sauti anayetoa,
Hata punda kumcheka!

Oa alyemegewa,
Ya Urulaini hakika,
Wimbo anayekwimbia,
Kwa kila analotamka!

Oa sura asokuwa,
Lakini mali asaka,
Na yako inapokuwa,
Kwake iwe yatunzika!

Oa asiyekulewa,
Na tunzo akizishika,
Staha anayeijua,
Wapi pakukanyagika!

Oa asiyezitoa,
Siri zilizofichika,
Watu kuwasimulia,
Hata wasiohusika!

Oa msafi wa nia,
Uoza asiyeshika,
Marashi akijitia,
Akupandishe Mizuka!

Oa asiyejitia,
Uzungu na Uamerika,
Nguo anayezivaa,
Mapaja zisofunika!

Ila nawe watakiwa,
Katakei kutoweka,
Ni utumwa wajitia,
Kwa watumwa Amerika!

Oa asiyeonea,
Wanyonge na malaika,
Yatima anayelea,
Kama wake kutunzika!

Oa anayetambua,
Uzee utapofika,
Wazazi atawalea,
Hadi wafe waridhika!

Oa shoo asokuwa,
Majiani kujiweka,
Njiani kiguu na njia,
Kaziye kujianika!

Oa anayevumilia,
Yote yatayomfika,
Asiye na mazoea,
Ya watu kutamanika!

Oa anayeamua,
Na mipango kupangika,
Pasiwe ombwe kutua,
Nyumbani pakachafuka!

Oa anayewalea,
Wana wakaelimika,
Lukmnani kumjua,
Na yake akayashika!

Oa asiyekulia,
Wewe unapojicheka,
Oa anayekujua,
Pasiwe na kufichika!

Oa unayemuoa,
Roho na mwili kushika,
Kitu kimoya mkawa,
Yenu yote ya hakika!

Oa mwana majaliwa,
Libasi mkajishika,
Mjipambe kwa hatua,
Na kizazi kukidaka!

Oa wana wakajua,
Watu wema wazalika,
Na Mungu wakimjua,
Yao hujarehemeka!

Oa wasiotumiwa,
Na mtu au mahoka,
Ovyo wasiochezewa,
Na chama au vibaka!

Oa wasiolegea,
Ukubwa kuja ushika,
Wanaojitafutia,
Wenyewe wakajiweka!

Oa wasio balaa,
Watu watakaokucheka,
Uonekane Kinyaa,
Mchamungu wa hakika!

Oa wasio na njaa,
Lolote likakubalika,
Wajaokujiachia,
Kwako ikawa mashaka!

Oa waliotulia,
Wenye mwendo wa hakika,
Yakini wanaojua,
Haraka haina baraka!

Oa si kwa kuchagua,
Kizazi anachotoka,
Ila kwa kutambua,
Wema aliyezalika!

Oa si alichopewa,
Tajiri alozalika,
Oa kwa kutambua,
Nanyi mtatajirika!

Oa si kama sanaa,
Televisheni kutoka,
Oa yatakayofatia,
Vyema yakaandalika!

Oa hata kimyakimya,
Bila sherehe mwafaka,
Watosha kuangalia,
Kwao mliozalika!

Oa mlichochangia,
Kwa heri kikatumika,
Yatima kuwaendea,
Hali ikabadilika!

Oa kwa kunyanyua,
Mikono zije baraka,
Na sujuda kuitia,
Mmtangulze Rabuka!

Saturday, January 14, 2012

Kitu gani watufaa ?

Labda stima kupaa, na bei juu kuwa,
Kisha na kila bidhaa, ghali sana kununua,
Watu wenda wakilia, nani wa kuwasikiya ?
Kitu gani watufaa, viongozi watalii?

Ajabu wanaotembea, mengi wakajionea,
Hawana wanalotwaa, japo ikawa sanaa,
Waje kuliigizia, nyumbani wakirejea,
Kitu gani watufaa, viongozi watalii?

Machoni tukiyatia, twaweza igilizia,
Na sisi kujiundia, chetu kitakachotufaa,
Hurudi tena kimya, mabegi yao yajaa,
Kitu gani watufaa, viongozi watalii?

