Wednesday, November 30, 2011

Haujaja

Mwenzio nilikungoja, usingizi haukuja,
Uliponiambia waja, nikasubiri kwa haja,
Umbeya kuubwabwaja,na maneno kuyafuja,
Uliniambia waja, mbona mwaya haujaja!

Uliogopa kufuja, vijisenti vya mseja,
Ujumbe niliungoja, simu ikaisha chaja,
Ikaondoka faraja, kwani wewe haujaja,
Uliniambia waja, mbona mwaya haujaja!

Linanisha daraja, kuvuka imesha haja,
Mie si mtu wa kungoja, kama vile kuna hoja,
Sipendi muda kufuja,majukumu yaningoja,
Uliniambia waja, mbona mwaya haujaja!

Pendo halijawa tija, kusubiri bila hoja,
Ningeliufunga mkaja,ningelipata mrija,
Soda nisingeifuja, ningeinywa kwa lahaja,
Uliniambia waja, mbona mwaya haujaja!

Darasa halidurusi

Darasa letu nuhusi, mambo yake w asiwasi,
Kalivaa ibilisi, kila kitu ni yabisi,
Maneno kama kamasi, na mafua ya utosi,
Darasa halidurusi, fikra zina nakisi!

Darasa Abunuwasi, mapya haliasisi,
Limejaa ubinafsi, ya umma kwao mkosi,
Wote wake waasisi, dhehebu wameliasi,
Darasa halidurusi, fikra zina nakisi!

Kawajaa ibilisi, dahari watanafusi,
Hawataki ufuasi, wa mauti kuwahisi,
Wataka ishi fususi, iwe radhi ya Qudusi,
Darasa halidurusi, fikra zina nakisi!

Awadanganya muasi, atawavisha libasi,
Iwe kwao majilisi, dunia isiwatusi,
Waishi yao kiasi, kiongozi ibiisi,
Darasa halidurusi, fikra zina nakisi!

Naona kuna nakisi, na hili wanalifosi,
Hajatokea msusi, hili akaja liasi,
Kufa kwetu mahsusi, kuishi si yetu chunusi,
Darasa halidurusi, fikra zina nakisi!

Nakiondoa kifusi, msiwe na wasiwasi,
Maisha si almasi, ardhi kuwa damisi,
Iishi bila anasi, milele ikatulia,
Darasa halidurusi, fikra zina nakisi!

Mkopo kapewa nani

Mwenye dhiki sijapewa, mkopo kapewa nani,
Redioni nasikia, wametwaa bilioni ,
Denda nikalitoa, na kujaa tumaini,
Mkopo kapewa nani, mwenye dhiki sijapewa?

Majina kuyasikia, zikanichafuka mboni,
NI wakubwa walokua, na nyumba za uani,
Fukara sijasikia, nikadhani ni utani,
Mkopo kapewa nani, mwenye dhiki sijapewa?

Anyang'anywa asokua, alopewa hazinani,
Miguu juu ikawa, kichwa kikaenda chini,
Haya yanaendelea, dawa sijaibaini,
Mkopo kapewa nani, mwenye dhiki sijapewa?

Wadai wanaojua, hakopeshwi masikini,
Tajiri akichukua, mnakua si shakani,
Maskini akipewa, kurudisha yumkini,
Mkopo kapewa nani, mwenye dhiki sijapewa?

Shule haina elimu

Hapa si mastakimu, inafaa kutambua,
Watu wasio adhimu, vingine hupadhania,
Wakajitia muhimu, daima kujizuzua,
Shule haina elimu, nani ataisomesha?

Na nilipotakadamu, hili nikaligundua,
Shule haina elimu, nani ataipatia,
Haipo yake kasimu, nani kuyagharamia,
Shule haina elimu, nani ataisomesha?

Ujinga kweli ni sumu, na wengi inshawaua,
Wengi wanajituhumu, badala ya kutuhumiwa,
Ubongo bila ya damu, muhali kufikiria,
Shule haina elimu, nani ataisomesha?

Wachache wanaofahamu, ni wengi wasiojua,
Na mengi kwetu haramu, ila tunayatumia,
Ni muhali wa kukimu, adhana isipokua,
Shule haina elimu, nani ataisomesha?

Niliwauliza wa Lamu, Fumo Lyongo akiwa,
Wanipe zao salamu, ufumbuzi kuujua,
Hawajaenda Kiamu, jibu hawajalitua,
Shule haina elimu, nani ataisomesha?

Nimeshakata tamaa

Tamaa imepotea, wengine nawaachia,
Labda kuwasaidia, usia najiandikia,
Muda ukijafikia, malengo kujifichua,
Nimeshakata tamaa, kazi kwa kizazi kipya!

La kwanza kuwaambia, dira imepinduliwa,
Vyama vimechukuliwa, na watu wenye tamaa,
Ukubwa wanauwania, na kazi hawajaijua,
Nimeshakata tamaa, kazi kwa kizazi kipya!

Waingia maharamia, wafuasi watolewa,
Sasa walioshikilia, mradi umeshakua,
Yao wanaazimia, ya wananchi wazimia,
Nimeshakata tamaa, kazi kwa kizazi kipya!

Wakubwa wanajifua, wanyonge wanafulia,
Shilingi inatitia, dola yazidi kupaa,
Bei zazidi kukwea, na lishe yadidimia,
Nimeshakata tamaa, kazi kwa kizazi kipya!

Mzee nimeshakua, ni yanini kukomaa,
Wanaotufuatia, mapambano kwendelea,
Ushauri nitatoa, watakaponiambia,
Nimeshakata tamaa, kazi kwa kizazi kipya!

Tungo wakijisomea, mengi pia kuyajua,
Wapi tulipopotea, porini tukaingia,
Nani wa kulaumiwa, mwema aliyedhaniwa,
Nimeshakata tamaa, kazi kwa kizazi kipya!

Mola tunamuombea, apange kumuumbua,
Wote tuje kumjua, awe kwenye historia,
Vizazi kumzomea, na moto kumwombea,
Nimeshakata tamaa, kazi kwa kizazi kipya!

Kituo cha afya hoi

Kituo kiko taabani, homa inakisumbua,
Daktari wake nani, aje kukiangalia,
Nyuzize ni hamsini, joto limeparamia,
Kituo cha afya hoi, daktari wake nani?

Malaria yumkini, maradhi tunahofia,
Isije enda kichwani, mgonjwa awe kichaa,
Tutakuwa mashakani, akianza kukimbia,
Kituo cha afya hoi, daktari wake nani?

Nesi hawaaminiani, ni nani wa kumwambia,
Kuuliza wa zamu nani, daktari alokua,
Mgonjwa kumuauni, nafuu akaijua,
Kituo cha afya hoi, daktari wake nani?

Majibu yao utani, na mengine ni mzaha,
Fakiri hawajioni, mzuri hawajamjua,
Kila mtu hatiani, ubaya wameshamtia,
Kituo cha afya hoi, daktari wake nani?

Mlinzi usingizini, kazi mbili kazidiiwa,
Usiku yuko lindoni, mchana getini atua,
Kumwamsha kabaini, kituo kimevamiwa,
Kituo cha afya hoi, daktari wake nani?

Kutugungua wageni, ndipo alipotulia,
Kumhoji kwa yakini, ulozi kahadithia,
Kimelogwa kwa yakini, na majirani wabaya,
Kituo cha afya hoi, daktari wake nani?

Ramli keshaamini, lazima kukipigia,
Ajulikane ni nani, mema asiyekitakia,
Hoja hatukuamini, kusepa tukaamua,
Kituo cha afya hoi, daktari wake nani?

Tarishi katoka ndani, wote tukamrukia,
Dakatari wa zamu nani, mgonjwa amezidiwa,
Katupeleka nyumbani, daktari ana njaa,
Kituo cha afya hoi, daktari wake nani?

Mlo kakosa maskini, mke kamkimbia,
Kafuata wa mjini, wajuao kuchagua,
Na kula vyenye thamani, si matembele kuzoa,
Kituo cha afya hoi, daktari wake nani?

Maneno kwisha kinywani, haraka tukajizoa,
Tukarudi maskini, maswali twaulizia,
Hali hii yumkini, mgonjwa atatibiwa?
Kituo cha afya hoi, daktari wake nani?

Mwanakijiji si mtu

Ukweli hatujathubutu, ila tutasema nini?
Wa shambani sio watu, watu wakaa mjini,
Hii ndio nchi yetu, na huu wetu utani,
Mwanakijiji si mtu, watu waishi mjini!

Hii ndio nchi yetu, na huu wetu utani,
Vijiji vyetu misitu, tena waishi gizani,
Wangelikuwa watu, huu si uhayawani?
Mwanakijiji si mtu, watu waishi mjini!

Nitawachukiza watu, walio serikalini,
Hilo kwangu sio kitu, ukweli watabaini,
Maana hawa wenzetu, hawakuzaliwa mjini,
Mwanakijiji si mtu, watu waishi mjini!

Huu ubaguzi wetu, kama Afrika kusini,
Twasahau watu wetu, kama sio hesabuni,
Twadhani eti si watu, wanaoishi vijijini?
Mwanakijiji si mtu, watu waishi mjini!

Kujiumbua wenzetu, ubaya wala sioni,
Haufai utukutu, haukubali Manani,
Na maisha ya wenzetu, si pungufu kwa thamani,
Mwanakijiji si mtu, watu waishi mjini!

Mtu hajawa kiatu, ingawa kina thamani,
Mtu hakika mwenzetu, hata awe masikini,
Na maendeleo yetu, bila yeye mashakani,
Mwanakijiji si mtu, watu waishi mjini!

Mtu awe na ukurutu, bado anayo thamani,
Na wewe wala si kitu, utaenda kaburini,
Utaacha kila kitu, naye angali duniani,
Mwanakijiji si mtu, watu waishi mjini!

Moyo ukiachwa butu, hushusha watu thamani,
Na akajiona mtu, ni ka-Mungu duniani,
Wawe watumwa wenzetu, na wakubwa majinuni,
Mwanakijiji si mtu, watu waishi mjini!

Iwe ni nuksi kwetu, makosa kutobaini,
Tuitoe toba yetu, atusamehe Manani,
Tuwapende watu wetu, kama ni wetu mwandani,
Mwanakijiji si mtu, watu waishi mjini!

Chozi la mamba

NInaiona hadaa, viongozi wakilia,
Mjini watu wajaa, vijiji wanakataa,
Hali sote tunajua, serikali yachangia,
Watu mjini kujaa, chozi la mamba mwalia.

Viongozi wa hadaa, haya wanajitakia,
Siasa zinatuua, wao wanafurahia,
Uchumi wamekalia, kama mibweha walia,
Watu mjini kujaa, chozi la mamba mwalia.

Kila kitu wanagawa, mjini wanaopewa,
Vijiji vyaambulia, ahadi nazo hadaa,
Maporini kumekua, vigumu kuendelea,
Watu mjini kujaa, chozi la mamba mwalia.

Haya tiulipoanzia, Uyahudi nao pia,
HIvi leo wamekua, na vijiji maridhia,
Tofauti hutojua, kijijini ukikaa,
Watu mjini kujaa, chozi la mamba mwalia.

Kwetu nyikani twajua, tena ni gizani pia,
Umeme haujaingia, na maji ni tope hua,
Katika kuendelea, mimi hili nakataa,
Watu mjini kujaa, chozi la mamba mwalia.

Busara tungetumia, vijana wasingekimbia,
Mahitaji yangekuwa, shamba yameshaenea,
Huna la kukusumbua, kila kitu wanunua,
Watu mjini kujaa, chozi la mamba mwalia.

Nani angeliamua, kijijini kutokaa,
Mjini tungekimbia, arkadi kuvamia,
Hewa tuipate poa, kutengemaa zetu afya,
Watu mjini kujaa, chozi la mamba mwalia.

KIpaumbele

Nchi imeshaamua, magari kwanza kutua,
Nchini yakaenea, mitaani yakajaa,
Ili watu kudhania, nchi inaendelea,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Mjinga hajatambua, nafasi kaitumia,
Garii pato lagombea, na wake hao jamaa,
Petroli likajaa, na watu kulala nja,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Ufahari wakolea, wajivuna kwenye njia,
Mfukoni ukiingia, ndururu haijasalia,
Eti huku kwendelea, kwa vipi sijajua,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Magari hutangulia, barabara kufatia,
Ni sheria yabuniwa, kitini waliokaa,
Mwehu wanamdhania, mwalimu kuvikataa,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Utu umewapotea, watazame kwenye njia,
Kila anayetumia, ataka wa kwanza kua,
Na haya yakitokea, wote huwa wachelewa,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Kwa mguu wanaotembea, vigumu kuheshimiwa,
Wajinga wanaambiwa, na matusi kutupiwa,
Ma'na walojaliwa, ndio wenye motokaa,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Pikipiki nazo pia, Bajaji zinafuatia,
Ubinadamu wapea, majiani ni balaa,
Watalii wakimbia, salama imepotea,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Kwenye hizi zetu njia, kama hakuna sheria,
Wenyewe wajiamulia, wanalolifikiria,
Na hata wakikosea, rushwa wanaitoa,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Polisi waangalia, wazidi changanyikwa,
Nani kumshikilia, nani kumuachia?
Imekua kizaazaa,kwenda nje kutembea,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Ila wanapoambiwa, virungu kuturushia,
Haraka huchangamkia, ila kuja tuibia,
Mradi umeshakua, walo juu hawajajua,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

KIpaumbele ?

Nchi imeshaamua, magari kwanza kutua,
Nchini yakaenea, mitaani yakajaa,
Ili watu kudhania, nchi inaendelea,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Mjinga hajatambua, nafasi kaitumia,
Garii pato lagombea, na wake hao jamaa,
Petroli likajaa, na watu kulala nja,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Ufahari wakolea, wajivuna kwenye njia,
Mfukoni ukiingia, ndururu haijasalia,
Eti huku kwendelea, kwa vipi sijajua,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Magari hutangulia, barabara kufatia,
Ni sheria yabuniwa, kitini waliokaa,
Mwehu wanamdhania, mwalimu kuvikataa,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Utu umewapotea, watazame kwenye njia,
Kila anayetumia, ataka wa kwanza kua,
Na haya yakitokea, wote huwa wachelewa,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Kwa mguu wanaotembea, vigumu kuheshimiwa,
Wajinga wanaambiwa, na matusi kutupiwa,
Ma'na walojaliwa, ndio wenye motokaa,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Pikipiki nazo pia, Bajaji zinafuatia,
Ubinadamu wapea, majiani ni balaa,
Watalii wakimbia, salama imepotea,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Kwenye hizi zetu njia, kama hakuna sheria,
Wenyewe wajiamulia, wanalolifikiria,
Na hata wakikosea, rushwa wanaitoa,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Polisi waangalia, wazidi changanyikwa,
Nani kumshikilia, nani kumuachia?
Imekua kizaazaa,kwenda nje kutembea,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Ila wanapoambiwa, virungu kuturushia,
Haraka huchangamkia, ila kuja tuibia,
Mradi umeshakua, walo juu hawajajua,
Barabara zije mwisho, magari tulete kwanza!

Mitumba ni hadhi yetu

Kunung'unika yafaa, wakubwa wameshaamua,
Suti mpya kuzivaa, ni wakubwa walokuwa,
Vizito wenye ridhaa, na vigogo nao pia,
Mitumba ni hadhi yetu, wakubwa walishaamua!