Hebu sasa angalia, Keko wanapoingia,
Mjasiriamali raia, waendapo kumvaa,
Mizani kajiundia, wao wamezikataa,
Kitu gani watufaa, viongozi watalii?

Sasa wamshtakia, viwango havijafaa,
Ndani kumsukumia, badala kumsaidia,
Huo sio ukichaa, watu tunaokataa?
Kitu gani watufaa, viongozi watalii?

Hawayajui Korea, zamani yaliyotokea,
Trekta kujiundia, rivasi gia zikawa,
Ila walishangilia, kwa yao kujiundia,
Kitu gani watufaa, viongozi watalii?

Kuvumbua si kukaa, ofisini kupepewa,
Viyoyozi mwatumia, kurepea mwaishiwa,
Hii ya kwenu tabia, nawaambia ni balaa,
Kitu gani watufaa, viongozi watalii?

Rushwa huwa wachukua, maofisa walokua,
Matajiri kuachiwa, nje wakaagizia,
Na uvumbuzi kuua, wa nyumbani ukichipua,
Kitu gani watufaa, viongozi watalii?

Yetu tusipotumia, hata kasoro zikiwa,
Tubaki twakimbilia, nje vinvyotokea,
Mbali hatutafikia, njiani tutaishia,
Kitu gani watufaa, viongozi watalii?

Viongozi twaambia, watalii walokuwa,
Basi hapa mkirejea, njooni na ya kujiundia,
Vinginevyo mtakua, mwaiua Tanzania!
Kitu gani watufaa, viongozi watalii?

Yao hayawezi dumu

Wa Adi walijaliwa, makubwa kujifanzia,
Na Thamudi nao pia, nyuma hawakubakia,
Hadi walipopotea, wenyewe wakajisifia,
Mungu asiowapenda, yao hayawezi dumu!

Hadi walipopotea, wenyewe wakajisifia,
Na muumba kumtania, madhambi kujipalia,
Kufuru walipozaa, juu walinyanyuliwa,
Mungu asiowapenda, yao hayawezi dumu!

Na chini walipotua, hakuna aliyebakia,
Sauli naye alipewa, akawa ajifikiria,
Wengine kuwatendea, kisichostahilia,
Mungu asiowapenda, yao hayawezi dumu!

Akaonywa hakusikia, Bwana akamsanzua,
Daudi kumchagua, Nabii na dola kutwaa,
Na leo tunajionea, haya waliopugukiwa,
Mungu asiowapenda, yao hayawezi dumu!

Mbwani twajifanyia, Mola anayochukia,
Na ujanja twajitia, kama yeye hatajua,
Huu ujinga tanzia, kujinyonga twaamua,
Mungu asiowapenda, yao hayawezi dumu!

Nadhikiri kuwaambia, badilisheni tabia,
Yaja yakuenguliwa, na mengine mabalaa,
Huruma kuwakimbia, na hasara kuingia,
Mungu asiowapenda, yao hayawezi dumu!

Viongozi bangaiza

Historia huua, ya kwao kuyafichiza,
Viogozi walokua, kazi wanabangaiza,
Hawarithi mapokeo, kila kitu hutekeza,
Viongozi bangaiza, historia huua !

Wizara wakichukua, kazi upya huanza,
Na idara kufatia, kumbukumbu hupoteza,
Kisa kilichosanzuliwa, wengine kutofatiza,
Viongozi bangaiza, historia huua !

Hizi zama za balaa, uovu watu wawaza,
Vyama vilivyofulia, au laana kuapizwa,
Huwa navyo vyaingia, na kisha vikateleza,
Viongozi bangaiza, historia huua !

Uongozi si sanaa, wala ploti kuigiza,
Huwaza na kuwazua, watu kukusikiliza,
Vinginevyo huwa ndoo, na maji kuyamwagiza,
Viongozi bangaiza, historia huua !

Hii ngoma ya majaa, sio uganga wa pweza,
Na tambo wanaozua, ni vigumu kuicheza,
Huishia kutitia, wawe kwa wengi kikwazo,
Viongozi bangaiza, historia huua !

Wacha wale raha

Wacha wale raha leo, kesho watalia sana,
Maisha kama mgao, na watu hupokezana,
Ni wachache wajuao, neema zisizosana,
Wacha wale raha ndogo, kesho watakonda sana !

Hadithi na mapokeo, haya yameona sana,
Na dunia kama chuo, weledi si wengi sana,
Na mambo yawapitayo, huja mwishoni kuona,
Wacha wale raha ndogo, kesho watakonda sana !

Wa Pwani kwenye mwambao, bahari husema sana,
Kungwi na wawaleao, kwao yanajulikana,
Na vyungu wainjikao, sio hao wabebao,
Wacha wale raha ndogo, kesho watakonda sana !

Mambo yataka tambuo, utotoni na ujana,
Wazazi waelewao, haya huwafunza wana,
Wasio wakati nao, hubaki wakapishana,
Wacha wale raha ndogo, kesho watakonda sana !

Na watenzi wajuao, tungo zao za maana,
Husema maneno hayo, na kuandika kwa kina,
Ila ni wajaliwao, huweza kuja yaona,
Wacha wale raha ndogo, kesho watakonda sana !

Umeme tunaibiwa?

Viongozi kuamua, kirahisi kuridhia,
Mashaka yananijaa, uwezo waliojaliwa,
Naona hii nazaa, uchumi tutatuua,
Umeme tunaibiwa?



Ukiritimba kuzaa, uoza uliokuwa,
Na chama kutuibia, kia kilichoingia,
Si chanzo kilichokua, hapa tulipofikia?
Umeme tunaibiwa?

Mameneja wasofa, na nchi kuajiriwa,
Mbumbumbu wa tasnia, zuzu wa teknolojia,
Kisha tunawaachia, spidi kukanyagia?
Umeme tunaibiwa?

Watumishi walojaa, tena pia wasofaa,
Shirika walipania, kama ng'ombe wa maziwa,
Kila siku kukamua, hata na damu ikiwa,
Umeme tunaibiwa?

Mijini tunalaliwa, vijijini waambaa,
Iweje asilimia, ndogo hivi ilokuwa,
Mzigo kuuchukua, na tuje kuendelea?
Umeme tunaibiwa?

Viongozi twahofia, njia wameshapotea,
VIchakani waingia, kwenye miba na balaa,
Nani wa kutuokoa, shari ikituvamia?
Umeme tunaibiwa?

Mameneja watakiwa, magwiji wa tasnia,
Watoke hata Ulaya, shirika kusimamia,
Mapfofesa wamejaa, na mafundi kwa gunia,
Umeme tunaibiwa?

Wengine waajiriwa, vibarua walokua,
Menijementi kung'aa, maamuzi kuzubaa,
Na ndugu wanaajiriwa, kwa kazi wasizojua,
Umeme tunaibiwa?

Ya babu teknolojia, ndiyo wanayotumia,
Teknohama yawia, vigumu kuielwa,
Vibovu wananunua, vyenyewe vyajiozea,
Umeme tunaibiwa?

Amerika na Ulaya, kazi zimeshapotea,
Nyumbani wanakaa, na umeme wanajua,
Ndioho walichosomea, na kulala walalia,
Umeme tunaibiwa?

Akili tungejaliwa, huko tungewafatia,
Kuzungumza kwa nia, na nchini kuwavutia,
Kwa ajira kuwatwaa, kuwekeza nako pia,
Umeme tunaibiwa?

Si Dowans kuwagawiwa, kitu wasiojipandania,
Huu uwizi twalia, nchi kwa hivi twaua,
Na wanyongaji twajua, ni nani waliokua,
Umeme tunaibiwa?

Muundo unaotumiwa, tayari umefubaa,
Shirika budi kugawa, kuwa nayo ya mkoa,
Haya ushindani kuwa, wateja kupigania,
Umeme tunaibiwa?

Ukubwa kuulilia, siyo tuliyojaliwa,
Kipaj hatukupewa, makubwa kuyajulia,
Akili zimesinyaa, ni vidogo kuvilea,
Umeme tunaibiwa?