Mitumba wameamua, ni hadhi inayofaa,
Kwetu akina raia, ni lazima kuivaa,
Lawama haitafaa, twapasa kuitikia,
Mitumba ni hadhi yetu, wakubwa walishaamua!

Ni nguo tumeanzia, na sasa pia vifaa,
Meli watatuletea, mitumba zilizokua,
Ndege za kupaa pia, mitumba tutatumia,
Mitumba ni hadhi yetu, wakubwa walishaamua!

Magari yameshajaa, wala hayatapungua,
Matrekta yaja pia, na malori kununua,
Dampo nchi sasa kua, wakubwa wameamua,
Mitumba ni hadhi yetu, wakubwa walishaamua!

Ajali zikitokea, mengine kusingizia,
Mola atatushangaa, kwa haya kuyaamua,
Jinsi tulivyozubaa, mikenge tunavyoingia,
Mitumba ni hadhi yetu, wakubwa walishaamua!

Mapato wamegundua, njia ya kujipatia,
NI kumi asilimia, watakayoichukua,
Roho zikiteketea, hayo yetu majaliwa,
Mitumba ni hadhi yetu, wakubwa walishaamua!

Akili zimefubaa, twashinda jitengenezea,
Walau kuviungia, nchini tulipokaa,
Kwa zana kuagizia, na kuja kujiungia,
Mitumba ni hadhi yetu, wakubwa walishaamua!

Vya nje kutegemea, kamasi watatutoa,
Mbona watu wamejaa, na kazi hawajapewa,
Wazungu wanaojua, mitambo kujiundia,
Mitumba ni hadhi yetu, wakubwa walishaamua!

Ulaya tukisogea, wengi watatuitikia,
Kwetu kinachotakiwa, mishahara kuitoa,
Nyumba kuwapatia, waishi na familia,
Mitumba ni hadhi yetu, wakubwa walishaamua!

Wapenda kuogelea, pwani tutawajengea,
Mali ghafi kununua, kazi iliyobakia,
Kuunda wakaanzia, vyote tunavyohitajia,
Mitumba ni hadhi yetu, wakubwa walishaamua!

Ustawi tutazua, tena fumba na kufumbua,
Tukazalisha vifaa, na nje kujiuzia,
Nyumbani vikazagaa, mradi umeme kufua,
Mitumba ni hadhi yetu, wakubwa walishaamua!

Tuacheni kuzubaa, nafasi hii sawia,
Twashinda ipalilia, au hatujaitambua,
Wengine wakigundua, fursa itapotea,
Mitumba ni hadhi yetu, wakubwa walishaamua!

Sukari kwetu anasa

Swali ninawatumia, wanaojua sheria,
Soko huru imekua, au siasa nazaa?
Vipi mnayoamua, kinyume chake kikawa?
Sukari kwetu anasa, soko mfungwa, soko huru?

Bei zote zatakiwa, zenyewe kujiamua,
Vipi mnaingilia, nini tulichoambua,
Si bora ingekua, mapema kuagizia,
Sukari kwetu anasa, soko mfungwa, soko huru?

Soko huru mkitua, acheni likaamua,
Na bei itatulia, mbali mkiangalia,
Sio kulala ikawa, hadi jambo kutokea
Sukari kwetu anasa, soko mfungwa, soko huru?

Mwakurupuka jamaa, bei kuitangazia,
Kichwani iliokaa, sio soko kuamua,
Kisha mnashangaa, mipakani kwelekea,
Sukari kwetu anasa, soko mfungwa, soko huru?

Inawaona vichaa, mfanyalo hamjajua,
Ukweli mkitambua, afueni tutajua,
Rahisi inapokuwa, sisi twende kununua,
Sukari kwetu anasa, soko mfungwa, soko huru?

Nje inapotakiwa, ni vyema kuiachia,
Mradi tumeshagundua, akiba ndani ikawa,
Ya nje tulonunua, hili tukitarajia,
Sukari kwetu anasa, soko mfungwa, soko huru?

Akili tukitumia, rahisi tukanunua,
Ghali yetu inapokuwa, wengine twawauzia,
Uchumi utajakua, biashara zikapaa,
Sukari kwetu anasa, soko mfungwa, soko huru?

Lishe

Aipate lishe nani, bei kama eropleni,
Zapaa juu angani, na sisi tungali chini,
Walio na afueni, wote hao wa mjini,
Lishe aipate nani, bei zapaa angani?

Bei zetu mumiani, damu zanywa miilini,
Tumebaki hamnani, ni mashine za Manani,
Naye ni kwayo imani, uhai ungenda mbweni,
Lishe aipate nani, bei zapaa angani?

Hili jambo la kanuni, si bure hulibaini,
Lataka kwa yumkini, taratibu na hisani,
Na sio uhayawani, wengine kutothamini,
Lishe aipate nani, bei zapaa angani?

Ukiwaacha maaluni, wasio nayo imani,
Wao hawana utani, ubaya watasaini,
Na roho ziwe shakani, mijini na vijijini,
Lishe aipate nani, bei zapaa angani?

Naamini, siamini, mpaka uone ndani,
Maisha ni kitu gani, kama hayana thamani,
Na kudhibiti ni nani, ila walo mamlakani?
Lishe aipate nani, bei zapaa angani?

Lishe

Aipate lishe nani, bei kama eropleni,
Zapaa juu angani, na sisi tungali chini,
Walio na afueni, wote hao wa mjini,
Lishe aipate nani, bei zapaa angani?

Bei zetu mumiani, damu zanywa miilini,
Tumebaki hamnani, ni mashine za Manani,
Naye ni kwayo imani, uhai ungenda mbweni,
Lishe aipate nani, bei zapaa angani?

Hili jambo la kanuni, si bure hulibaini,
Lataka kwa yumkini, taratibu na hisani,
Na sio uhayawani, wengine kutothamini,
Lishe aipate nani, bei zapaa angani?

Ukiwaacha maaluni, wasio nayo imani,
Wao hawana utani, ubaya watasaini,
Na roho ziwe shakani, mijini na vijijini,
Lishe aipate nani, bei zapaa angani?

Naamini, siamini, mpaka uone ndani,
Maisha ni kitu gani, kama hayana thamani,
Na kudhibiti ni nani, ila walo mamlakani?
Lishe aipate nani, bei zapaa angani?

Lishe

Aipate lishe nani, bei kama eropleni,
Zapaa juu angani, na sisi tungali chini,
Walio na afueni, wote hao wa mjini,
Lishe aipate nani, bei zapaa angani?

Bei zetu mumiani, damu zanywa miilini,
Tumebaki hamnani, ni mashine za Manani,
Naye ni kwayo imani, uhai ungenda mbweni,
Lishe aipate nani, bei zapaa angani?

Hili jambo la kanuni, si bure hulibaini,
Lataka kwa yumkini, taratibu na hisani,
Na sio uhayawani, wengine kutothamini,
Lishe aipate nani, bei zapaa angani?

Ukiwaacha maaluni, wasio nayo imani,
Wao hawana utani, ubaya watasaini,
Na roho ziwe shakani, mijini na vijijini,
Lishe aipate nani, bei zapaa angani?

Naamini, siamini, mpaka uone ndani,
Maisha ni kitu gani, kama hayana thamani,
Na kudhibiti ni nani, ila walo mamlakani?
Lishe aipate nani, bei zapaa angani?

Maji hakika uhai

Uhai maji hakika, pale yanapotulia,
Maji yakishatoweka, uhai unapotea,
Jambo hili si dhihaka, twafaa kuzingatia,
Maji hakika uhai, twapasa kulitambua!

Bakhressa si dhihaka, hili kaling'amua,
Jina alilopachika, sadifu linshakua,
Atamlipa Khalaka, na Muhyi alokua,
Maji hakika uhai, twapasa kulitambua!

Wengine wana wahaka, biashara watambua,
Wataka kutajirika, kwa mito nayo mvua,
Mungu anavyovitaka, bure bure vingekua,
Maji hakika uhai, twapasa kulitambua!

Serikali kujengeka, maji budi kuyatoa,
Vyanzo vikalindika, vya mito nayo mvua,
Pasiwe nayo mashaka, katika hii dunia,
Maji hakika uhai, twapasa kulitambua!

Haya yakitengeneka, uchumi tutaunyanyua,
Maji yatajauzika, kwa nayo wasiokua,
Nchi ikatajirika, mara fumba na kufumbua,
Maji hakika uhai, twapasa kulitambua!

Nadhani limeeleweka, fanya kinachotakiwa,
Acheni kujishobodoka, na ovyo kushangilia,
Nchi malezi yataka, sio wasanii kua,
Maji hakika uhai, twapasa kulitambua!

Nanywa tope

Kitu gani washangaa, tope nalimiminia,
Ndiyo maji yalokuwa, kijijini twatumia,
Ndivyo mlivyoamua, toka uhuru kwingia,
Waamua ninywe tope, kwanini unashangaa!

Dodoma tumezoea, Umasaini nao pia,
Maji yasiyotufaa, ndyo tunayotumia,
Serikali yashangaa, hali hili wamezaa?
Waamua ninywe tope, kwanini unashangaa!

Kunywa safi mwaamua, nyie juu mlokua,
Na kisha mnashangaa, tope tunapobugia,
Na hamjatufikia, japo tunawangojea,
Waamua ninywe tope, kwanini unashangaa!

Wadudu ni wetu pia, Mungua anatusaidia,
Anazilinda aya, vingine tungejifia,
Tunaowategemea, bure ghali wamekua,
Waamua ninywe tope, kwanini unashangaa!

Beti zimeshatimia, ujumbe nimeutoa,
Vingine kuangalia, au utu wapotea,
Vipi tutawafikiria, dhamana mnaopewa?
Waamua ninywe tope, kwanini unashangaa!

Umeme wanaolia

Habari toka mjini, umeme unawahini,
Ila huku vijijini, hatujui jambo gani,
Twashangaa kwa yakini, wanakosa kitu gani,
Umeme wao mjini, giza letu vijijini.

Umeme wao mjini, sisi hatujabaini,
GIza letu vijijini, japo miaka hamsini,
Washangaa duniani, wakitua vijijini,
Umeme wao mjini, giza letu vijijini.

Ni kisingizio gani, waweza toa mjini,
Kama huu uhaini, hauletwi na uhuni,
Miradi walobaini, mbona yote mashakani,
Umeme wao mjini, giza letu vijijini.

Nafaka wala njiani, na mbegu zi mdomoni,
Wamechoka wahisani, malengo hawabaini,
Twashangaa kitu gani, na shetani yumo ndani,
Umeme wao mjini, giza letu vijijini.

Shetani ndio wahuni, ya k wao wanathamini,
Hawajali vijijini, kila kitu kuwahini,
Ni maendeleo gani, mbona sisi hatuoni?
Umeme wao mjini, giza letu vijijini.

Na wengine hayawani, wataka tuliamini,
Jambo lisilo makini, wala ukweli huoni,
Hatujawa majinuni, uongo kuuthamini,
Umeme wao mjini, giza letu vijijini.

Mapinduzi ni auni, tukatazame Japani,
Wanarudi vijijini, wamechoka na mjini,
Na sisi tuwe njiani, kuthamini vijijini,
Umeme wao mjini, giza letu vijijini.

Uchafu tumezoea

Usafi huwa tabia, mbali inayotokea,
Ukijenga mazoea, akilini hubakia,
Huna utaloamua, bila ya kuzingatia,
Uchafu ni mazoea, huponywa na taadibu!

Uchafu usipotia, pahala hapana doa,
Ila hapo ukiachia, pachafu patajakua,
Usafi njema tabia, uchafu unazuia,
Uchafu ni mazoea, huponywa na taadibu!

Binafsi watakiwa, usafi kuangalia,
Nia kutokulegea, hata ukiwa mkiwa,
Na ukajihudumia, ukawa ni mashalaa,
Uchafu ni mazoea, huponywa na taadibu!

Si nje unaanzia, bali ndani unakokaa,
Vitu vyote vyatakiwa, daima safi vikawa,
Kuvipanga ni murua, si ovyo vikasambaa,
Uchafu ni mazoea, huponywa na taadibu!

Muhimu pakafagiwa, na bora ni kudekiwa,
Taka ukajizolea, mbali ziende tupiwa,
Nyumba yote ikang'aa, na vizuri kunukia,
Uchafu ni mazoea, huponywa na taadibu!

Nje nako kufagia, taka kutokuhamia,
Na kisha panda maua, watu yanayovutia,
Kwa rangi zilizojaa, na harufu kunukia,
Uchafu ni mazoea, huponywa na taadibu!

Bustani inafaa, kwa nyumba pia mitaa,
Na misitu manispaa, miti bora kupandia,
Hali ya hewa ikawa, ni yenye kutamaniwa,
Uchafu ni mazoea, huponywa na taadibu!

Taadibu kwa wasia, na maneno ya kufaa,
Kwa uple simamia, na nyenzo kuwapatia,
Watu katika mitaa, uchafu kwao si nia,
Uchafu ni mazoea, huponywa na taadibu!

Ila ukivumilia, uchafu huwa tabia,
Watu wakaizoea, wasiwe nayo kinaya,
Yote waone ni sawa, pepo ikawa kinyaa,
Uchafu ni mazoea, huponywa na taadibu!

Tarafu

Si watu wa kukinai, huo sio mwendo wao,
Hawa watu bila rai, hulinda nafsi yao,
Wengine hawawajui, ila kwa matamanio,
Tarafu hawaijui, bado wataka kula wao.

Mengine ni goigoi, haraka si mwendo wao,
Haki hawatanabahi, ila iwe ni ya kwao,
Hawadai maslahi, nayo kama siyo yao,
Tarafu hawaijui, bado wataka kula wao.

Hawa ni wetu nabii, wenyewe wajichaguao,
Zama hizi za uhai, haya ndiyo wavunayo,
Si kama ninakebehi, huu ndio ukweli wao,
Tarafu hawaijui, bado wataka kula wao.

Ni rahisi yao bei, gharama waibebayo,
Hutoi9na nishai, utaridhi wasemayo,
Ukiona hayafai, wawa ni mtaji kwao,
Tarafu hawaijui, bado wataka kula wao.

Kandili si karabai, huelewa wajuao,
Nazi haijawa tui, bila lako kamulio,
Na chunusi sio ndui, usimuache mkeo,
Tarafu hawaijui, bado wataka kula wao.

Wazee wa Tanzania

Wazee mnatumiwa, kama fala mmekua,
Amkeni twawambia, asubuhi inshakua,
Yenu kusimamia, na sio kusimamiwa,
Wazee wa Tanzania, iundeni Jumuiya !

Wangapi wadhulumiwa, na yote tunayajua,
Serikali imekaa, pembeni yaangalia,
Vipi mwachaguliwa, harabu kuitikia?
Wazee wa Tanzania, iundeni Jumuiya !

Wazee mmejaliwa, busara zimewajaa,
Historia mwajua, na nchi ilikotokea,
Na tunakoelekea, mwaweza mkakosoa,
Wazee wa Tanzania, iundeni Jumuiya !

Na tunakoelekea, mwaweza mkakosoa,
Wakubwa kuwaambia, njia mmeshakosea,
Safari mkiendelea, lazima mtapotea,
Wazee wa Tanzania, iundeni Jumuiya !

Mkikubali kutumiwa, ni nani kuwaambia?
Wao watakujadhania, eti njia wanaijua,
Wakafosi kupotea, jahazi mrama likawa,
Wazee wa Tanzania, iundeni Jumuiya !

Wazee nawatambua, hekima mmeshapewa,
Mengi mmeshagundua, na wapi tunakosea,
Kussema mkijaliwa, wengi watayasikia,
Wazee wa Tanzania, iundeni Jumuiya !