Mifumu tumefumua, na siasa kuzitia,
Wajuzi tunawatoa, na mangimeza kutia,
Kipi kitaendelea, kuwepo wasiojua?
Umeme tunaibiwa?

OVATAIMU BALAA, NI MCHEZO UMEKUA,
KAZI YA LIMOJA SAA, SIKU NZIMA HUCHUKUA,
HAZINA YAHUJUMIWA, SISI TUNAANGALIA?
Umeme tunaibiwa?

Mikataba walotia, sisi kujadhulumiwa,
Tungali tuanwatetea, na ujanja kuutumia,
Ili kuwazawadiwa, cha mbele tulichotwaa,
Umeme tunaibiwa?

Nchi washikilia, nani atawaingia,
Hatua kuzichukua, na kuilipa fidia,
Mnyonge araruliwa, nasi tunaangalia?
Umeme tunaibiwa?

Maamuzi twagugumia, chini chini twatambaa,
Uzaini twaingia, wananchi kuwaibia,
Siasa tumepungukiwa, ni ujinga tunatumia,
Umeme tunaibiwa?

Manunuzi twaibia, na invoisi kujaa,
Upepo vilivyokuwa, ndani havitoingia,
Mdhibiti kalemaa, ndani hatojionea,
Umeme tunaibiwa?

Mnyonge budi kulia, kwa ninavyodhulumiwa,
Sina linaloingia, bila ya kuchukuliwa,
Mizigo naongezewa, hadi sasa natambaa,
Umeme tunaibiwa?

Friday, January 13, 2012

Siombi kitu zaidi

MIMI ni wako Abdi, yako nayaitikia,
Nakutambua Ahadi, mmoja uliyekua,
Nami daima abadi, budi kukutumikia,
Siombi kitu zaidi, unachonikadiria !

Nkkuze niwe shahidi, siku ya kushuhudia,
Haki nikaifaidi, kwa ulimi wa murua,
Hakika iwe ni jadi, kizazi nikijaliwa,
Siombi kitu zaidi, unachonikadiria !

Nitangulize uradi, hadi siku ya ahadi,
Na nisiwe mkaidi, ikinipasa sajidi,
Na unipande mdadi, kwa jina kulihimidi,
Siombi kitu zaidi, unachonikadiria !

Nipe wepesi wa radi, katika ya tawhidi,
Nijalie niwe badi, mwepesi kutaradadi,
Bidii nayo juhudi, kwa uzuzi na kuakidi,
Siombi kitu zaidi, unachonikadiria !

Nakuhimidi Wadudi, daima si maulidi,
Na siingojei Idi, kwa tabaraki hadidi,
Waniitao gaidi, upofu iwe ahadi,
Siombi kitu zaidi, unachonikadiria !

Niwe katikati budi, ya joto na ubaridi,
Nisiombe la zaidi, ukisha kuniahidi,
Iwe ni ya kwangu sudi, kupata bila idadi,
Siombi kitu zaidi, unachonikadiria !

Nitunze umaridadi, wa nafsi zumaridi,
Uwe kiongozi Hadi, tena rafiki rashidi,
Nikuitapo Swamadi, Malaika waninadi,
Siombi kitu zaidi, unachonikadiria !

Maajidi na Wajidi, niepushe na hasadi,
Na wachawi wa miradi, njiani wanaojinadi,
Na wewe kama Wahidi, kwako niwe ni waridi,

Mitume waso idadi, ibada iwe zawadi,
Inyooshe fuadi, sala ziwe makusudi,
Na masharifu jadidi, uwape yao mihadi,
Siombi kitu zaidi, unachonikadiria !

Waislamu wazidi, shetani kumkaidi,
Uwape yao Mubidi, wapende kwako kurudi,
Iwe ni zao nakidi, mazuri kukuahidi,
Siombi kitu zaidi, unachonikadiria !

Uwape kubwa juhudi, kwa elimu na zaidi,
Na waache kuritadi, kidini kwa ufisadi,
Kuifia ikibidi, hili wapae ahidi,
Siombi kitu zaidi, unachonikadiria !