Mkianza Jumuiya, haya kuzungumzia,
Pia itawatetea, na kilio kikasikiwa,
Adha zikawapungua, mkapata kupumua,
Wazee wa Tanzania, iundeni Jumuiya !

Wanawake Tanzania

Waoga walikimbia, au walondolewa,
Vyeo kutunukiwa, majuu wakaishia,
Ukubwa ulipokoa, watoto kazi kulea,
Wanawake Tanzania, iundeni Jumuiya.

Wengine wanatumiwa, na wakubwa walokua,
Zawadi wakigaiwa, mapambano yapotea,
Nchi inaangamia, nyie mnazainiwa?
Wanawake Tanzania, iundeni Jumuiya.

Uchama mnatakiwa, kabisa kuukataa,
Jumuiya kuizua, wanawake kuingia,
Bila mmoya kubagua, chama anachotokea,
Wanawake Tanzania, iundeni Jumuiya.

Maslahi ya radhia, hakika yafanania,
Vinginevyo haijawa, ila wanaopendelewa,
Wao watajivunia, kwa hivyo wanavyopewa,
Wanawake Tanzania, iundeni Jumuiya.

Wamoja mkishakua, nguvu mtajionea,
Milima mtabomoa, na madaraja kutua,
Nchi juu ikapaa, na jamii kupumua,
Wanawake Tanzania, iundeni Jumuiya.

Hamfai kubakia, sarawili kuivua,
Baba kumtegemea, na nyie mnshakua,
Waume mwatarajiwa, sasa kuja watumikia,
Wanawake Tanzania, iundeni Jumuiya.

Waume wanaowafaa, hawa wote Watanzania,
Sauti mkaitoa, hoja mkajijengea,
Na sio kushangilia, au wengine kuzomea,
Wanawake Tanzania, iundeni Jumuiya.

Vijana wa Tanzania

Vijana mnatumiwa, wazee kuwainua,
Nyuma mnabakia, makombo mnayapewa,
Wakati umefikia, usukani kuutwaa,
Vijana wa Tanzania, kuweni kitu kimoja!

Vyama sasa vyawagawa, kutawala iwe poa,
Nanyi hamjajua, madebe mwawapigia,
Akili zikikomaa, kando mtawafagia,
Vijana wa Tanzania, kuweni kitu kimoja!

Yenu hii Tanzania, ya wazee haijawa,
Ima fa ima kuamua, nchi kuisimamia,
Wazee wameshapoa, akili zinalemaa,
Vijana wa Tanzania, kuweni kitu kimoja!

Maamuzi wachelewa, haraka yanayofaa,
Tanzania kuongoa, juu ikaja kupaa,
Vijana mnatakiwa, vitani kuja ingia,
Vijana wa Tanzania, kuweni kitu kimoja!

Bungeni wanaosinzia, lazima kuwaondoa,
Hatimaye kubakia, uangavu walokua,
Fikra kuzichangia, bora tukaja jaliwa,
Vijana wa Tanzania, kuweni kitu kimoja!

Vijana wa Tanzania, uchama kuukataa,
Jumuiya yenu kuwa, ya vijana Tanzania,
Uchama mbali kufia, umoja tukaulea,
Vijana wa Tanzania, kuweni kitu kimoja!

Nguvu zitawazidia, chini ya chama hupwaya,
Mengi wanayoamua, ni wazee yawafaa,
Na si kizazi kipya, ambacho hufikiriwa,
Vijana wa Tanzania, kuweni kitu kimoja!

Nyie wazazi mshakua, kizazi kinachojia,
Balaa kuwaondolea, mwapasa mengi kujua,
Salama nchi ikawa, hata mtapojifia,
Vijana wa Tanzania, kuweni kitu kimoja!

Napuyanga Mmachinga

Mmachinga natembea, daima chini ya jua,
Kichwa kinaungua, sina pa kukimbilia,
Riziki nimenuia, ni lazima kuingia,
Napuyanga mmachinga, changudoa atanua!

Halali nimeamua, haramu sintochukua,
Serikali yaamua, mjini kuniondoa,
Bongo hawajatumia, mimi hilo ninajua,
Napuyanga mmachinga, changudoa atanua!

Twaweza kusaidiwa, kivutio tuje kuwa,
Watalii kutujia, na vitu kuvinunua,
Nchi juu itakuwa, na uchumi utapaa,
Napuyanga mmachinga, changudoa atanua!

Akili wameamua, likizo kwenda kukaa,
Vitu kufikiria, uvivu wameshaingia,
Maamuzi kuamua, masikini waje lia,
Napuyanga mmachinga, changudoa atanua!

Napuyanga, natembea, nimezibeba bidhaa,
Watu nawafikishia, hadi wanakotokea,
Nyumbani kuwafikia, nafuu kuwapatia,
Napuyanga mmachinga, changudoa atanua!

Mimi sijaheshimiwa, ila wao changudoa,
Magari wawanunulia, na mitaani kung'aa,
Uchumi sijaelewa, nini wanachochangia,
Napuyanga mmachinga, changudoa atanua!

Atanua changudo, Mmachinga natembea,
Nani kunisaidia, hali akaninyanyua,
Mwanamke sijakua, labda wangetokea,
Napuyanga mmachinga, changudoa atanua!

Ninakunywa nisahau

Ninakunywa nimsahau, mpenzi wangu wa zamani,
Tanzania ya nahau, upendo na ulaini,
Aliyekuwa mdau, mwandani mwenye imani,
Ninakunywa nisahau, masahibu nchi yangu!

Amenifanya bahau, tena hatuaminiani,
KIsha ananidharau, na kuwapenda wageni,
Nikijaribu msahau, ninashindwa kwa yakini,
Ninakunywa nisahau, masahibu nchi yangu!

Anitenda makuruhu, ila yungali moyoni,
Yamenishinda malau, nataka hama nyumbani,
Nachelea kuwa mwehu, kumuacha mawazoni,
Ninakunywa nisahau, masahibu nchi yangu!

Namuomba Binti Chau, akienda redioni,
Ushauri kunukuu, Hamada niuthamini,
Siridhiki na makuu, mlevi nifanye nini?
Ninakunywa nisahau, masahibu nchi yangu!

Zimenitoka nahau, mwenzenu majaribuni,
Sasa ni mifupa na fuu, nyama sinayo mwilini,
Na mwingi wa kusahau, nami si usingizini,
Ninakunywa nisahau, masahibu nchi yangu!

Shoka hataki kazi

Shoka kakataa kazi, kukiondoa kisiki,
Kasema huyu hamwezi, kiuno hakishikiki,
Amemzidi ujuzi, na tena hatabiriki,
Shoka kakataa kazi, ya kisiki cha mpingo.

Kagundua pingamizi, kisiki hakikatiki,
Litamchosha mkwezi, mwenye afya ya kaniki,
Hata na wao Maswezi, hili hawaaminiki,
Shoka kakataa kazi, ya kisiki cha mpingo.

Hautambi ujuzi, hakina mpango kisiki,
Hukufanya mpuuzi, watazame Wagiriki,
Hata ufanye zoezi, ukija kwaye hacheki,
Shoka kakataa kazi, ya kisiki cha mpingo.

Hili kubwa dudumizi, kung'oka haliafiki,
Wanageuzwa machizi, wakijaribu hilaki,
Hutiririka machozi, mahala hapakaliki,
Shoka kakataa kazi, ya kisiki cha mpingo.

Makalio kuwa nje

Mshairi nashagaa, katakei walokua,
Majina sijatambua, kuitwa nini wafaa,
Kila nikiwaangalia, naona kama bidhaa?
Makalio kuwa nje, ni shoga au ni mende?

Wanawake naelewa, wateja wanavutia,
Kina blaza sijajua, nini wanafukuzia,
Chupi ikitokezea, na makalio bwabwajaa,
Makalio kuwa nje, ni shoga au ni mende?

Kama shoga sijajua, au mende wamendea?
Wazazi mwawaangalia, au mmechanganyikiwa,
Kama dini msojua, na vitabu mwasomea?
Makalio kuwa nje, ni shoga au ni mende?

Huu si Utanzania, yakini naukataa,
Kuiga kulikokua, taahira walokua,
Huku wanajidhania, ni wazima walokua,
Makalio kuwa nje, ni shoga au ni mende?

Weza chelewa uishi

Weza chelewa uishi, alowahi ende kufa,
Hii ni yetu aushi,na haya yake maarifa,
Huzua kama mzushi, tena pasipo kashfa,
Weza chelewa uishi, uwahi uende kufa.

Maisha kama nakshi,hupuputika wasifa,
Umri ni kama moshi, humalizika masafa,
Hauna tija ubishi, haujajenga orofa,
Weza chelewa uishi, uwahi uende kufa.

Bahati ni bakshshi, na wala haina ofa,
Huli la mwenzio dishi, hata apate kifafa,
Na wala hapana mzishi, ukiandikiwa mofa,
Weza chelewa uishi, uwahi uende kufa.

Hundi haijawa keshi, ayajua hata lofa,
Njia hauirekebishi, akiichora latifa,
Ukileta ushawishi, hukukuta yaso sifa,
Weza chelewa uishi, uwahi uende kufa.

Weza chelewa uishi

Weza chelewa uishi, alowahi ende kufa,
Hii ni yetu aushi,na haya yake maarifa,
Huzua kama mzushi, tena pasipo kashfa,
Weza chelewa uishi, uwahi uende kufa.

Maisha kama nakshi,hupuputika wasifa,
Umri ni kama moshi, humalizika masafa,
Hauna tija ubishi, haujajenga orofa,
Weza chelewa uishi, uwahi uende kufa.

Bahati ni bakshshi, na wala haina ofa,
Huli la mwenzio dishi, hata apate kifafa,
Na wala hapana mzishi, ukiandikiwa mofa,
Weza chelewa uishi, uwahi uende kufa.

Hundi haijawa keshi, ayajua hata lofa,
Njia hauirekebishi, akiichora latifa,
Ukileta ushawishi, hukukuta yaso sifa,
Weza chelewa uishi, uwahi uende kufa.

Mjinga akijaliwa

Juzi halikuanzia, milenie latukia,
Ukubwa anayepewa, fala hujizungushia,
Wakao kumsifia, na wala si kumuongoa,
Mjinga akitawala, werevu huwachukia!

Ukubwa wanaolilia, kwa magambo nazo riha,
Akili waliovia, jipya wasilojua,
Bahau hujivunia, matofali ya kujengea,
Mjinga akitawala, werevu huwachukia!

Na yeye juu akiwa, nchi huiporomoa,
Ahadi nyingi hutoa, ila chache hutimia,
Si mtu wa kujijua, tao hajaigundua,
Mjinga akitawala, werevu huwachukia!

Huzungukwa na hadaa, ndani na nje mwake pia,
Taa kwao mshumaa,na tamaa ni kinaya,
Ukubwawe huutumia, machafu kuyawazia,
Mjinga akitawala, werevu huwachukia!

Mola kumgeukia, usanii hutumia,
Hujifanya wanajua, kumbe njia wapotea,
Nafsi haiwi ua, bali tunda la kuoza,
Mjinga akitawala, werevu huwachukia!

Huzungukwa na jamaa, njia wasiozijua,
Ni ng'ombe waloachiwa, mchungaji bila kua,
Na simba akitokea, kila mtu lwake huwa,
Mjinga akitawala, werevu huwachukia!

Vitabu vinatuambia, hakika mali hadaa,
Pia wake zetu baa, tusipokujaangalia,
Aidha na wana pia, Mola anaotujalia,
Mjinga akitawala, werevu huwachukia!

Muumini maridhia, mitihani huijua,
Kila akitahiniwa, maksi huzichukua,
Hatimaye hujinoa, kufaulu kujaliwa,
Mjinga akitawala, werevu huwachukia!

Haya nawasimulia, kukumbushana ni nia,
Kumbusha tunaambiwa, wapo watakaosikia,
Faida kwako ikawa, siku ya kuhesabiwa,
Mjinga akitawala, werevu huwachukia!

NInasujudu Alaa, Awali uliyekuwa,
Akheri mtarajiwa, uweze kunijalia,
Kuiepuka hadaa, salama hai nikawa,
Mjinga akitawala, werevu huwachukia!

Sunday, November 27, 2011

Mhandisi mlimbwende?

Mhandisi mlimbwende, atafutwe duniani,
Asiye shoga na mende, na mzuri wastani,
Na dunia imgande, na kumtunuku thamani,
Mhandisi mzuri nani, shindano kimataifa?

Kama yupo na aunde, tuvitakavyo nchini,
Tuache kuwa vibonde, wa wazungu duniani,
Ardhi yetu itande, kwa tulivyovibaini,
Mhandisi mzuri nani, shindano kimataifa?

Magari nani aunde, yatembee majiani,
Meli nazo tuzipande, kwenda nazo visiwani,
Na mitambo tuichunde, migodini na viwandani,
Mhandisi mzuri nani, shindano kimataifa?

Ndege nazo tuziunde, za mizigo na liinsani,
Ziruke hadi ziende, kwa wetu hao watani,
Viongozi wazipande, waende ughaibuni,

Viongozi wazipande, waende ughaibuni,
Sio za watu wagande, kwa nauli maaluni,
Na wenyewe wawaponde, wawe hawana thamani,
Mhandisi mzuri nani, shindano kimataifa?

Vyeti lazima vivunde, ubora umkononi,
Injinia tuwapende, waundao vya thamani,
Tena mema tuwatende, watupeleke angani,
Mhandisi mzuri nani, shindano kimataifa?

Na milima na mabonde, tuyaambae nyikani,
Mbele tusonge kipande, chakuridhisha moyoni,
Na dunia itupende, kutupa mpya thamani,
Mhandisi mzuri nani, shindano kimataifa?

Nishani kwa mwalimu?

Huwa hana wadhifa, anzia na kitaifa,
Ukija kimataifa, hayo ya mbali masafa,
Labda wampe FIFA, kazi ya soka urefa,
Mwalimu bora ni nani, shindano kimataifa?

Mwalimu fakiri hufa, hii ndiyo yake sifa,
Akiwapa maarifa, wajao jenga ghorofa,
Malapa ni yake sifa, nyumba yake ina ufa,
Mwalimu bora ni nani, shindano kimataifa?

Mshaharawe maafa, na kukopwa yake dhifa,
Hata akiwachachafya, hali mkate wa mofa,
Hubakia kuwa lofa, bila mapya maarifa,
Mwalimu bora ni nani, shindano kimataifa?

Huwa naipiga chafya, kwa elimu taarifa,
Iwe bora kitaifa, wakati zazidi nyufa,
Walimu kwenye maafa, wakuze vipi wadhifa?
Mwalimu bora ni nani, shindano kimataifa?

Itabakia kifafa, elimu ya kitaifa,
Nusura sio sharifa, katika haya masafa,
Kwa Wachaga na Waswafa, tunatakiwa hanifa,
Mwalimu bora ni nani, shindano kimataifa?

Iwe ya kimataifa, kwa maudhui na sifa,
Na lugha iwe wadhifa, Kiswahili maarifa,
Lugha ziwe falsafa, kusomwa hadi yakufa,
Mwalimu bora ni nani, shindano kimataifa?

Lugha ziwe falsafa, kusomwa hadi yakufa,
Chekechea makhalifa, mwanzo waijenge sifa,
Vyuoni iwe tarafa, za wageni swahifa,
Mwalimu bora ni nani, shindano kimataifa?