Patiliza makuwadi, dini wasiiiritadi,
Wenye majina mamedi, wasiwe wenye ugwadi,
Idi wasio idadi, dini wasiikaidi,
Siombi kitu zaidi, unachonikadiria !

Viongozi magumashi

Viongozi magumashi, ni wazuri kwa nakshi,
Ila siwajumlishi,kwenye bora matamshi,
Kazi yao ushawishi, japo nyama washiwashi,
Nitabakia mshashi, kwa kazi ya pushipushi!

Wapendeza kwa ucheshi, ila hawana upishi,
Wapikacho matapishi, na hili sio uzushi,
Husema hawapandishi, lakini hawateremshi,
Nitabakia mshashi, kwa kazi ya pushipushi!

Ni wazuri matoashi, na nafasi haitoshi,
Ila sio waanzilshi, kwa yenye utamanishi,
Kawaida ni wabishi,na makisha hawashushi,
Nitabakia mshashi, kwa kazi ya pushipushi!

Daima walazimishi, na kisha walalamishi,
Fikra zao kijeshi, kukokota wasoishi,
Na ya kwao madishi, ya umma hayaonyeshi,
Nitabakia mshashi kwa kazi ya pushipushi!

Kushushua ni watashi, na kuzomea uashi,
Wakkipewa bakshishi, kila kitu ni ucheshi,
Hawanuni kwa tapishi, kwao ulaji na nyweeshi,
Nitabakia mshashi kwa kazi ya pushipushi!

Vigelegele wazushi, hata palipo mazishi,
Ni mizigo huishushi, wakubwa hawabakishi,
Ni mswaki na burashi, ndipo menu huwa freshi,
Nitabakia mshashi kwa kazi ya pushipushi!

Mengi ni mafurushi, ndani kitu hakiishi,
Ni garasha na mijeshi, hutembea na beleshi,
Na yao hayenda joshi, kwani sio waendeshi,
Nitabakia mshashi kwa kazi ya pushipushi!

Wengine hawaharishi, kinyesi bali matusi,
Tabia yao uzushi, daima hawana utashi,
Huishi kama waishi, kumbe ya watu madishi,
Nitabakia mshashi kwa kazi ya pushipushi!

Huona ya wote poshi, na mengine hatarishi,
Wa Mtwara hadi Moshi, wajua wanavyoishi,
Ulaya hapawatoshi, kwa milo na bakshishi,
Nitabakia mshashi, kwa kazi ya pushipushi!

Hali kwetu ni mazishi, na matatizo hayeshi,
Haviishi vifurushi, vya zawadi na mapishi,
Hugongana matarishi, ajabu hawaangushi,
Nitabakia mshashi, kwa kazi ya pushipushi!

Watu hutaka kuishi, na kuwa kama arshi,
Ukubwa hauzeeshi, neema virutubishi,
Hili halina ubishi, shaibu bado waishi,
Nitabakia mshashi, kwa kazi ya pushipushi!

Hamsini haitoshi, maisha tunayoishi,
Huyakwepa mazamishi, na kuchelewesha mazishi,
Hili hawababaishi, wamejaa magumashi,
Nitabakia mshashi, kwa kazi ya pushipushi!

Wanaosha hawaoshwi, hawajui matamshi,
Ni harusi si mazishi, mengine waweza gushi,
Wekeza yao uashi, na kutuma waandishi,
Nitabakia mshashi, kwa kazi ya pushipushi!

Tarafu haiwachoshi, hugeuzwa king'arishi,
Wana walio wabishi, watakao wasiishi,
Huishia na hashishi, madawa navyo vimoshi,
Nitabakia mshashi, kwa kazi ya pushipushi!

Refu sana garimoshi, ila kungoja hukeshi,
Hayazeeki marashi, ila kwenye matapishi,
Naishi kama siishi, ila hawanitamanishi,
Nitabakia mshashi, kwa kazi ya pushipushi!