Maudhui si kashfa, kwa Kiswahili latifa,
Wachina kwa maarifa, ndivyo wanavyosahifa,
Lugha ngeni taarifa, kuongezea wadhifa,
Mwalimu bora ni nani, shindano kimataifa?

Atujalie Raufa, tujezipanda ghorofa,
Elimu na maarifa, visijekosa wadhifa,
Tulinyanyue taifa, liwe la kimataifa,
Mwalimu bora ni nani, shindano kimataifa?

Nesi bora ?

Nesi analaumiwa, eti ana roho mbaya,
Na anaowaangalia, hali hawajamjua,
Mimi nachanganyikiwa, wapi pa kusimamia,
Nesi bora duniani, ni nani kimataifa?

Kazi yao ya dunia, hawana pa kutulia,
NI wapi watajakaa, wajaliwe kupumua,
Watu wanaugulia, huduma watarajia?
Nesi bora duniani, ni nani kimataifa?

Wengine wajichafua, kuogeshwa hutakiwa,
Wa kule wanangojea, na wao dawa kupewa,
Hawa wanasubiria, shindano kuja patiwa,
Nesi bora duniani, ni nani kimataifa?

Shida zimezidia, wengine wawa vichaa,
Au kubwa malaria, mtu inamsumbua,
Hapo kazi kubwa hua, kitandani kumvaa,
Nesi bora duniani, ni nani kimataifa?

Wengine kula balaa, lazima kusimamiwa,
Au mirija kutiwa, na kisha kumiminiwa,
Daftari zangojea, taarifa kuchukua,
Nesi bora duniani, ni nani kimataifa?

Operesheni huvia, nesi kama hatatokea,
Bosi huchanganyikiwa, asijue pakuanzia,
Nesi akishatokea, ni rahisi kazi huwa.
Nesi bora duniani, ni nani kimataifa?

Vijisenti twavitaa, yeye tupu abakia,
Mshahara wake njaa, na nyumbani ni balaa,
Hili hatujazingatia, lawama hizi mafua,
Nesi bora duniani, ni nani kimataifa?

Daktari mzuri

Daktari kali njaa, rushwa anaipokea,
Mwanasiasa shujaa, mwenyewe kauchukua,
Mshahara kachukua, mnono uliokua,
Daktari mzuri nani, shindano kimataifa?

Hadithi yafanania, ugali anayepakua,
Mwingi kajipakulia, kiongozi alokua,
Na waliobakia, kidunchu wanapewa,
Daktari mzuri nani, shindano kimataifa?

Mchuzi wote katwaa, wengine warumangia,
Kichwani kaazimia, yeye ndiye wa kufaa,
Wengine kwake mzaha, tena waliolaniwa,
Daktari mzuri nani, shindano kimataifa?

Ubinafsi wamjaa, kiongozi hajajua,
Aone yote ni sawa, akili anatumia,
Nchi inadidimia, wa kwake bado wapaa,
Daktari mzuri nani, shindano kimataifa?

Daktari kachakaa, kashindwa kuvumilia,
Shindanoni kaingia, ukweli wake atoa,
Wenyewe kujitibia, mimi Ulaya napaa,
Daktari mzuri nani, shindano kimataifa?

Daktari mwenye njaa, vipi kifo kuzuia,
Mwatutakia balaa, zahanati wakijaa,
Roho watajatutoa, nakisi kujizibia,
Daktari mzuri nani, shindano kimataifa?

Mbunge mrembo?

Akili tumeamua, zitue kwenye jukwaa,
Kupambana kwa hatua, na sura inavyokua,
Tuone wa kunyakua, ushindi nani atakua,
Ni nani mbunge mrembo, shindano kimataifa ?

Kama vile mabondia, nao watashindania,
Akili awe kulia, na kushoto sura kua,
Wapambane kishujaa, hadi atakayezidiwa,
Ni nani mbunge mrembo, shindano kimataifa ?

Hadi atakayezidiwa, ubingwa kuutwaa,
Ngao akaichukua, ukutani ikakaa,
Wanawe wakatambua, bingwa alikwishang'aa,
Ni nani mbunge mrembo, shindano kimataifa ?

Ndani tuajaingia, nini kazungumzia,
Kilicho cha manufaa, kwa wenzake Watanzania,
Na siku alipotoa, mada isiyosinyaa,
Ni nani mbunge mrembo, shindano kimataifa ?

Vigelegele ikiwa, maksi hatozipewa,
Sifuri kuambulia, na zomeo la jukwaa,
Macho chini akatua, atakavyoumbuliwa,
Ni nani mbunge mrembo, shindano kimataifa ?

Na kama ilitokea, mwenyewe kujitanua,
Ubinafsi kulea, na umimi kubobea,
Jukwaa litamzuzua, kwa miluzi na nazaa,
Ni nani mbunge mrembo, shindano kimataifa ?

Waziri mrembo?

Ni nani aliyekuwa, mrembo kwenye dunia,
Waziri alojaliwa, uzuri kuuchukua,
Sifa kummiminia, apite kwenye jukwaa,
Ni nani waziri mrembo, shindano kimataifa?

Mamissi tunawajua, cheo wanazawadiwa,
Twataka waliopewa, na nafasi kuchukua,
Jukumu walitumia, na wajibu wamepokea,
Ni nani waziri mrembo, shindano kimataifa?

Katika hii dunia, nchi ipi kutokea,
Afrika au Asia, au pengine Ulaya,
Ili tupate kujua, nchi iliyojaliwa,
Ni nani waziri mrembo, shindano kimataifa?

Ni mweusi atakua, au mweupe mzawa,
Kusini watamtoa, au kaskazi kua?
Magharibi kazaliwa, au Mashariki dia?
Ni nani waziri mrembo, shindano kimataifa?

Dunia kaifanyia, nini kilichomnyanyua?
Na ukimlingania, kitu gani kazidia,
Wenzie wamsifia, au wanamuambaa?
Ni nani waziri mrembo, shindano kimataifa?

Sura yake yavutia, na macho amejaliwa?
Ngozi laini kapewa, hariri kumithilia,
Na sauti ni ya hua, au kunguru amepewa?
Ni nani waziri mrembo, shindano kimataifa?

Tunataka kumjua, na vipi kutuagua,
Ujinga kuja jivua, na ufakiri kutua,
Ya heri kutunukiwa, malau tukaambaa,
Ni nani waziri mrembo, shindano kimataifa?

Sura mbaya siioni

Kote nimeshaangalia, ni uzuri waenea,
Wakilishi watimia, hesabu haijapungua,
Waliokwishateuliwa, na ukubwa wakapewa,
Siioni sura mbaya, barazani kutokea.

Wakubwa wanachagua, malaika walokua,
Urulaini radhia, dunia waliopewa,
Watutungia sheria, mashaalah naitoa,
Siioni sura mbaya, barazani kutokea.

Ila ninavyojua, akili wanaojaliwa,
Sura hawajajaliwa, bahati ikitokea,
Ila mamisi najua, bandia washindiliwa,
Siioni sura mbaya, barazani kutokea.

Hili ninalishangaa, malaika walokua,
Nani anawachagua,kwa jinsi wafanania,
Utadhani pacha pia,kumbe hawana jamaa,
Siioni sura mbaya, barazani kutokea.

Sura mviringo hua, na umbo wastania,
Hakuna lakuzidia, na macho wamejaliwa,
Mwanamme huumia, sio changu nikijua,
Siioni sura mbaya, barazani kutokea.

Hawa ndio wanafaa, yetu kuzungumzia,
Au roho warushia, na pepo wazipepea,
Hili sipati kujua, ila wapo wanaojua,
Siioni sura mbaya, barazani kutokea.

Baraza imejaliwa, harufu za kuvutia,
Mavazi ya maridhia, kila rangi zinang'aa,
Ila hoja sijazijua,ukame nahisi kua,
Siioni sura mbaya, barazani kutokea.

Ila kuigilizia, hilo sijalibishia,
Na kasuku huambiwa, sawasawa kurudia,
Ni fotokopi murua, wakubwa kuzitumia,
Siioni sura mbaya, barazani kutokea.

Dada nawahurumia, sura wasiojaliwa,
Chama hiki mtaloa,hawatawafikiria,
Sura usipojaliwa,kingine ni kuhamia,
Siioni sura mbaya, barazani kutokea.

Nyie wenye sura mbaya, undeni chama kipya,
Huenda mkatokea, nafasi kuichukua,
Ya haki iliyokuwa, na wala si ya kupewa,
Siioni sura mbaya, barazani kutokea.

Macho nimewafumbua, wenyewe kuogelea,
Bahari wametifua, majini waso shujaa,
Nuksi zakaribia, lazima kuwashtua,
Siioni sura mbaya, barazani kutokea.

Mkubwa hasemi uongo

Wazee wamenambia, radhi napaswa kutoa,
Wadai nimekosea, mkubwa kumdhania,
Wao wanavyoelewa, haiwi linalodaiwa,
Mkubwa huongopewa, abadani haongopi!

Hilo nimezingatia, naapa kutorudia,
Sasa nimeshalijua, sintalizungumzia,
Kauli nitaitumia, kulingana ilokuwa,
Mkubwa huongopewa, abadani haongopi!

Uongo hatotumia, ukubwa alojaliwa,
Ila aliyelaaniwa, na wanaomfuatia,
Ila nilivyoambiwa, mkubwa huongopewa,
Mkubwa huongopewa, abadani haongopi!

Na wanaomwongopea, ajenda hatoijua,
Hadi chali amekuwa, au kutokujitambua,
Pale akiambiwa, pembeni sasa sogea,
Mkubwa huongopewa, abadani haongopi!

Ukubwa juu hupaa, chini muhali tembea,
Na wanachokitambua, ni kula pia kupewa
Mikononi vikijaa, adimu kujitambua,
Mkubwa huongopewa, abadani haongopi!

Watu tumbo kuchumia, ndivyo walivyozaliwa,
Ya wengine kuwasumbua,hayo hawakuzoea,
Ubinafsi huwajaa, kuzidi hayawania,
Mkubwa huongopewa, abadani haongopi!

Hao wanaomsadia, ndio wanaotuhadaa,
Ya kwao kujichumia, na nafsi kulindia,
Mkubwa wakamzidia,mikenge akaivaa,
Mkubwa huongopewa, abadani haongopi!

Ukubwa unapokua, vibarakala huzua,
Matumbo miungu huwa, yakaanza abudiwa,
Nafsi hubarikiwa, utukufu zikapewa,
Mkubwa huongopewa, abadani haongopi!

Kombakomba huzaliwa, kama kupe vile huwa,
Mwilini huning'inia, kwa wakubwa walokua,
Na wengine jibwa huwa, kumlinda alokuwa,
Mkubwa huongopewa, abadani haongopi!

Hao ndio huchagua, lipi afaa sikia,
Na adha kumwepushia, mabaya kutosikia,
Mtu kipofu akawa, kwenye yake tasnia,
Mkubwa huongopewa, abadani haongopi!

Bubu na kiziwi hua,awe asiyeyajua,
Karibu yanayotokea, nayo ya mbali pia,
Dunia humpitia, yakama keshajifia,
Mkubwa huongopewa, abadani haongopi!

Thursday, November 24, 2011

Mwapenda msichoona?

Kaimu naishangaa, kupenda kisichokua,
Karibu kilichokua, kuacha kuangalia,
Fimbo ya mbali kuua, nyoka wasiyemjua,
Mwapenda msichoona, pendeni mnachoona!

Ndani walioingia, wanazidi kuchukiwa,
Kama vile ndege hua, mwituni anayepaa,
Zaidi athaminiwa, si tunduini alokaa,
Mwapenda msichoona, pendeni mnachoona!

Watu moyo huumia, kwa wanachokumbukia,
Na kile walichoshikilia, vigumu kuthaminiwa,
Na cha mbali huliliwa, cha ndani kuhujumiwa,
Mwapenda msichoona, pendeni mnachoona!

Laiti wangelijua, tunaowahurumia,
Ubishi wanaozua, na talaka kulilia,
KIsa wanahadaiwa, na hao wapita njia,
Mwapenda msichoona, pendeni mnachoona!

Pendo linalokufaa, si la ndoto kuotea,
Ni pendo lakushikilia, mikononi kulitia,
Kutomasa likakua, kila siku kuchanua,
Mwapenda msichoona, pendeni mnachoona!

Bora ni ulichopewa, sio cha kutarajia,
Kile unachokilea, kikaja nawe kukufaa,
Kwingine kisikotulia, ila ulipokaa,
Mwapenda msichoona, pendeni mnachoona!

Mengi twaangalia, kisha kuyafutulia,
Ku'delete' wanambia, neno wamelisanzua,
Moyo daima kutua, ukajenga mazoea,
Mwapenda msichoona, pendeni mnachoona!

Na mnavyosimulia, kama vile mnalia,
Machoni kisichokuwa, kizuri sana kikawa,
Ila kikija jongea, hapo huwa ni balaa,
Mwapenda msichoona,pendeni mnachoona!

Wadudi namwinamia, mapenzi kuniridhia,
Nitosheke na dunia, zaidi kutolilia,
Niwe mwepesi kutoa, na mzito kupokea,
Mwapenda msichoona, pendeni mnachoona!

Wednesday, November 23, 2011

Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

VITA mnavyikimbia, waoga mmeshakua?
Mwawaje ni kina hawa, au mlituhadaa?
Kiume mlivyovaa, vingine kuwadhania?
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Katiba vita radhia, kila mtu kuingia,
Washairi mwatakiwa, mengi kuzungumzia,
Ili wapate kujua, hao wasiyoyajua,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Iliyopo kuzingatia, chimbuko la Tanzania,
Na mamlaka kujua,sasa nani atakua,
Naye kumpigania, hadi ukubwa kutwaa,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Na mkubwa twamjua, mwenyewe Mtanzania,
Si rais alokua, wala chama chake pia,
Ni mimi na wewe pia, ukuu tunaopewa,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Ni katiba yaamua, sio ninawaongopea,
Ila kinachotokea, katiba yapinduliwa,
Ukubwa wasiopwa, wataka kutuchezea,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Rais anatakiwa, hili kulizingatia,
Si mambo kujifanyia, kama kweli hajajua,
Na kisha kusingizia, waongo wasiokua,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Rais ni Mtanzania, hakuna wa kumzidia,
Ila katiba yakataa, juu ya wengine kua,
Kwenye kuiandaa, katiba yetu mpya,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Kusalimu kuamua, amri mmeshapewa,
Mzaha kwenu hatia, mashtaka mtazua,
Au mkajachukiwa, nchi kuingia makiwa,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Vyama vyote navyo sawa, hakuna kuteuliwa,
Chini kushuka murua, juu waliotangulia,
Tuzungumze raia, nchi tunayokusudia,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Ni heri kuzungumzia, tuliyoyakusudia,
Hata miezi ikiwa, mradi huru tukawa,
Tunakotoka kujua, na twendako kutambua,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Uzazi sio mzaha, wengi patashika hua,
Machungu kuvumilia, hadi mwana akazaliwa,
Na katiba kuizaa, ndivyo hivyo 'navyokua,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Na katiba kuizaa, ndivyo hivyo 'navyokua,
Mwana kilema si dua, uzima twatarajia,
Na bora kilichokua, kiumbe kikitokea,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

VITA mnavyikimbia, waoga mmeshakua?
Mwawaje ni kina hawa, au mlituhadaa?
Kiume mlivyovaa, vingine kuwadhania?
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Katiba vita radhia, kila mtu kuingia,
Washairi mwatakiwa, mengi kuzungumzia,
Ili wapate kujua, hao wasiyoyajua,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Iliyopo kuzingatia, chimbuko la Tanzania,
Na mamlaka kujua,sasa nani atakua,
Naye kumpigania, hadi ukubwa kutwaa,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Na mkubwa twamjua, mwenyewe Mtanzania,
Si rais alokua, wala chama chake pia,
Ni mimi na wewe pia, ukuu tunaopewa,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Ni katiba yaamua, sio ninawaongopea,
Ila kinachotokea, katiba yapinduliwa,
Ukubwa wasiopwa, wataka kutuchezea,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Rais anatakiwa, hili kulizingatia,
Si mambo kujifanyia, kama kweli hajajua,
Na kisha kusingizia, waongo wasiokua,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Rais ni Mtanzania, hakuna wa kumzidia,
Ila katiba yakataa, juu ya wengine kua,
Kwenye kuiandaa, katiba yetu mpya,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Kusalimu kuamua, amri mmeshapewa,
Mzaha kwenu hatia, mashtaka mtazua,
Au mkajachukiwa, nchi kuingia makiwa,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Vyama vyote navyo sawa, hakuna kuteuliwa,
Chini kushuka murua, juu waliotangulia,
Tuzungumze raia, nchi tunayokusudia,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Ni heri kuzungumzia, tuliyoyakusudia,
Hata miezi ikiwa, mradi huru tukawa,
Tunakotoka kujua, na twendako kutambua,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Uzazi sio mzaha, wengi patashika hua,
Machungu kuvumilia, hadi mwana akazaliwa,
Na katiba kuizaa, ndivyo hivyo 'navyokua,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Na katiba kuizaa, ndivyo hivyo 'navyokua,
Mwana kilema si dua, uzima twatarajia,
Na bora kilichokua, kiumbe kikitokea,
Mkowapi washairi, nchi kuipigania?

Tumeweza ufisadi, tunajaribu urongo.

Uongo tunajaribu, ufisadi tumeweza,
Wananchi kuwaghilibu, ili sisi kupendeza,
Wadhanie tu dhahabu, na wengine kapi chaza,
Tumeweza ufisadi, tunajaribu urongo.

Wakubwa wanahatibu, moyoni wasowekeza,
Linawamaliza gubu,na hasadi kuwaponza,
Muumba wamjaribu, naye hawatamuweza,
Tumeweza ufisadi, tunajaribu urongo.

Hata na akina babu, kwalo hili wanyamaza,
Uchama wawaadhibu, taifa walipoteza,
Na vichwa wenye harabu, jema wanalitangaza,
Tumeweza ufisadi, tunajaribu urongo.

Uongo waujaribu, malengo kuyapoteza,
Wa janibu na ghaibu, hakika wawashangaza,
Waonwa kitu cha ajabu, wengine kuwapakaza,
Tumeweza ufisadi, tunajaribu urongo.

Wameyakosa majibu, kwani si watu wa kuwaza,
Hawana haya na aibu,wananchi wawachuuza,
Na makubwa masahibu,katiba waigeuza,
Tumeweza ufisadi, tunajaribu urongo.

Katiba ina majibu, na hayamo kwenye giza,
Wananchi ndio habibu, mamlaka yatangaza,
Si rais na mahbubu,wapaswao kuyafanza,
Tumeweza ufisadi, tunajaribu urongo.

Si rais na mahbubu,wapaswao kuyafanza,
Ni wananchi taratibu, watakiwa kutangaza,
Kwa kuwatumia naibu,kazi watakaoagizwa,
Tumeweza ufisadi, tunajaribu urongo.

Tume tukitaadabu, mkuu hatoifanza,
Atawaachia sulubu, wananchi kuitengeza,
Uchama usighilibu, kwa ajizi na mafunza,
Tumeweza ufisadi, tunajaribu urongo.

Twaisetiri aibu, haya si kwa Kiingereza,
Kajifunzeni adabu, au tutawapatiliza,
Watanzania kwa ghibu, sasa hamtawacheza,
Tumeweza ufisadi, tunajaribu urongo.

Msifikiri mabubu, kwa magadi kuwasuuza,
Hakuna kwao ajabu, mkishindwa kuongoza,
Watafanya mjarabu, nchi ikajapendeza,
Tumeweza ufisadi, tunajaribu urongo.

Tuesday, November 22, 2011

Nilinde

Ulinde ulimi wangu, usidhuru viungo vyangu,
Na linda mkono wangu, usiwadhuru wenzangu,
Ilinde akili yangu, isitamani Uungu,
Naulinde moyo wangu, nisitamani vya wenzangu,
Nahami fikra zangu, nisiige ya wenzangu,
Yalinde mawazo yangu, yasiwe husuda kwangu,
Na kihami chakula changu, kisije kuwa njaa yangu,
Na mlinde mke wangu, asiwe kifo cha utu wangu,
Na waokoe wanangu,wasiwe machungu yangu,
Nilinde jamaa zangu, wasiwe zahama yangu,
Nilinde na wafuasi wangu,wasiwe mashaka yangu,
Na yatunze maji yangu, yasije kuwa sumu kwangu,
Ulinde uongozi wangu. usiwe mauti kwa wenzangu,
Usifanze ukubwa wangu,uwe mwisho wa chama changu,
Ponya ubinafsi wangu,usiwe ndio mauti yangu!

Monday, November 21, 2011

Birigiji

Kitamba kishachoka, imebaki mazoea,
Rangi inafutika, chazidi kufubaa,
Ukata umenishika, siwezi tena nunua,
Birigiji imechoka, njano imeshapotea!

Wale niliowashika, uchuro wanichulia,
Tayari wanshanizika, wangoja kunifukia,
Utajiri nilozika, waje kuufukua,
Birigiji imechoka, njano imeshapotea!

Miguu inachanika, magoti yanatitia,
Watu wakereheka, hawataki niangalia,
Na sasa nimeishika, dhana ya kunyanyapaa,
Birigiji imechoka, njano imeshapotea!

Ila siachi kucheka, kila nikiwaangalia,
Hukumu wanaoweka, hivi itanifikia,
Au wao kuwafika, nami nashuhudia?
Birigiji imechoka, njano imeshapotea!

Laiti ningebahatika, ukweli nikaujua,
Ni moja tu ningeshika, hadi juu nikapaa,
Ninabaki nateseka, johari sijavumbua,
Birigiji imechoka, njano imeshapotea!

Jaha haikunitaka, toka nilipozaliwa,
Kazi kushughulika, riziki kuokotea,
Zao halitaniweka, ila mwenyewe kuvua,
Birigiji imechoka, njano imeshapotea!

Binzari njano na nyekundu

Mbona ya kwako manjano, hali yangu ni nyekundu,
Hapanao uwiano, au huu ni utundu?
Ni tofauti unono, au vyote ni chachandu?
Binzari yangu njano, mbona ya kwako nyekundu?

Au ni wangu uono, na na rangi hii utandu,
Ikiwa hauna meno, vipi utafune nundu,
Hujui piga piano, vipi usiwe kingwendu?
Binzari yangu njano, mbona ya kwako nyekundu?

Mia sio miatano, chururu ni bandubandu,
Uvimilivu kivuno, waridhikao matandu,
Nayo mafuta ya mbono, hayajawa ya ukindu,
Binzari yangu njano, mbona ya kwako nyekundu?

Mwulize Haji Machano, aliyeishaumwa na tandu,
Sijui hili agano, la manjano na wekundu,
Naona ni utengano, wewe na jambia mimi mundu,
Binzari yangu njano, mbona ya kwako nyekundu?

Siwezi sema si neno, ananielewa Pandu,
Keshaniunga mkono, anaitumia Jandu,
Waogopa kisonono, ukimwi wafanza utundu?
Binzari yangu njano, mbona ya kwako nyekundu?

Bilauri

Menginey bighairi, ufanisi kuchagua,
Hakuna linalojiri, ila kwa kupiga hatua,
Na waliotasawari, hili vyema walijua,
Nusu tupu bilauri, au nusu imejaa ?

Mwenye kutafuta kheri, daima utamgundua,
Namna anavyofikiri, ni nusu imepungua,
Na shari mkusudia, ni kabisa haijajaa,
Nusu tupu bilauri, au nusu imejaa ?

Kudra mwenye hiari, Mola atamwangazia,
Ismu haachi kariri, njiaze anamopitia,
Ilmu ataviinjari, na dahari si dunia,
Nusu tupu bilauri, au nusu imejaa ?

Ilmu atavinjari, Alamu keshamwambia,
Hili kwake si ghururi, ni ndia iloandaliwa,
Abadani si kafiri, kukufuru anojua,
Nusu tupu bilauri, au nusu imejaa ?

Na wengine hushauri, kutopotosha kujaa,
Mithili huikariri, nusu kitu kimejaa,
Ni rahisi kufikiri, ila gumu kutumia,
Nusu tupu bilauri, au nusu imejaa ?

Ingelikuwa safri, nusu njia kufikia,
Atazituma habari, fikio akaribia,
Inshallah kwa saburi, hatimaye kuingia,
Nusu tupu bilauri, au nusu imejaa ?

Ingekuwa utajiri, upungufu hatojua,
Atamsifu Qahari, kitu hajapungukiwa,
Ni mzima wa bukheri, na mengi kamjalia,
Nusu tupu bilauri, au nusu imejaa ?

Mtawala hudhihiri, Muumba kumwangukia,
Na kila akifikiri, hutosheka alopewa,
Ukubwa ataghairi, zaidi akakataa,
Nusu tupu bilauri, au nusu imejaa ?

Iweje kwangu mshairi, hili kutolitambua,
Tayari nimeshakiri, jambo kulikubalia,
Sio ya kwangu dhamiri, ukweli kuupindua,
Nusu tupu bilauri, au nusu imejaa ?

Mitumba ya nguo, sasa ya kila kitu....

Hamsini kutimia, Tanzania twaendelea?
Au nyuma twasogea, hili bado sijajua,
Lakini ninachokijua, gurudumu lakataa,
Tulianza mtumba nguo, sasa hata ndege pia !!

Mkoloni kachukua, akili zilizobakia,
Badala kujitambua, sasa tunajiumbua,
Badala ya kuvumbua, sasa twaanza fukua,
Tulianza mtumba nguo, sasa hata ndege pia !!

Elimu zimepotea, ujuzi wazidi via,
Tunachojitengenezea, ni wizi wa kubakua,
Nalilia Tanzania, kaburini kujitia,
Tulianza mtumba nguo, sasa hata ndege pia !!

Watu wetu twawajua, vibovu walishanunua,
Na mikataba wakatia, vilivyokuwa vya hewa,
Ikiongoza sanaa, nchi jangwa hubakia,
Tulianza mtumba nguo, sasa hata ndege pia !!

Wapo watu wa dunia, kazi hawajaajiriwa,
Vitu hivi wanajua, kutengeza kwa hatua,
Letu kuwafuatilia, ajira kuwapatia,
Tulianza mtumba nguo, sasa hata ndege pia !!

KIsha elimu kuzua, yenye mengi manufaa,
Iwe inayodhamiria, kitu kututengenezea,
Kitu hicho kikifaa, nchi itazidi jongea,
Tulianza mtumba nguo, sasa hata ndege pia !!

Haya yote ni nazaa, mitumba kuinunua,
Hapa twatangazia, MV Bukoba nyingi kuzaa,
Na Spice Islander pia,maelfu kuuawa,
Tulianza mtumba nguo, sasa hata ndege pia !!

Ndege juu zikipaa, za mtumba zitakuwa,
Kama Kongo itakua, kuanguka na kuua,
Kilio kikubwa kuwa, na laana kusambaa,
Tulianza mtumba nguo, sasa hata ndege pia !!

Hawa wanaoshupaa, lao wanaliazimia,
Huenda twajipalia, wa moto mkubwa mkaa,
Na hao kujivunia, pasenti wanazojua,
Tulianza mtumba nguo, sasa hata ndege pia !!

Mabomu tutauziwa, ya Mbagaala kumbukia,
Ila haya yatulia, mpaka ukitumia,
Kisha huharibikiwa, kisha kuchanganykiwa,
Tulianza mtumba nguo, sasa hata ndege pia !!

Sheria tunazijua, kwa tunavyozi pindua,
Hawana la kutwambia, mkenge weshatutia,
Mikosi twaingojea, na misiba na balaa,
Tulianza mtumba nguo, sasa hata ndege pia !!

Ni heri ukazaliwa, taahira ulokuwa,
Kuliko Mtanzania, rahisi kumhadaa,
Na kimya kutulia, hata mauti kumvaa,
Tulianza mtumba nguo, sasa hata ndege pia !!

Vyuo vikuu vyajaa, nini wanachosomea,
Kutengeza wasojua, hadi mtumba kununua?
Dunia yatushangaa, mizubao tulivyokuwa
Tulianza mtumba nguo, sasa hata ndege pia !!

Fisadi wafurahia, mavuno wategemea,
Na kampuni watazua, zingine zitoke Ulaya,
Watoto walikokuwa, na makuadi kutumia,
Tulianza mtumba nguo, sasa hata ndege pia !!

Historia twangojea, kuja kutushuhudia,
Bure kulialia, wakubwa wameshaamua,
Mungu atawaangazia, ya kwake kuwatunukia,
Tulianza mtumba nguo, sasa hata ndege pia !!

Na kinachofuatia, kizazi nasikitikia,
Mzigo kuuchukua, vifaa vilivyochakaa,
Kama reli ilivyokuwa, na zetu za simu njia,
Tulianza mtumba nguo, sasa hata ndege pia !!

Mchanga karata

ANA jozi ya pakiti, mchanga karata mwivi,
Anafanya tashtiti, wala sitii chumvi,
Twamtaka mwenyekiti, ambe aache ujuvi,
Mchanga karata mwivi, ana jozi ya pakiti.

Katufanya kaimati, hazigwai hata mvi,
Au sie matikiti, au mchana walevi,
Kikaagoni hauketi, hatujakua uduvi,
Mchanga karata mwivi, ana jozi ya pakiti.

Twamshikia manati, hayeeshi hivi hivi,
Kokoto tutamseti, aone mambo ni hevi,
Kweli hatumeremeti, ila hatunuki mavi,
Mchanga karata mwivi, ana jozi ya pakiti.

Yeye hatujamsaliti, wala kumwiita govi,
Vinginevyo hatupeti, twachanga bila ugomvi,
Mchanga karata mwivi, ana jozi ya pakiti.

Picha yake siipati, kisa yeye kuwa hivi,
Na maana haileti, naona geni jamvi,
Yumkini afriti,kampa wake ulevi,
Mchanga karata mwivi, ana jozi ya pakiti.

Alilolivaa koti, linalinda wake wivi,
Wadhani mtanashati, kumbe mkubwa mchimvi,
Keshabwagia na toti, chakari mpaka mvi,
Mchanga karata mwivi, ana jozi ya pakiti.

Achemshaye makuti, atambue hayaivi,
Na kiti ni cha kuketi, wala sio cha uvuvi,
Dogo wewe hulikuti, japo huanza kiwavi,
Mchanga karata mwivi, ana jozi ya pakiti.

Asemwe kwenye wavuti, wote wamjue mwivi,
Akakaa katikati, la ulimwengu jamvi,
Hata akiwa smati, atemee mate mwivi,
Mchanga karata mwivi, ana jozi ya pakiti.

Jumbe kichukue kiti, tumtete wetu mwivi,
Hata kama ana suti,isitufanye walevi,
Tumsute na kumseti, akomeshe wake wivi,
Mchanga karata mwivi, ana jozi ya pakiti.