Ni nani wa kumwogopa

Nitamwogopa mtu gani, kama Mola yuko nami,
Nani ni mwenye mizani, awezaye kunihami,
Nani ni mwenye hisani, asiye nao umimi?
Ni nani wa kumwogopa, kama Mola niko naye?

Huyu siye tu Manani, bali ni wa kwangu Ami,
Nikiwepo duniani, wa kwanza kwenye ulimi,
Naomba yake auni, kuchunga wangu usemi,
Ni nani wa kumwogopa, kama Mola niko naye?

Na kama nikiwa mgeni, Uturuki na Ajemi,
Naomba yake ihsani, aniepushe na watemi,
Nuru iwepo mbeleni, na nyuma ikinihami,
Ni nani wa kumwogopa, kama Mola niko naye?

Nuru iwepo usoni, kuiepuka jahimi,
Kadhalika na machoni, uoni uwe wa lami,
Naye bila kusaini, iwe kitu sikifumi,
Ni nani wa kumwogopa, kama Mola niko naye?

Nikuze yangu imani, katika hii jamii,
Upole na umakini, ujaze wangu ulimi,
Katika feli na kani, pasiwe kitu sipimi,
Ni nani wa kumwogopa, kama Mola niko naye?

Kama Mola niko naye

Nitamwogopa mtu gani, kama Mola yuko nami,
Nani ni mwenye mizani, awezaye kunihami,
Nani ni mwenye hisani, asiye nao umimi?
Kama Mola niko naye, ni nani nitamwogopa?

Huyu siye tu Manani, bali ni wa kwangu Ami,
Nikiwepo duniani, wa kwanza kwenye ulimi,
Naomba yake auni, kuchunga wangu usemi,
Kama Mola niko naye, ni nani nitamwogopa?

Na kama nikiwa mgeni, Uturuki na Ajemi,
Naomba yake ihsani, aniepushe na watemi,
Nuru iwepo mbeleni, na nyuma ikinihami,
Kama Mola niko naye, ni nani nitamwogopa?

Nuru iwepo usoni, kuiepuka jahimi,
Kadhalika na machoni, uoni uwe wa lami,
Naye bila kusaini, iwe kitu sikifumi,
Kama Mola niko naye, ni nani nitamwogopa?

Nikuze yangu imani, katika hii jamii,
Upole na umakini, ujaze wangu ulimi,
Katika feli na kani, pasiwe kitu sipimi,
Kama Mola niko naye, ni nani nitamwogopa?

Waungwana huungana

Waungwana lao moja, si watu wa kuumana,
Ya kwao hupanga hoja, ya wengi kuwa maana,
Akili kosa kufuja, kila ana la kunena,
Waungwana huungana, sio wanaogombana.

Huiepuka mirija, na hula wanachovuna,
Wananchi 'kuwangeleja', hilo kwao si amana,
Nao hujifunga mkaja, hali ngumu wakiiona,
Waungwana huungana, sio wanaogombana.

Na Juja na Maajuja, watawasoma kwa kina,
Huijua ngojangoja, matumbo huumizana,
Tarehe budi kutaja, na mamboye kufanana,
Waungwana huungana, sio wanaogombana.

Wanaostahili koja, afu huafikiana,
Ukubwa sio daraja, ila nafuu kuona,
Watufanyao mateja, lazima kufukuzana,
Waungwana huungana, sio wanaogombana.

Huzitamka lahaja, lugha zinapoumana,
Na watu huwa wamoja, japo wanatofautiana,
Watafute lenye tija, dunia kutulizana,
Waungwana huungana, sio wanaogombana.

Huitafuta siraja, dhiki zinapopandana,
Na mujibu utskuja, na watu wakafaana,
Mwenye shida huitaja, haja tukatimiziana,
Waungwana huungana, sio wanaogombana.

Tanganyika na Unguja, yabidi kuhimizana,
Watu wataka faraja, na sio kutafutana,
Ibakie kwenda hija, uchumi unapofana,
Waungwana huungana, sio wanaogombana.

Jina lako kulitaja, nafuu hupatikana,
Hutowakwaza waseja, yao yakawa amina,
Chimbuko lake faraja, kwako linapatikana,
Waungwana huungana, sio wanaogombana.