Sheria isoandikwa

Laanatullahi kua, jamii wanaohadaa,
Hata Kurani yatoa, mwongozo sahihi kua,
Kuandika yafaa, ushahidi manufa,
Sheria isoandikwa, si sheria usanii!

Haki wanaoziua, kuandika hukataa,
Siri watawaambia, ili wapate kwibia,
Hili nani hajajua, ila walo makataa,
Sheria isoandikwa, si sheria usanii!

Kila jambo inafaa, kimaandishi likawa,
Vinginevyo kutania, tena mkubwa mzaha,
Wajua wanasheria, baadhi wajisheua,
Sheria isoandikwa, si sheria usanii!

Cheo wanakitetea, binafsi manufaa,
Ila sio Watanzania, kikweli kuwakwamua,
Isoandikwa sheria, mahakama hukataa,
Sheria isoandikwa, si sheria usanii!

Mazingira waandaa, utata unaozua,
Mafuu haya wajua, sembuse wazima walokua?
Hekima kuzingatia, yaliyokwishajaribiwa,
Sheria isoandikwa, si sheria usanii!

Twashindwa kuwaelewa, vyeo waliotunukiwa,
Akili watuchezea, kama wanaotumiwa,
Au shaitwani raia, mshauri mkuu kawa?
Sheria isoandikwa, si sheria usanii!

Misahafu kuchukua, na kanuni kuzijua,
Karne yanukuliwa, visa na mikasa pia,
Ubovu wanaoujua, pua walishaangukia,
Sheria isoandikwa, si sheria usanii!

Nchi yetu yapotea, arijojo imekua,
Nani kuifuatia, aweze kuiokoa,
Nahofu kubwa balaa, akili kutotumia,
Sheria isoandikwa, si sheria usanii!

Hujali mgonjwa, unajali maiti?

Mgonjwa hukumjali, unajali kwenda zika,
Ni saa kumi na mbili, kilioni unafika,
Hukumjulia hali, kumsindikiza wataka?
Hukumjali mgonjwa, unajali kwenda zika?

Yaonekana ni hili, ulilokuwa wataka,
Ndotoyo sasa kamili, unawahi kwenda zika,
Kaburi halina mwali,kila mja lamtaka,
Hukumjali mgonjwa, unajali kwenda zika?

Mtazame mswahili, tabiaye ni mikiki,
Kimbelembele kikweli, hata pawe hahusiki,
Ila sio hospitali, mauti hyadiriki,
Hukumjali mgonjwa, unajali kwenda zika?

Mgonjwa humwacha hali huduma astahiki,
Ila kwenda kula wali, siku ya mazishi haki,
Mila hii si akili, na wala sijaiafiki,
Hukumjali mgonjwa, unajali kwenda zika?

Ukweli naukabili, siogopi unafiki,
Ninaliona dhalili, tena lenye ushiriki,
Asiyekuwa na mali, ndio kabisa hawafiki,
Hukumjali mgonjwa, unajali kwenda zika?

Majilisi kulihali, udhalimu zashiriki,
Hawataki jua hali, kwenye kifo wanafiki,
Tiketi au kibali, ni mazishi kuhakiki,
Hukumjali mgonjwa, unajali kwenda zika?

Usiponijua hali, usinizike sitaki,
Ni haramu si halali, siutaki unafiki,
Kilio chako si kweli, ni uchuro haumezeki,
Hukumjali mgonjwa, unajali kwenda zika?

Asiyenijua hali, kwangu amekwishafariki,
Marhum ilhali, kwa yakini huniziki,
Baki na wako ahali, mazishi yangu hufiki,
Hukumjali mgonjwa, unajali kwenda zika?

Vijiji na maendeleo

Hao watujiao, waje wanaojiamini,
Ziishe na ndoto zao, na usanii vijijini,
Twataka vitendo vyao, watatufanyia nini,
Twataka maendeleo, si hotuba vijijini!

Wajue matamanio, ya watu wa vijijini,
Kuwa na mipangilio, nani anafanya nini,
Isiwe maendeleo, hadithi ya maskini,
Twataka maendeleo, si hotuba vijijini!

Ni masoko tutakayo, kuuza hadi ugenini,
Nchi zituzungukao, tusiwe kizuizini,
Na yeu yote mazao, yafike bora sokoni,
Twataka maendeleo, si hotuba vijijini!

Na yeu yote mazao, yafike bora sokoni,
Na wengine wauzao, tukutanie njiani,
Huko Kenya watakao, njia safi waachieni,
Twataka maendeleo, si hotuba vijijini!

Msumbiji watakao, huru tuwe barabarani,
Zambia wapelekao, wasitiwe mashakani,
Rwanda na Burundi nao, iwe kama ni nyumbani,
Twataka maendeleo, si hotuba vijijini!

Kongo wote watakao, wayaelewe mkoani,
Mpunga uulimao, si tu wa hapa ndani,
Si kosa yako mazao, kuuzwa huko mpakani,
Twataka maendeleo, si hotuba vijijini!

Na kwa wingi wavunao, wapeleke Marekani,
Ulaya na nchi zao, wanunue duniani,
Uchina wayatakayo, tuuze kwa kujiamini,
Twataka maendeleo, si hotuba vijijini!

Ni yetu haya mazao, maji yatakayobaini,
Na ngano tuilimayo, umeme tutauwini,
Kahawa tuivunao, kuja jenga vijijini,
Twataka maendeleo, si hotuba vijijini!

Wenetu watotakao, ili kutafuta mjini,
Waanze kwa yetu mazao, biashara kusaini,
Wawwe wayapelekayo, kona zote duniani,
Twataka maendeleo, si hotuba vijijini!

Na wanavijiji wajao, waishi kama mjini,
Pasiwe wayakosayo, eti waishi shambani,
Ila watu wang'arao, kwa siha pia imani,
Twataka maendeleo, si hotuba vijijini!

Wanasiasa wa leo, hawatufai yakini,
Wataka ishi kileo, sisi twishi kizamani,
NI wao wajaliwao, sisi tuko taabuni,
Twataka maendeleo, si hotuba vijijini!

Wajua shida tunayo, watununua kwa thumuni,
Hakika sisi vimeo, ila hatujajibaini,
Tugeuke ni walao, kura tusimpe mzaini,
Twataka maendeleo, si hotuba vijijini!

Wale na watu wao, kwetu wakose thamani,
Tuwe tuwachukiayo, duniani na mbinguni,
Tusiwape tarajio,ila wawe lawamani,
Twataka maendeleo, si hotuba vijijini!

Na kura watuibiao, sheria tuzibaini,
Kukataa watuziao, kura kuwa ushahidini,
Hata wale watumwao, na dola ilio mjini,
Twataka maendeleo, si hotuba vijijini!

Demokrasia iwe kwao, inaishi vijijini,
Tuwe tuwaondoao, wafanyao uhaini,
Tupitishe maazimio, vinara bora kuwini,
Twataka maendeleo, si hotuba vijijini!

Kwetu kukipendwa kwanza

Kujipenda tumeshindwa, vipi mengine kuweza,
Naona uongo twaunda, ukweli hatutaweza,
Utakuwaje mkandwa, na mgongo hujabanza,
Kwetu kukipendwa kwanza, ustawi utaanza!

Vyaelea vilivyoundwa, iwe meli au meza,
Mjuzi aliyeshindwa, na siye anayeweza,
Na nchi bila kufundwa, majenzi haitaweza,
Kwetu kukipendwa kwanza, ustawi utaanza!

Sio mtu wa kupendwa, vitendo asiyeweza,
Kwa maneno ni kiwanda, kila kitu hutengeza,
Bali kwa kutofundwa,vitendo hataviweza,
Kwetu kukipendwa kwanza, ustawi utaanza!

Mwenetu akishapendwa, machungu atayaweza,
Akiki tukimranda, umma hatoupuuza,
Hulijua lipi ganda, na mbegu akaitunza,
Kwetu kukipendwa kwanza, ustawi utaanza!

Kushinda kama kushindwa, ni mwanzo wa kujifunza,
Walozaliwa watenda, hili halitawachuuza,
Na hata ukimponda, kusimama ataweza,
Kwetu kukipendwa kwanza, ustawi utaanza!

Mwana ataka kufundwa, malezi yasomkwaza,
Na Mwenyezi akimpenda, nuru itamwongoza,
Hatohitaji kupendwa, mambo makubwa kufanza,
Kwetu kukipendwa kwanza, ustawi utaanza!

Twaona wanavyojipinda, na mengi hawataweza,
Adili wameisunda, wataka fanza uweza,
Muunda huwa muundwa, dunia kumchakaza,
Kwetu kukipendwa kwanza, ustawi utaanza!

Wanasema wawapendwa, wale watakaowekeza,
Mzawa wamemganda, kila siku kumchuza,
Na wanawe wawakwinda, elimu wanawakwaza,
Kwetu kukipendwa kwanza, ustawi utaanza!

Mola wangu kuwafunda, wanangu sintoliweza,
Wa mwanzo na mziwanda, Hafeez ninakutunza,
Walee unavyopenda, na wawe wenye kuweza,
Kwetu kukipendwa kwanza, ustawi utaanza!

Ni wewe wa kuwapenda, mimi hilo sintoweza,
Naomba changu kibanda, utawa kuja ufanza,
Na ibada kuiganda, tarafu ninayoweza,
Kwetu kukipendwa kwanza, ustawi utaanza!

Friday, November 18, 2011

Aliamini

Bismillahi Yaghanii, ubeti ninaanzia,
Ningali yangu makani, ya Karimu Ijumaa,
Hili nimelibaini, na sasa ninalitoa,
Siogopi kuchukiwa, kwa kuwa aliamini!

Nikiwa aliamini, siogopi kuchukiwa,
Kusema kweli imani, hidaya walojaliwa,
Atanienzi Manani, na pepo kuniridhia,
Siogopi kuchukiwa, kwa kuwa aliamini!

Nawajua duniani, wagumu wa kusikia,
Wataka niyaamini, kwayo wanayonihadaa,
Kunifanya majinuni, thawabu wakanifutia,
Siogopi kuchukiwa, kwa kuwa aliamini!

Urongo sintaamini, Mola ninamhofia,
Duni makazi motoni, milele nitakokaa,
Nikifa duniani, peponi milele kukaa,
Siogopi kuchukiwa, kwa kuwa aliamini!

Kufa hapa duniani, hai pepo ninakua,
Na hili nalithamini, daima kuzingatia,
Simwachii shetani, njiani kuja potea,
Siogopi kuchukiwa, kwa kuwa aliamini!

Waipendao amani, uongo waukataa,
Huwaweka mashakani, utulivu kupotea,
Tembeeni ulimwenguni, ukweli mtajionea,
Siogopi kuchukiwa, kwa kuwa aliamini!

Waliokuwa rahani, amani imepotea,
Na sababu wabaini, hadaa zilizidia,
Na ahadi za ubani, udi zisizoujua,
Siogopi kuchukiwa, kwa kuwa aliamini!

Nijalie maskini, aliamini nikawa,
Pamoja na hali duni, nikawa wa kuaminiwa,
Mwislamu wa zamani, mmojawapo ikawa,
Siogopi kuchukiwa, kwa kuwa aliamini!

Niafikishe Manani, ya heri kunijalia,
Daima kuniongoa, nisje nikapotea,
Siratul kupitia, salama nami nikawa,
Siogopi kuchukiwa, kwa kuwa aliamini!

Ibilisi ashangaa

Profesa wa hadaa, ibilisi ashangaa,
Twamshinda Watanzania, kwa umbeya na hadaa,
Uzaini tunaulewa, malengo yetu yakawa,
Ibilisi ashangaa, uongo tulivyobobea.

Siasa zetu balaa, uongo tunavyotumia,
Viongozi wanajua,na bado waendelea,
Ni wagumu kutubia, watanguliza dunia,
Ibilisi ashangaa, uongo tulivyobobea.

Nini watatuambia, wakubwa waliokua,
Eti wabambikiwa, ukweli hawakujua,
Au ni wakubwa wabia, kwenye dhambi ya hadaa?
Ibilisi ashangaa, uongo tulivyobobea.

Watu tumekomalia, nafsi kuzipaua,
Na aushi ya hadaa, miaka isochukua,
Ovyo yanayodidimia, tetemeko 'kitekea,
Ibilisi ashangaa, uongo tulivyobobea.

Ukweli tunaujua, lakini twaukataa,
Maamuzi kuamua, Khafidi akachukia,
Hasara yetu ikawa, hadi mwisho wa dunia,
Ibilisi ashangaa, uongo tulivyobobea.

Uongo twautambua, bado twaukubalia,
Dhuluma ikaenea, kila kona kusambaa,
Wanyonge kumlilia Alaa ada ikawa,
Ibilisi ashangaa, uongo tulivyobobea.

Ibilisi asomea, kwayo tuliyobobea,
Mengine hakuyajua, hadi macho kumfumbua,
Elimu ajipatia, viumbe tuliojaliwa,
Ibilisi ashangaa, uongo tulivyobobea

Elimu ajipatia, viumbe tuliojaliwa,
Ibilisi amekuwa, mwanafunzi mwaminiwa,
Kutamba kunapungua, viumbe wamtangulia,
Ibilisi ashangaa, uongo tulivyobobea.

Kila anapoingia, sisi tunshapitia,
Na mwengine yamwia, vigumu sana kujua,
Abakia ashangaa, cheo tulichojipatia,
Ibilisi ashangaa, uongo tulivyobobea.

Ushamba tumemtoa, wamjini twaingia,
Na pindi tukiziwa, nguvu tutatumia,
Naye kumgeukia, kuja kutusaidia,
Ibilisi ashangaa, uongo tulivyobobea.

Mwanadamu ninalia, k.o. kujipatia,
Ibilisi kumtoa, raundi mwanzo ilokuwa,
Na sasa twaendelea, taji kubwa kujapewa,
Ibilisi ashangaa, uongo tulivyobobea.

Zawadi ya udhalimu

Hili si utaalamu, wala hadithi yabisi,
Aelewa mwanadamu, hedaya yake maasi,
Mkuu wa mahakimu, kaukana ni najisi,
Zawadi ya udhalimu, ni nuksi na mikosi!

Akiwa mwongo imamu, maamuma muflisi,
Na wanaotakadamu, huishi kwa wasiwasi,
Haitulii kaumu, madhali kuna nakisi,
Zawadi ya uzaini, ni nuksi na mikosi!

Kadiri kitu muhimu, nayo yataka kiasi,
Wanatwambia walimu, kitu hiki ni balansi,
Mahala isipodumu, sio njema majilisi,
Zawadi ya udhalimu, ni nuksi na mikosi!

Si taabu kwa Alimu, aliye bora Qudusi,
Jambo hili kaukumu, alipoasi Ibilisi,
Na hadi leo ladumu, kwa ngumbaru na mamajusi,
Zawadi ya uzaini, ni nuksi na mikosi!

Wala halinayo zamu, wala nusu na sudusi,
Hili jambo la kiamu, wengi huwa lawaghasi,
Na wakubwa madhalimu, huwatoa makamasi,
Zawadi ya udhalimu, ni nuksi na mikosi!

Walopewa uadhimu, wakaiivua lebasi,
Wakalifanya haramu, halali kiujasusi,
Viumbe kuwadhulumu, na maovu kuasisi,
Zawadi ya uzaini, ni nuksi na mikosi!

Hukasirika Rahimu, akaishusha nuksi,
Dhiki isiwe admu, kwa balaa na mikosi,
Na nchi ikesha hamu, na kujaa kinamasi,
Zawadi ya udhalimu, ni nuksi na mikosi!

Waulize wakarimu, mambo wanaodadisi,
Walo huru na hadimu, aya wanazo fususi,
Wala haikugharimu, bure waweza durusi,
Zawadi ya uzaini, ni nuksi na mikosi!

Haramu na halali

NANI asiyetambua, haramu kilichokua,
Halali hakitozaa, ila kwa kubambikia,
Mwanaharamu akiwa, huachi kumgundua,
Haramu haitozaa, halali kilichokua.

Ndivyo dunia yajua, kinyumewe haijawa,
Haya ukifuatia, siri utaielewa,
Kila ukweli mchelea, huja yakamuumbua,
Haramu haitozaa, halali kilichokua.

Nadhiri sintoitoa, nikaja kujeruhiwa,
Nitokako sijajua, kilichokwishakutokea,
Na mwenye kujua haya, ni pekee adilia,
Haramu haitozaa, halali kilichokua.

Waweza kushupalia, uhalali kuulilia,
Hata ndani kuingia, sebuleni kutulia,
Bado utajafulia, chenyewe kukuumbua,
Haramu haitozaa, halali kilichokua.

Uongo utauzaa, na kisha kuulea,
Kisomo kukipatia, na daawa mashalaa,
Ila chako kisokuwa, hakitakuja kukurudia,
Haramu haitozaa, halali kilichokua.

Nasaba ina ulua, na sumaku yavutia,
Hazipishani tabia, na mwenendo hufatia,
Walo nje hutambua, chako na kisichokua,
Haramu haitozaa, halali kilichokua.

Ya mwongo ni fupi njia, na matuta yamejaa,
Na usipoangalia, meno waweza ng'olewa,
Na chini waliokaa, hujikuta wanaelea,
Haramu haitozaa, halali kilichokua.

Siri sintoifichua, uyusufu watakiwa,
Na waliokwishajaliwa, si muhali nakwambia,
Hapa nilipofikia, kisomo nishawapatia,
Haramu haitozaa, halali kilichokua.

Tuesday, November 15, 2011

Mkweli akiitwa mwongo

Ndivyo ilivyo dunia, waovu kusingizia,
Upofu watajitia, ukweli kutoujua,
Ni watu wa kuangamia, kwa dunia kutania,
Mkweli akiitwa mwongo, mrongo hujiumbua!!!



Mrongo hujiumbua, uongo akiuzua,
Na kisha kumpakazia, msafi aliyekuwa,
Hata mkubwa akiwa, ni mtu wa kumzomea,
Mkweli akiitwa mwongo, mrongo hujiumbua!!!

Laana waliovaa, ukweli huukataa,
Ili mradi wabwia, unga wa kukangamaa,
Lao kulipigania, japo laua raia,
Mkweli akiitwa mwongo, mrongo hujiumbua!!!

Wapo wezi wa vifaa, na wapo wa watu pia,
Ila hawa ni balaa, wanaoiba sheria,
Na katiba kupindua, usafi wakajitia,
Mkweli akiitwa mwongo, mrongo hujiumbua!!!

Na kisha kutangazia, umama kitu usojua,
Wanaharakati nia, na madhumuni mabaya,
Kuwa wamekusudia, umma kuupotoa,
Mkweli akiitwa mwongo, mrongo hujiumbua!!!

Wote ninawaambia, mmeishiwa waheshimiwa,
Mkenge mmeingia, na watu hamjawajua,
Ya leo Tanzania, ya jana haitakuwa,
Mkweli akiitwa mwongo, mrongo hujiumbua!!!

Umma mnaupindua, na katiba kuchakachua,
Na ukweli mnaujua, uchama mnatetea,
Nchi mwataka kugawa,kutawala kwendelea,
Mkweli akiitwa mwongo, mrongo hujiumbua!!!

Tumeshawashtukia, na Mola twamgeukia,
Wape wasichotarajia, ewe wetu mkuu Alaa,
Juu zaidi ulokua, chini wapate ingia,
Mkweli akiitwa mwongo, mrongo hujiumbua!!!

Wajua la kuwawia, na dua tunaitambua,
Usiku kuweka nia, na kisimamo kwingia,
Na masharifu na watawa, kufunga kwa hiyo nia,
Mkweli akiitwa mwongo, mrongo hujiumbua!!!

Kwanza kuwachambua, kwa uongo kutwambia,
Na kisha kusingizia, ni warongo wasokua,
Dhambi kuwajazia, kibaba chao kujaa,
Mkweli akiitwa mwongo, mrongo hujiumbua!!!

Fanya yao jumuia, Firauni ilokua,
Shamu wakishafkia, uje mwenyewe kuvua,
Na Mola mwenye kujua,ni haki utatumia,
Mkweli akiitwa mwongo, mrongo hujiumbua!!!

Afu twakutarajia, taifa kuliokoa,
Hao wanaojipendelea, ahera wangepigania,
Ili wapate tangulia, kama ukweli wajua,
Mkweli akiitwa mwongo, mrongo hujiumbua!!!

Wahitajika vijana, mapinduzi ya dunia.

IKIWA bado mwalala, mwahitajika vijana,
Mapinduzi yanakua, kwa usiku na mchana,
Marekani kuanzia, Ulaya sasa kwa sana,
Wahitajika vijana, mapinduzi ya dunia.

Viongozi twaonea, hawana wanalo sana,
Wao pia watumiwa, na mabepari wenye zana,
Makampuni ya dunia, ndiyo yanayotubana,
Wahitajika vijana, mapinduzi ya dunia.

Salamu mnatumiwa, changamkeni vijana,
Kuamka mwatakiwa, msifanze danadana,
Ni hatia kuchelewa, ntasgubdwa kuungana,
Wahitajika vijana, mapinduzi ya dunia.

Sitini yaliyotokea, wakashindwa ongozana,
Mfumo ukaendelea, hadi leo wasutana,
Sasa kinachotakiwa, kiongozi wa amana,
Wahitajika vijana, mapinduzi ya dunia.

Mabepari wa dunia, wao wameshaungana,
Wanazikwapua hazina, masikini twabakia,
Vibarakala watwana, nao wanawatumikia,
Wahitajika vijana, mapinduzi ya dunia.

Uwakilishi wavia, weshafanywa ni watwana,
Matumbo watumikia, sio wenu muamana,
Wenyewe msipojitoa, mtajaumizwa sana,
Wahitajika vijana, mapinduzi ya dunia.

Yaandamana dunia, ubepari wachukia,
Wazidi nuka hadaa, na kuvuja kwa usaha,
Ni ipo sasa nasaha, vijana watasikia?
Wahitajika vijana, mapinduzi ya dunia.

Hatima sijaijua, ila sianzi paua,
Ukuta sijanyanyua, sijui kama ntakaa,
Nayangoja majaliwa, kujua sikujaliwa,
Wahitajika vijana, mapinduzi ya dunia.

Hongereni wawakilishi

Hongereni wawakilishi

Ukweli tumeujua, ni wapi wanalalia,
Na mengi tumegundua, hata na zao hadaa,
Yakini tunatumiwa, wakubwa kuwajengea,
Hongereni wawakilishi, wa chama na serikali.

Kasri wajijengea, au kuja zinunua,
Kaburini kujengea, watakapotufukia,
Na minara yao kukua, dunia ikawajua,
Hongereni wawakilishi, wa chama na serikali.

Upande waliokua, madhali tunatambua,
Sasa twawasifia, vyeo wanshachukua,
Hongera kuwatupia, jinsi walivyonunuliwa,
Hongereni wawakilishi, wa chama na serikali.

Hongera twawatumia, wawakilishi nazaa,
Chama mwakisaidia, kiweze kutubagua,
Kutufanya ni majuha,hatuna tunalolijua,
Hongereni wawakilishi, wa chama na serikali.

Hongera wa kutununua, na kisha kujinunua,
Ila moto mkipewa, msije kutugaia,
Wenyewe kufurahia, nari mtakayojaliwa,
Hongereni wawakilishi, wa chama na serikali.

Macho wanaotufungua, wadaiwa kutuhadaa,
Nyie upofu mwatutia, ni vipi kuwatambua?
Ni Mola anayejua, naye atawazawadia,
Hongereni wawakilishi, wa chama na serikali.

Kusoma mnazidiwa, hoja zote zimepaa,
Kazi kushangilia, na vigelegele kubwia,
Wenyewe mmejichagua, nani amewachagua?
Hongereni wawakilishi, wa chama na serikali.

Nguo zetu mmevaa, ila wafu twawajua,
Ni wasiomsaidia, yule anayeteketa,
Ila humshindilia, akazidi angamia,
Hongereni wawakilishi, wa chama na serikali.

Wawakilishi hatuna

VYAMA huwa vyachukua, na wabunge wakwapua,
Ili fedha kujazia, kura wende zinunua,
Mwasema mmechaguliwa, kumbe mmejichagua?
Wawakilishi hatuna, wa wananchi Afrika.

Afrika ililaniwa, na sasa inalaniwa,
Mweupe keshapangua, mweusi ameingia,
Mkoloni nawambia, sio rangi kutambua,
Wawakilishi hatuna, wa wananchi Afrika.

Lengo lao kulijua, ukubwa kutoachia,
Wako tayari kuua, madarakani kubakia,
Na wizi wanatambua, ndio unaowasaidia,
Wawakilishi hatuna, wa wananchi Afrika.

Katiba watapindua, kwa hila kuzitumia,
Wananchi kuwahadaa, mbumbumbu wasiojua,
Jambo hili wamejaliwa, huwezi kuwafikia,
Wawakilishi hatuna, wa wananchi Afrika.

Afrika yaugua, maradhi yasotibiwa,
Na wanayoyachangia, viongozi walokuwa,
Kisa uroho na tamaa,mamlaka kung'ang'ania,
Wawakilishi hatuna, wa wananchi Afrika.

Nchi wanailangua, na haki wazichukua,
Na mabunge yamejaa, watu wa kuteuliwa,
Ili kuja kutumiwa, siku inayochaguliwa,
Wawakilishi hatuna, wa wananchi Afrika.

Muumba wetu radhia, tuangalie raia,
Ni wewe unayetwaa, na pia unayetoa,
Kikombe kutuondolea, mikosi kuikimbia,
Wawakilishi hatuna, wa wananchi Afrika.

Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Siasa zimefubaa, viranja vipofu kua,
Hawajali Tanzania, ya kwao wafikiria,
Sasa waanza tugawa, kabla hatujajigawa,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Hadaa nchi yavaa, vazi linalowapwaya,
Na wakubwa kwa tamaa, ukweli waushangaa,
Juu chini imekua, nchi haitoendelea,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Nchi tunaipindua, ukubwa twauchukua,
Rais sio raia, katiba kusimamia,
Ni ubabe watumiwa, na uzaini kuzaa,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Raia wa Tanzania, wenzao wangechagua,
Toka chini kutokea, uwakilishi kupewa,
Makundi kila jamaa, kujawawakilishia,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Mdau mmoja katwaa, kwa mabavu kutumia,
Haki ya kujiandikia, mswaada usiofaa,
Kisha kung'ang'ania, wabungewe kutumia,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Hili naona kinyaa, na sintolikubalia,
Kizazi nakiambia, katiba ijayo baa,
Na mkiikubalia, taifa litapotea,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Wachache waliokuwa, vipi sawa na wengi kua,
Laki tisa twaambiwa, Zanzibar walokua,
Kisha ukubwa wapewa, ya kwetu kuja amua?
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Zanzibar ni mkoa, kwa kimo na yake hatua,
Vinginevyo haujawa, ni pulizo lililojaa,
Msikubali mikoa, kuburuzwa na kisiwa,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Mikubwa yetu mikoa, Zanzibar yazidia,
Nayo ingelifaa, uwakilishi swa kua,
Dhuluma twaikataa, na Mola aitambua,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Waumini twashangaa, kuritadi wamekua,
Hili washangilia, kama wanaotumiwa,
Kidogo walichopewa, kikubwa kimeshakua,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Kizazi mwakisusia, wenyewe mwajiangalia,
Laana mnaichukua, na vizazi kufatia,
Wote mnaotuhadaa, ilhali mnajua,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Viziwi wa roho na moyo.

Ni heri ya kuzaliwa, kiziwi usiosikia,
Kuliko ya kuzaliwa, roho uliyepofua,
Hukuambaa dunia, ukadhani washikilia,
Viziwi si kwa sikio, ila kwa roho na moyo.

Roho isiposikia, mja huwa kafulia,
Viungo vingi huvia, moto vikiuhofia,
Hapana litalokua, vyote hujakusinyaa,
Viziwi si kwa sikio, ila kwa roho na moyo.

Moyo ukizuzuliwa, uwe usiosikia,
Huwa ni kubwa balaa, matamanio kukua,
Na iizidipo tamaa, hubaki kuangamia,
Viziwi si kwa sikio, ila kwa roho na moyo.

Na macho huyapofua, ishara kutozijua,
Zezeta nusu akawa, taahira kuzubaa,
Awe wa kuhurumia, mdomo anapofungua,
Viziwi si kwa sikio, ila kwa roho na moyo.

Moyo umenfiungua, wewe ulonichagua,
Haya ninafurahia, tena ninajivunia,
Na sifa kwako natoa, kingine sintochagua,
Viziwi si kwa sikio, ila kwa roho na moyo.

Si bora wa kuzaliwa, heshima wanipatia?
Kutosheka nimekua,na ukwasi sijajua?
Na milango wafungua,hata nisiyotarajia?
Viziwi si kwa sikio, ila kwa roho na moyo.

Naiombea Tanzania, viongozi kujaliwa,
Milki wanaojua, na ufalme usovia,
Hofu ikawaingia, na uongofu kuvaa,
Viziwi si kwa sikio, ila kwa roho na moyo.

Vipofu wanageuka

Kuona vigumu hua, licha macho nayo kuwa,
Hongozi ikizidia, hakuna asiyelewa,
Chakari wote hulewa, wanofanya kutojua,
Vipofu wanageuka, wazima walozaliwa.

Mungu akishachukia, shetani atamwachia,
Na mtu akadhania, ya kwamba amejaliwa,
Kumbe moto apalia,kwa mawe yanayoungua,
Vipofu wanageuka, wazima walozaliwa.

Motoni wengi huingia, vyeo waliojaliwa,
Kwa kushinda zingatia, haki za chini walokuwa,
Wachache wanojua,mkumbo wanafuatia,
Vipofu wanageuka, wazima walozaliwa.

Hoja watazisikia, wala hawataelewa,
Milango hufunguliwa, na hushindwa kuingia,
Huoneshwa hata njia, wasijue pa kuanzia,
Vipofu wanageuka, wazima walozaliwa.

Shetani huwatangulia, kwa yote wakiazimia,
Huwafanyia mzaha, nyikani wakapotea,
Waamini wanajua, kumbe maaluni wawa,
Vipofu wanageuka, wazima walozaliwa.

Sodom na Gomorrah, haya yalikwishatokea,
Ya haki walikataa, haramu wakalilia,
Ndiyo yanayotokea, viso halali mwapewa,
Vipofu wanageuka, wazima walozaliwa.

Kitanzi wakitungua, na sasa wanakivaa,
Dahari wategemea, wataendelea kuwa,
Ila Muumba ajua, kwanini mchwa apaa,
Vipofu wanageuka, wazima walozaliwa.

Nani wa kumtegemea, kama hutotusikia,
Mola wetu unajua, moyoni yaliyojaa,
Bure kukusimulia, jamala twaingojea,
Vipofu wanageuka, wazima walozaliwa.

Mkuu uliyekuwa, wa mbinguni na dunia,
Gumu halijatokea, ukashindwa kutatua,
Yasubiri Tanzania, hukumu kuiridhia,
Vipofu wanageuka, wazima walozaliwa.

Wahitajika vijana, mapinduzi ya dunia.

IKIWA bado mwalala, mwahitajika vijana,
Mapinduzi yanakua, kwa usiku na mchana,
Marekani kuanzia, Ulaya sasa kwa sana,
Wahitajika vijana, mapinduzi ya dunia.

Viongozi twaonea, hawana wanalo sana,
Wao pia watumiwa, na mabepari wenye zana,
Makampuni ya dunia, ndiyo yanayotubana,
Wahitajika vijana, mapinduzi ya dunia.

Salamu mnatumiwa, changamkeni vijana,
Kuamka mwatakiwa, msifanze danadana,
Ni hatia kuchelewa, ntasgubdwa kuungana,
Wahitajika vijana, mapinduzi ya dunia.

Sitini yaliyotokea, wakashindwa ongozana,
Mfumo ukaendelea, hadi leo wasutana,
Sasa kinachotakiwa, kiongozi wa amana,
Wahitajika vijana, mapinduzi ya dunia.

Mabepari wa dunia, wao wameshaungana,
Wanazikwapua hazina, masikini twabakia,
Vibarakala watwana, nao wanawatumikia,
Wahitajika vijana, mapinduzi ya dunia.

Uwakilishi wavia, weshafanywa ni watwana,
Matumbo watumikia, sio wenu muamana,
Wenyewe msipojitoa, mtajaumizwa sana,
Wahitajika vijana, mapinduzi ya dunia.

Yaandamana dunia, ubepari wachukia,
Wazidi nuka hadaa, na kuvuja kwa usaha,
Ni ipo sasa nasaha, vijana watasikia?
Wahitajika vijana, mapinduzi ya dunia.

Hatima sijaijua, ila sianzi paua,
Ukuta sijanyanyua, sijui kama ntakaa,
Nayangoja majaliwa, kujua sikujaliwa,
Wahitajika vijana, mapinduzi ya dunia.

Mungu atakalo huwa

Mola aliloamua, ndilo linalotokea,
Ila shetani hupewa, watu wa kuwachukua,
Uroho walojaa, na tadi kuwapofua,
Mungu atakalo huwa, sio atakalo mtu!

Tamaa walojaa, shetani huwatumia,
Mamlaka kukwapua, kwa ya kwao manufaa,
Sheria kujitungia, za dhuluma na hatia,
Mungu atakalo huwa, sio atakalo mtu!

Kamba hujakuachiwa, wenyewe kujinyongea,
Si manani kazubaa, itihari kawaachia,
Na nari haitochagua, kumeza wanaojizuzua,
Mungu atakalo huwa, sio atakalo mtu!

Watakaoshindania, kuitawala dunia,
Matamanio kuzaa, pepo yanayoiondoa,
Muumba hatachelewa, watakayo kuachiwa,
Mungu atakalo huwa, sio atakalo mtu!

Kiasi huwavumilia, hadi siku kuingia,
Wenyewe hujizodoa, huku wakilialia,
Milango ikifunguliwa, motoni wataingia,
Mungu atakalo huwa, sio atakalo mtu!

Na nchi ilolaniwa, kwa ufisadi na hadaa,
Mola hujawaridhia, wabaya kuwachagua,
Maovu waliojaa, na mema wasonukia,
Mungu atakalo huwa, sio atakalo mtu!

Muumba huwagawia, mnachokistahilia,
Vinginevyo mngepewa, wazuri walokuwa,
Sisi wenyewe raia, madhambi yametujaa,
Mungu atakalo huwa, sio atakalo mtu!

Sisi wenyewe raia, madhambi yametujaa,
Hata viongozi pia, wa dini waliokuwa,
Wote wenye roho mbaya, bwana tusomsujudia,
Mungu atakalo huwa, sio atakalo mtu!

Haya yanayotokea, wenyewe tumeandaa,
Budi kuyavumilia, huku toba tunaitoa,
Ili mola kutuvua, na hii ya wovu kofia,
Mungu atakalo huwa, sio atakalo mtu!

Masharifu na watawa, muanze kujitambua,
Muache nanyi tumiwa, mnaiongeza balaa,
Ni nani ataongoa, ikiwa nyie mwavia?
Mungu atakalo huwa, sio atakalo mtu!

Nzuri yetu Tanzania, ila Mola hatujamjua,
Nia yetu kwake mbaya, na bado avumilia,
Ila mwisho utatua, wingule kuliepua,
Mungu atakalo huwa, sio atakalo mtu!

Muumba kumrudia, bora kuliko kuchagua,
Mwaona mnavyopewa, uoza vilivyokua,
Na haya kuendelea, na nchi kudidimia,
Mungu atakalo huwa, sio atakalo mtu!

Neema tusipojua, mabaa tutayajua,
Mikosi na nuksi pia, tutafunga nazo ubia,
Haya yakawa ni njia, wenyewe tulochagua,
Mungu atakalo huwa, sio atakalo mtu!

Monday, November 14, 2011

Hongereni wawakilishi

Ukweli tumeujua, ni wapi wanalalia,
Na mengi tumegundua, hata na zao hadaa,
Yakini tunatumiwa, wakubwa kuwajengea,
Hongereni wawakilishi, wa chama na serikali.

Kasri wajijengea, au kuja zinunua,
Kaburini kujengea, watakapotufukia,
Na minara yao kukua, dunia ikawajua,
Hongereni wawakilishi, wa chama na serikali.

Upande waliokua, madhali tunatambua,
Sasa twawasifia, vyeo wanshachukua,
Hongera kuwatupia, jinsi walivyonunuliwa,
Hongereni wawakilishi, wa chama na serikali.

Hongera twawatumia, wawakilishi nazaa,
Chama mwakisaidia, kiweze kutubagua,
Kutufanya ni majuha,hatuna tunalolijua,
Hongereni wawakilishi, wa chama na serikali.

Hongera wa kutununua, na kisha kujinunua,
Ila moto mkipewa, msije kutugaia,
Wenyewe kufurahia, nari mtakayojaliwa,
Hongereni wawakilishi, wa chama na serikali.

Macho wanaotufungua, wadaiwa kutuhadaa,
Nyie upofu mwatutia, ni vipi kuwatambua?
Ni Mola anayejua, naye atawazawadia,
Hongereni wawakilishi, wa chama na serikali.

Kusoma mnazidiwa, hoja zote zimepaa,
Kazi kushangilia, na vigelegele kubwia,
Wenyewe mmejichagua, nani amewachagua?
Hongereni wawakilishi, wa chama na serikali.

Nguo zetu mmevaa, ila wafu twawajua,
Ni wasiomsaidia, yule anayeteketa,
Ila humshindilia, akazidi angamia,
Hongereni wawakilishi, wa chama na serikali.

Wawakilishi hatuna

VYAMA huwa vyachukua, na wabunge wakwapua,
Ili fedha kujazia, kura wende zinunua,
Mwasema mmechaguliwa, kumbe mmejichagua?
Wawakilishi hatuna, wa wananchi Afrika.

Afrika ililaniwa, na sasa inalaniwa,
Mweupe keshapangua, mweusi ameingia,
Mkoloni nawambia, sio rangi kutambua,
Wawakilishi hatuna, wa wananchi Afrika.

Lengo lao kulijua, ukubwa kutoachia,
Wako tayari kuua, madarakani kubakia,
Na wizi wanatambua, ndio unaowasaidia,
Wawakilishi hatuna, wa wananchi Afrika.

Katiba watapindua, kwa hila kuzitumia,
Wananchi kuwahadaa, mbumbumbu wasiojua,
Jambo hili wamejaliwa, huwezi kuwafikia,
Wawakilishi hatuna, wa wananchi Afrika.

Afrika yaugua, maradhi yasotibiwa,
Na wanayoyachangia, viongozi walokuwa,
Kisa uroho na tamaa,mamlaka kung'ang'ania,
Wawakilishi hatuna, wa wananchi Afrika.

Nchi wanailangua, na haki wazichukua,
Na mabunge yamejaa, watu wa kuteuliwa,
Ili kuja kutumiwa, siku inayochaguliwa,
Wawakilishi hatuna, wa wananchi Afrika.

Muumba wetu radhia, tuangalie raia,
Ni wewe unayetwaa, na pia unayetoa,
Kikombe kutuondolea, mikosi kuikimbia,
Wawakilishi hatuna, wa wananchi Afrika.

Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Siasa zimefubaa, viranja vipofu kua,
Hawajali Tanzania, ya kwao wafikiria,
Sasa waanza tugawa, kabla hatujajigawa,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Hadaa nchi yavaa, vazi linalowapwaya,
Na wakubwa kwa tamaa, ukweli waushangaa,
Juu chini imekua, nchi haitoendelea,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Nchi tunaipindua, ukubwa twauchukua,
Rais sio raia, katiba kusimamia,
Ni ubabe watumiwa, na uzaini kuzaa,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Raia wa Tanzania, wenzao wangechagua,
Toka chini kutokea, uwakilishi kupewa,
Makundi kila jamaa, kujawawakilishia,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Mdau mmoja katwaa, kwa mabavu kutumia,
Haki ya kujiandikia, mswaada usiofaa,
Kisha kung'ang'ania, wabungewe kutumia,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Hili naona kinyaa, na sintolikubalia,
Kizazi nakiambia, katiba ijayo baa,
Na mkiikubalia, taifa litapotea,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Wachache waliokuwa, vipi sawa na wengi kua,
Laki tisa twaambiwa, Zanzibar walokua,
Kisha ukubwa wapewa, ya kwetu kuja amua?
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Zanzibar ni mkoa, kwa kimo na yake hatua,
Vinginevyo haujawa, ni pulizo lililojaa,
Msikubali mikoa, kuburuzwa na kisiwa,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Mikubwa yetu mikoa, Zanzibar yazidia,
Nayo ingelifaa, uwakilishi swa kua,
Dhuluma twaikataa, na Mola aitambua,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Waumini twashangaa, kuritadi wamekua,
Hili washangilia, kama wanaotumiwa,
Kidogo walichopewa, kikubwa kimeshakua,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Kizazi mwakisusia, wenyewe mwajiangalia,
Laana mnaichukua, na vizazi kufatia,
Wote mnaotuhadaa, ilhali mnajua,
Muswada unatugawa, itakuwaje katiba ?

Viziwi wa roho na moyo.

Ni heri ya kuzaliwa, kiziwi usiosikia,
Kuliko ya kuzaliwa, roho uliyepofua,
Hukuambaa dunia, ukadhani washikilia,
Viziwi si kwa sikio, ila kwa roho na moyo.

Roho isiposikia, mja huwa kafulia,
Viungo vingi huvia, moto vikiuhofia,
Hapana litalokua, vyote hujakusinyaa,
Viziwi si kwa sikio, ila kwa roho na moyo.

Moyo ukizuzuliwa, uwe usiosikia,
Huwa ni kubwa balaa, matamanio kukua,
Na iizidipo tamaa, hubaki kuangamia,
Viziwi si kwa sikio, ila kwa roho na moyo.

Na macho huyapofua, ishara kutozijua,
Zezeta nusu akawa, taahira kuzubaa,
Awe wa kuhurumia, mdomo anapofungua,
Viziwi si kwa sikio, ila kwa roho na moyo.

Moyo umenfiungua, wewe ulonichagua,
Haya ninafurahia, tena ninajivunia,
Na sifa kwako natoa, kingine sintochagua,
Viziwi si kwa sikio, ila kwa roho na moyo.

Si bora wa kuzaliwa, heshima wanipatia?
Kutosheka nimekua,na ukwasi sijajua?
Na milango wafungua,hata nisiyotarajia?
Viziwi si kwa sikio, ila kwa roho na moyo.

Naiombea Tanzania, viongozi kujaliwa,
Milki wanaojua, na ufalme usovia,
Hofu ikawaingia, na uongofu kuvaa,
Viziwi si kwa sikio, ila kwa roho na moyo.

Vipofu wanageuka

Kuona vigumu hua, licha macho nayo kuwa,
Hongozi ikizidia, hakuna asiyelewa,
Chakari wote hulewa, wanofanya kutojua,
Vipofu wanageuka, wazima walozaliwa.

Mungu akishachukia, shetani atamwachia,
Na mtu akadhania, ya kwamba amejaliwa,
Kumbe moto apalia,kwa mawe yanayoungua,
Vipofu wanageuka, wazima walozaliwa.

Motoni wengi huingia, vyeo waliojaliwa,
Kwa kushinda zingatia, haki za chini walokuwa,
Wachache wanojua,mkumbo wanafuatia,
Vipofu wanageuka, wazima walozaliwa.

Hoja watazisikia, wala hawataelewa,
Milango hufunguliwa, na hushindwa kuingia,
Huoneshwa hata njia, wasijue pa kuanzia,
Vipofu wanageuka, wazima walozaliwa.

Shetani huwatangulia, kwa yote wakiazimia,
Huwafanyia mzaha, nyikani wakapotea,
Waamini wanajua, kumbe maaluni wawa,
Vipofu wanageuka, wazima walozaliwa.

Sodom na Gomorrah, haya yalikwishatokea,
Ya haki walikataa, haramu wakalilia,
Ndiyo yanayotokea, viso halali mwapewa,
Vipofu wanageuka, wazima walozaliwa.

Kitanzi wakitungua, na sasa wanakivaa,
Dahari wategemea, wataendelea kuwa,
Ila Muumba ajua, kwanini mchwa apaa,
Vipofu wanageuka, wazima walozaliwa.

Nani wa kumtegemea, kama hutotusikia,
Mola wetu unajua, moyoni yaliyojaa,
Bure kukusimulia, jamala twaingojea,
Vipofu wanageuka, wazima walozaliwa.

Mkuu uliyekuwa, wa mbinguni na dunia,
Gumu halijatokea, ukashindwa kutatua,
Yasubiri Tanzania, hukumu kuiridhia,
Vipofu wanageuka, wazima walozaliwa.

Birigiji

Kitamba kishachoka, imebaki mazoea,
Rangi inafutika, chazidi kufubaa,
Ukata umenishika, siwezi tena nunua,
Birigiji imechoka, njano imeshapotea!

Wale niliowashika, uchuro wanichulia,
Tayari wanshanizika, wangoja kunifukia,
Utajiri nilozika, waje kuufukua,
Birigiji imechoka, njano imeshapotea!

Miguu inachanika, magoti yanatitia,
Watu wakereheka, hawataki niangalia,
Na sasa nimeishika, dhana ya kunyanyapaa,
Birigiji imechoka, njano imeshapotea!

Ila siachi kucheka, kila nikiwaangalia,
Hukumu wanaoweka, hivi itanifikia,
Au wao kuwafika, nami nashuhudia?
Birigiji imechoka, njano imeshapotea!

Laiti ningebahatika, ukweli nikaujua,
Ni moja tu ningeshika, hadi juu nikapaa,
Ninabaki nateseka, johari sijavumbua,
Birigiji imechoka, njano imeshapotea!

Jaha haikunitaka, toka nilipozaliwa,
Kazi kushughulika, riziki kuokotea,
Zao halitaniweka, ila mwenyewe kuvua,
Birigiji imechoka, njano imeshapotea!